TRENDING NOW





Na Mwandishi Wetu.

Dar es Salaam-Tanzania, 17 Septemba 2026: Je, umekwama katika ufanyaji wa kazi ambayo unajua kabisa hiyo siyo kwa ajili yako, na umewahi kujiuliza kama kitu ambacho una uwezo nacho ni kile ambacho unakifanya kila siku ukiwa nyumbani, njiani au kwa ajili ya kujifurahisha tu, kinaweza kuwa zaidi ya burudani?

Serengeti Lite, kinywaji pendwa cha Kampuni ya vinywaji ya Serengeti, kwa kushirikiana na KUNTA Africa, wanataka kupata jibu la swali hilo, kwa kutangaza rasmi ujio wa awamu nyingine ya Nyota Bigi msimu wa pili, ambayo inalenga kusaka nyota mkubwa ajaye wa Tanzania, katika mikoa ya Dar es salaam, Mwanza, Arusha na Dodoma. Usaili utaanza jijini Dar es salaam kuanzia tarehe 3 Oktoba, tarehe 10 safari itaendelea katika mkoa wa Mwanza, Arusha tarehe 17, na Oktoba 24 itakuwa jijini Dodoma.

Msimu wa pili wa Nyota Bigi unatafuta waimbaji, wacheza mziki, waigizaji, wachekeshaji, wabunifu, wana mitindo, na vipaji vingine vya ubunifu ambavyo Tanzania bado haijavivumbua. Mpango huu ni sehemu ya Kampeni ya Serengeti Lite ya “Lite your Imagination” inayolenga kuwahamasisha vijana kuchukulia ubunifu wao kwa uzito, kujieleza na kuona kipaji chao kinaweza kuwafikisha wapi.

Akizungumza katika uzinduzi wa msimu wa pili wa Nyota Bigi jijini Dar es salaam, Mkurugenzi wa Masoko na Ubunifu wa Kampuni ya vinywaji ya Serengeti, Henry Esiaba, alisema jukwaa hili lipo kwa ajili ya kuthibitisha kwamba vipaji viko kila mahali na Nyota Bigi ipo wa ajili ya vipaji hivyo. 

“Tuna vipaji vingi katika kila kona ya nchi hii. Ila kinachokosekana wakati mwingine ni nafasi ya kuonekana. Nyota Bigi ipo kwa ajili ya kuwapa vijana wa Tanzania jukwaa hilo. Tumerudi kwa msimu wa pili, pamoja na washirika wetu KUNTA Africa, kwa sababu tunataka kugundua vipaji zaidi, kuviweka mbele ya hadhira kubwa na kuvipa msukumo unaostahili, popote vilipo,.” Alisema Esiaba.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Bia wa Kampuni ya vinywaji ya Serengeti, Rhona Namanya, amesema kuwa msimu huu wa pili ni mkubwa zaidi na kuwa wamejikita katika kutafuta vipaji mbalimbali katika miji zaidi Tanzania kulinganisha na msimu wa kwanza mwaka jana. 
“Mwaka huu tunafurahi kuwajulisha Watanzania kuwa msimu wa pili utakwenda katika miji mbalimbali Tanzania ukilinganisha na mwaka jana ambapo tulitafuta vipaji hapa Dar es Salaam tu.  Msimu huu wa pili tutakwenda kwenye miji mingine ikiwepo Arusha, Mwanza na Dodoma. Hii inaonyesha dhamira yetu ya kukuza vipaji zaidi hapa Tanzania.” Alisema Rhona.

Usajili tayari umefunguliwa kupitia msimbo wa QR wa Nyota Bigi, tovuti ya Nyota Bigi, WhatsApp au simu. Waombaji wanapaswa kuwa na umri wa miaka 18 hadi 35, kuwa na kitambulisho halali na kuwasilisha video fupi inayoonyesha kipaji chao. Usaili utafanyika ana kwa ana na mtandaoni, hivyo kutoa njia mbalimbali kwa wenye vipaji kujitokeza.

Kwa watakaofanikiwa kuvuka hatua hiyo, Nyota Bigi inatoa fursa ya kuingia katika tasnia pana ya ubunifu, huku nafasi zikiongezeka zaidi ya mashindano yenyewe. Washiriki wanaweza kupata fursa za kuunganishwa na maeneo mbalimbali ya masoko kupitia mitandao ya kijamii, uanamitindo, burudani, usimamizi wa vipaji na studio za kurekodi, na hivyo kupata nafasi yakufanikiwa zaidi.

Kwa Serengeti Lite, Nyota Bigi inaweka “Lite Your Imagination” katika vitendo kwa kuwapa vijana nafasi ya kutoka kwenye kufikiria tu kile wanachoweza kufanya na kuanza kukiweka wazi kupitia vipaji vyao. Jukwaa hili ni sehemu ya mwendelezo wa Serengeti Lite katika kukuza ubunifu wa vijana nchini Tanzania.

Mkuu wa Idara ya Masoko na Uwezeshaji, Vodacom Business, Joseph Sayi, akizungumza na wafanyabiashara wa rejareja wa bidhaa za Tanzania Breweries PLC (TBL) wakati wa semina ya kuwajengea uwezo kupitia Mpango wa Maendeleo ya Wafanyabiashara wa Rejareja (GRIT), iliyofanyika jijini Mwanza jana. Mafunzo hayo yaliyowashirikisha wafanyabiashara 150 yalilenga kuwaongezea ujuzi katika usimamizi wa biashara, fedha na matumizi ya suluhisho za kidijitali. Semina hiyo ni sehemu ya ushirikiano wa miaka miwili kati ya TBL na Vodacom Tanzania unaolenga kuwafikia zaidi ya wafanyabiashara 24,000  nchini.
Zaidi ya wafanyabiashara 150 jijini Mwanza leo wamefanya mafunzo yanayolenga kuwajengea uwezo ili kuwasaidia kuendesha biashara zao kwa ufanisi zaidi, kusimamia fedha na kuongeza faida, kupitia Mpango wa Maendeleo ya Wafanyabiashara wa Rejareja (GRIT) unaotekelezwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kwa ushirikiano na Vodacom Tanzania Plc yamewaleta pamoja wafanyabiashara kutoka maeneo mbalimbali ya jiji la Mwanza kwa ajili ya kujifunza namna ya kuboresha usimamizi wa biashara, ikiwemo kupanga matumizi ya fedha, kudhibiti bidhaa na kufanya maamuzi yanayoweza kusaidia biashara zao kukua.

Akifungua mafunzo hayo, Mkurugenzi Mtendaji wa TBL, Michelle Kilpin, alisema kuwa GRIT ni sehemu ya juhudi za kampuni hizo ili kuwawezesha wafanyabiashara wanaofanya kazi nazo kwa kuwapatia maarifa na ujuzi unaoweza kuwasaidia kusimamia biashara zao kwa ufanisi zaidi. Alisema uwezo wa kusimamia fedha, bidhaa na shughuli za kila siku ni muhimu katika kuweka biashara katika nafasi nzuri ya kukua na kuchangia maendeleo ya jamii.

Miongoni mwa wakufunzi katika mafunzo hayo ni Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) Dkt. Patrokil Kanje, aliyewafundisha washiriki namna ya kuendesha biashara kwa ufanisi, kusimamia gharama na kutambua maeneo yanayoweza kusaidia kuongeza faida.

Akizungumza katika mafunzo hayo, Dkt. Kanje aliwasisitiza wafanyabiashara kuwa na uelewa wa kina kuhusu biashara zao, hasa katika kufuatilia mauzo, gharama na faida. 
Alieleza kuwa mfanyabiashara anapaswa kufahamu si tu kiasi anachouza, bali pia gharama anazotumia na faida anayobaki nayo, kwa kuwa taarifa hizo ni muhimu katika kufanya maamuzi sahihi, kudhibiti matumizi na kupanga ukuaji wa biashara.

Kwa mfanyabiashara, changamoto ya kila siku si kuuza bidhaa pekee. Ni kuhakikisha fedha zinazopatikana zinatumika kwa uangalifu, bidhaa zinaendelea kuwepo, gharama zinasimamiwa na biashara inabaki na faida. 

Hivyo, mafunzo hayo yanaweka mkazo kwenye maarifa ambayo mfanyabiashara anaweza kuyatumia moja kwa moja katika biashara yake.Kwa upande wake Mkuu wa Idara ya Masoko na Uwezeshaji wa Vodacom Tanzania Plc Joseph Sayi, amewahimiza wafanyabiashara kutumia suluhisho za kidijitali katika shughuli zao za kila siku, akieleza kuwa teknolojia inaweza kurahisisha miamala, kusaidia usimamizi wa fedha na kuimarisha mawasiliano na wateja.

Sayi alisema matumizi sahihi ya suluhisho za kidijitali yanaweza kuwasaidia wafanyabiashara kurahisisha baadhi ya shughuli za biashara, kupata huduma kwa urahisi na kutumia taarifa katika kufanya maamuzi yanayolenga kuimarisha biashara zao.
Mafunzo haya ni sehemu ya mpango wa miaka miwili kati ya TBL na Vodacom Tanzania unaolenga kuwafikia zaidi ya wafanyabiashara 24,000 wa TBL nchini.

Kupitia GRIT, wafanyabiashara wanatarajiwa kupata ujuzi katika maeneo mbalimbali muhimu kwa uendeshaji wa biashara, ikiwemo usimamizi wa mtaji na mtiririko wa fedha, udhibiti wa bidhaa, huduma kwa wateja, ukuaji wa biashara pamoja na matumizi ya teknolojia na suluhisho za kidijitali.

Kwa wafanyabiashara walioshiriki jijini Mwanza, mafunzo hayo yanatoa fursa ya kuangalia biashara zao kwa mtazamo mpana zaidi, si kwa kuzingatia mauzo ya siku hiyo pekee, bali namna ya kujenga biashara inayoweza kusimamiwa vizuri, kukabiliana na changamoto na kukua kwa muda mrefu.

Mpango huo unatarajiwa kuendelea kuwafikia wafanyabiashara katika maeneo mbalimbali nchini, ukiweka mkazo katika kuwapa maarifa na zana zinazoweza kuwasaidia kufanya biashara kwa ufanisi zaidi katika mazingira yanayozidi kubadilika.
Tume ya Taifa ya UNESCO ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inashiriki katika Jukwaa la Nne la Kimataifa la Maadili ya Akili Unde linaloendelea mjini Riyadh, Saudi Arabia, likiwakutanisha wawakilishi kutoka nchi mbalimbali duniani kujadili namna ya kuhakikisha maendeleo na matumizi ya akili unde yanaongozwa na maadili, uwajibikaji na kuhudumia maslahi ya jamii.

Jukwaa hilo linatoa nafasi kwa nchi na wadau mbalimbali kubadilishana uzoefu na kujadili masuala yanayohusu mustakabali wa akili unde, ikiwemo namna ya kuimarisha mifumo ya sera na utawala, kujenga uwezo na kuhakikisha teknolojia hiyo inatumika kwa kuzingatia haki za binadamu, usalama, usawa na uwajibikaji.

Kwa Tume ya Taifa ya UNESCO, ushiriki huo ni sehemu ya kuendelea kuunganisha Tanzania na UNESCO katika mijadala na ajenda za kimataifa zinazohusu sayansi, teknolojia, elimu, utamaduni na maendeleo ya jamii.

Tume inawakilishwa katika jukwaa hilo na Bi Fides Mallya, Afisa Programu kutoka Sekta ya Sayansi Jamii ya Tume ya Taifa ya UNESCO ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, anayeshiriki katika shughuli na mijadala mbalimbali inayoendelea katika jukwaa hilo.

TUME YASHIRIKI MJADALA WA AFRIKA

Katika jukwaa hilo, Tume ya Taifa ya UNESCO inashiriki pia katika mjadalawa viongozi na wadau kutoka Afrika unaolenga kujadili namna bara hilo linavyoweza kuwezeshwa ili kunufaika kikamilifu na maendeleo ya teknolojia ya akili unde.

Mjadala huo unaangazia umuhimu wa Afrika kuimarisha uwezo wake katika sayansi, teknolojia, utafiti, ubunifu na ujuzi wa kidijitali, pamoja na kujenga mazingira bora ya kisera na kitaasisi yatakayowezesha matumizi salama na yenye tija ya akili unde.

Kwa kushiriki katika mjadala huo, Tume inaendelea kufuatilia mwelekeo wa kimataifa kuhusu akili unde na kuchangia katika mijadala inayolenga kuhakikisha maendeleo ya teknolojia hiyo yanazingatia mahitaji ya jamii na yanachangia maendeleo jumuishi na endelevu.

USHIRIKI WA TUME WAIUNGANISHA TANZANIA NA UNESCO

Ushiriki wa Tume katika jukwaa hilo unaonesha nafasi yake muhimu kama kiungo kati ya Tanzania na UNESCO, kwa kuwezesha ushiriki wa nchi katika mijadala, programu na ajenda za UNESCO katika ngazi ya kimataifa.

Kupitia majukwaa hayo, Tume inaendelea kufuatilia maendeleo na mwelekeo wa kimataifa katika maeneo ya UNESCO, kubadilishana uzoefu na nchi nyingine na kutafuta fursa za ushirikiano zinazoweza kuchangia maendeleo ya Tanzania.

Katika eneo la akili unde, ushiriki huo unaipa Tume fursa ya kufuatilia mijadala kuhusu maadili, utawala na matumizi yanayowajibika ya teknolojia hiyo, huku ikiendelea kuhusisha mijadala ya kimataifa na mahitaji ya maendeleo ya Tanzania.

UJUMBE WA TUME WAKUTANA NA BALOZI

Katika mwendelezo wa ushiriki wa Tume katika jukwaa hilo, ujumbe wa Tanzania unaoshiriki katika shughuli za jukwaa umepata fursa ya kufanya kikao na Balozi wa Tanzania nchini Saudi Arabia.

Kikao hicho kimekuwa fursa ya kubadilishana taarifa kuhusu ushiriki wa Tanzania katika jukwaa hilo na kuimarisha uratibu kati ya ujumbe wa Tanzania na Ubalozi wa Tanzania nchini Saudi Arabia katika masuala yanayohusu shughuli za kimataifa.

Jukwaa la Nne la Kimataifa la Maadili ya Akili Unde linaendelea mjini Riyadh likiwa sehemu ya juhudi za kimataifa za kuimarisha ushirikiano katika kuhakikisha maendeleo ya akili unde yanaenda sambamba na maadili, uwajibikaji, haki za binadamu na maendeleo jumuishi.
Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Jakaya Mrisho Kikwete, amemtembelea na kumpa pole Mbunge Mstaafu wa Jimbo la Nkasi, Mhe. Ally Mohamed Keissy, kufuatia msiba wa shimeji yake - dada wa mkewe uliotokea hivi karibuni.
Dkt Kikwete akioneshwa nyumba aliyowahi kuishi akiwa afisa wa CCM miaka ya 1980 alipomtembelea na kumpa pole Mbunge Mstaafu wa Jimbo la Nkasi, Mhe. Ally Mohamed Keissy, kufuatia msiba wa shimeji yake - dada wa mkewe uliotokea hivi karibuni.

Na Mwandishi Wetu.

Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Jakaya Mrisho Kikwete, amemtembelea na kumpa pole Mbunge Mstaafu wa Jimbo la Nkasi, Mhe. Ally Mohamed Keissy, kufuatia msiba wa shimeji yake - dada wa mkewe uliotokea hivi karibuni.

Dkt Kikwete alimtembelea Mhe. Keissy nyumbani kwake katika eneo la Cheyo, mjini Tabora, tarehe 14 Septemba 2026, muda mfupi baada ya kuhitimisha ziara yake ya kikazi ya siku nne mkoani Tabora.

Ziara hiyo ya kutoa pole ilikuwa pia na kumbukumbu ya pekee kwa Dkt Kikwete, kwani eneo la Cheyo si geni kwake. Yeye mwenyewe liwahi kuishi katika eneo hilo na jirani na nyumba ya Mhe. Keissy miaka ya 1980 alipokuwa akifanya kazi mkoani Tabora akiwa Afisa wa Chama Cha Mapinduzi (CCM).

Katika ziara hiyo, Dkt Kikwete aliambatana na Naibu Waziri, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, Dkt Jafaar Seif, pamoja na Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Mhe. Upendo Wella, ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Tabora.

Dkt Kikwete alimpa Mhe. Keissy na familia yake pole kwa msiba huo na kuwatakia moyo wa subira na faraja katika kipindi hiki cha majonzi.

Na Mwandishi Wetu

MWIMBAJI nyota wa Afro-pop kutoka Nigeria, Yemi Alade, ameachia album yake mpya yenye nyimbo 16 inayokwenda kwa jina ‘It’s Yemi Alade’, ikiwa ni kazi inayoadhimisha utambulisho wake, urithi wa Kiafrika na safari yake ya kimuziki.

Album hiyo inaunganisha mitindo mbalimbali ya muziki ikiwemo Afropop, Highlife, Afrobeats, R&B, Lingala, Dancehall na Afro House, huku Yemi Alade akitumia kazi hiyo kuonesha ukuaji wake kisanaa pamoja na mizizi iliyojenga safari yake ya muziki.

Kwa mujibu wa Yemi Alade, album hiyo ni kama barua ya mapenzi kwa mashabiki wake wa muda mrefu, huku ikiwa pia ni heshima kwa mizizi yake ya muziki wa Highlife na safari yake kuelekea hatua mpya za ubunifu.

“It’s Yemi Alade ni barua ya mapenzi kwa mashabiki wangu wakuu. Ni heshima kwa mizizi yangu ya Highlife, sherehe ya nilikotoka na uchunguzi wa ninakokwenda,” amesema Yemi Alade.

Amesema aliamua kuchanganya sauti za zamani, mpya na zilizokopwa kutoka katika mitindo mbalimbali ili kuunda kazi inayoheshimu misingi ya muziki wa Kiafrika huku ikiufikisha katika maeneo mapya ya ubunifu.
Album hiyo imewakutanisha wasanii mbalimbali kutoka Afrika, akiwemo Bien, Njerae na Sofiya Nzau kutoka Kenya; Singuila kutoka Ufaransa; Spyro, Don Jazzy, Jeriq na Teni kutoka Nigeria, pamoja na Ferre Gola wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).

Baadhi ya nyimbo zilizomo katika album hiyo ni Alhaja, General Market, Coco Na Yam akishirikiana na Ferre Gola, Yemi Mi Lova akiwa na Spyro, Ala Bekee akiwa na Don Jazzy, Owa, Minister of Enjoyment, Don’t Be Shy akiwa na Bien, Titanium, Earth Song akiwa na Sofiya Nzau na Njerae, Paradise akiwa na Singuila, pamoja na Away akiwa na Teni na Overtake akiwa na Jeriq.

Album hiyo pia ina nyimbo mbili za ziada, ambazo ni Worry akishirikiana na Fave na Ashawo (Sawa Sawa).

Kabla ya kuachia album hiyo, Yemi Alade tayari alikuwa ametoa baadhi ya nyimbo zilizotoa taswira ya kazi hiyo, ikiwemo Ala Bekee featuring Don Jazzy na Don’t Be Shy featuring Bien, ambayo imeendelea kupata mafanikio katika chati za muziki nchini Kenya na Afrika Mashariki.
Yemi Alade amesema jina la album hiyo lilipendekezwa na mashabiki baada ya kuwaomba kupitia mitandao ya kijamii kutoa mawazo kuhusu jina la album yake inayofuata.

Amesema jina ‘It’s Yemi Alade’ lilijitokeza mara kwa mara miongoni mwa mapendekezo ya mashabiki, jambo lililomfanya kulichagua na kulifanya kuwa sehemu ya uhusiano wake wa karibu na jamii inayofuatilia muziki wake.

Album hiyo imetolewa duniani kote kupitia Effyzzie Music.

Yemi Alade ni mwimbaji na mtunzi wa nyimbo kutoka Nigeria anayejulikana kimataifa kupitia nyimbo zake zikiwemo Johnny, huku akiwa amejenga jina kubwa katika muziki wa Afrika na kupata uteuzi na tuzo mbalimbali za kimataifa.

Mbali na muziki, Yemi Alade pia anajihusisha na shughuli za kijamii na ni Balozi wa Nia Njema wa UNDP, akishiriki katika juhudi za kuwawezesha vijana na kuchangia maendeleo ya jamii kupitia James and Helen Pathway Foundation.

Muasisi na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete Foundation (JMKF), Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, akiondoka leo Septemba 16, 2026 baada ya kuhitimisha ziara yake ya siku nne mkoani Tabora kwa kutembelea na kukagua zahanati pamoja na nyumba mbili za watumishi zilizojengwa katika Kijiji cha Gengesita, Kata ya Kizengi, Wilaya ya Uyui. Katika Uwanja wa ndege wa Tabora amesindikizwa na Naibu Waziri Ofisi ya Rais TAMISEMI, Dr Jafaar Seif na Mkuu wa Wilaya ya Urambo Dkt. Khamis Mkanachi na viongozi wengine wa wilaya na mkoa.
Dkt Kikwete akisalimiana na wafanyakazi wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege (TAA) wanaohiudumu katika Uwanja wa Ndege wa Tabora wakati akiondoka mwishoni mwa ziara yake ya siku nne ya mkoa huo leo Septemba 15, 2026.

Na Mwandishi Wetu, Tabora.

Tabora, 15 Septemba, 2026. Muasisi na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini wa Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete Foundation (JMKF), Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, amehitimisha ziara yake ya siku nne mkoani Tabora kwa kutembelea na kukagua zahanati pamoja na nyumba mbili za watumishi zilizojengwa katika Kijiji cha Gengesita, Kata ya Kizengi, Wilaya ya Uyui.

Ziara hiyo ilikuwa sehemu ya ufuatiliaji wa utekelezaji wa Mradi wa Jamii Salama unaotekelezwa na JMKF kupitia huduma za kliniki tembezi pamoja na ujenzi wa miundombinu ya afya katika maeneo ya
pembezoni.

Akizungumza na vyombo mbalimbali baada ya ziara hiyo, Dkt. Kikwete alisema ameridhishwa na utekelezaji wa mradi huo pamoja na kukamilika kwa ujenzi wa zahanati mbili ambazo sasa zimeanza kutoa huduma kwa wananchi. Aliishukuru Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa ushirikiano wake na JMKF katika utekelezaji wa miradi hiyo.

Dkt. Kikwete pia aliishukuru kampuni ya Marekani ya S.C. Johnson & Son, ambayo ndiyo imefadhili miradi hiyo, kwa mchango wake katika kuhakikisha huduma za afya zinawafikia wananchi wa maeneo ya pembezoni. 

Aidha, alizishukuru serikali za Mkoa wa Tabora pamoja na Wilaya za Uyui na Sikonge kwa ushirikiano waliouonesha tangu kuanza kwa utekelezaji wa miradi hiyo.

Kwa mujibu wa JMKF, kila zahanati imejengwa kwa lengo la kutoa huduma kamili za afya ya msingi, ikiwemo idara ya wagonjwa wa nje, kliniki ya afya ya uzazi na mtoto, wodi ya wazazi, vyoo vya umma, kichomea taka, mashimo maalumu kwa ajili ya kondo la nyuma pamoja na nyumba mbili za watumishi.

Hatua hiyo inalenga kuhakikisha huduma za afya zinapatikana karibu na wananchi, huku makazi ya watumishi yakitarajiwa kusaidia upatikanaji na ubaki wa wataalamu wa afya katika maeneo ya pembezoni, hususan wauguzi wakunga.

Kwa miaka mingi, umbali umekuwa kikwazo kikubwa kwa wakazi wa vijiji vya Gengesita, kilicho takribani kilomita 152 kutoka ofisi za Halmashauri ya Wilaya ya Uyui, na Ipembe, kilicho takribani kilomita 199 kutoka ofisi za Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge. Hali hiyo imekuwa changamoto zaidi kwa wajawazito, watoto, wazee na wagonjwa wanaohitaji huduma za haraka.

Ujenzi wa zahanati hizo unatokana na mafanikio ya Mradi wa Jamii Salama ambao JMKF iliuendesha mwanzoni mwa mwaka 2025 kupitia kliniki tembezi, ambapo mamia ya kina mama wajawazito walipatiwa huduma muhimu za afya bila malipo.

Baada ya kuona ukubwa wa mahitaji ya huduma za afya katika maeneo hayo, JMKF iliamua kujenga zahanati hizo ili kuweka msingi wa huduma za kudumu kwa jamii zilizo mbali na vituo vya afya vya wilaya na mkoa. JMKF inaendelea kushirikiana na Serikali, wadau wa maendeleo na sekta binafsi katika kuimarisha upatikanaji wa huduma bora za afya, hususan kwa jamii zilizo katika maeneo yenye changamoto ya umbali wa kufikia vituo vya kutolea huduma.
GEITA: Kwa vijana walio nje ya mfumo rasmi wa elimu, kukosa ajira si lazima kuwe na maana ya kukosa kabisa fursa za kufanya kazi; wakati mwingine changamoto kubwa ni kukosa maarifa na ujuzi unaowawezesha kuzitambua na kuzitumia fursa zilizopo.

Hilo ndilo linalolenga kushughulikiwa na Mradi wa BRIDGE Tanzania, unaotekelezwa na Tume ya Taifa ya UNESCO ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Korea Kusini, kwa kuwapatia vijana walio nje ya mfumo rasmi wa elimu elimu ya msingi na ujuzi wa vitendo unaoweza kuwawezesha kujiajiri na kushiriki katika shughuli za kiuchumi.

Katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita, vijana 210 tayari wamepatiwa mafunzo kupitia mradi huo, huku baadhi yao wakianza kutumia ujuzi walioupata katika uzalishaji wa bidhaa mbalimbali, zikiwemo sabuni za miche, sabuni za maji na vyakula vya mifugo.

Mafunzo hayo pia yanahusisha kusoma, kuandika, kuhesabu na ujasiriamali, yakilenga kuwajengea vijana uwezo unaoweza kutumika katika maisha yao na katika mazingira ya soko.

Akizungumza wakati wa kikao cha Kamati ya Uongozi ya Wilaya (District Steering Committee) ya Mradi wa BRIDGE Tanzania kilichofanyika Nzera, Geita, Mratibu Msaidizi wa Kitaifa wa mradi huo, Adriano Adrian Hyera, alisema hadi sasa vijana 210 katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita wamepatiwa mafunzo.

Alisema mradi huo unaweka mkazo katika kuwapa vijana fursa ya kupata maarifa na ujuzi ambao unaweza kuwasaidia kujenga uwezo wa kujitegemea.

“Lengo si kuwapa vijana mafunzo pekee, bali kuwajengea uwezo ambao wataweza kuutumia baada ya mafunzo ili kujipatia kipato na kujitegemea,” alisema Hyera.

Kwa mujibu wa muundo wa mradi, vijana ambao hawakupata fursa ya kukamilisha elimu ya msingi hupewa nafasi ya kujenga uwezo katika kusoma, kuandika na kuhesabu, kabla ya kuendelea na mafunzo ya ujuzi wa vitendo unaoendana na mazingira yao na fursa zinazopatikana katika soko.

Mtazamo huo unaweka msisitizo katika kuunganisha elimu na ujuzi wa vitendo, ili kijana anapomaliza mafunzo asiishie kuwa na maarifa ya darasani pekee, bali awe na uwezo wa kutumia ujuzi huo katika shughuli za uzalishaji na kujiajiri.

Katika utekelezaji wake Geita, mradi unawawezesha vijana kujifunza kwa vitendo na pia unatoa vifaa na mahitaji muhimu kwa ajili ya mafunzo, ili kuwapa nafasi ya kufanya mazoezi ya uzalishaji wakati wa kujifunza.

Baadhi ya vijana walionufaika na programu hiyo wamesema mafunzo yamewajengea uwezo wa kufanya shughuli mbalimbali za uzalishaji na kuwapa mtazamo mpya kuhusu namna wanavyoweza kutumia ujuzi wao kama njia ya kujipatia kipato.

Ujuzi huo unawapa pia nafasi ya kutengeneza bidhaa ambazo zinaweza kutumika katika jamii na, kwa kuzingatia ubora na mahitaji ya soko, kuwa sehemu ya shughuli zao za kiuchumi.

Kutoka elimu ya msingi hadi ujuzi wa soko

Kwa mtazamo wa mradi, elimu na ujuzi haviwekwi katika maeneo mawili tofauti, bali vinaunganishwa ili kumjengea kijana uwezo wa kutumia maarifa yake katika mazingira halisi.

Baada ya kujenga msingi wa kusoma, kuandika na kuhesabu, kijana hupewa ujuzi wa vitendo unaozingatia eneo analotoka na fursa zinazopatikana katika soko.

Hii inalenga kuwapa vijana ambao hawakumaliza elimu rasmi nafasi ya kupata ujuzi unaoweza kuwasaidia kushindana katika shughuli za kiuchumi pamoja na vijana wengine waliopitia njia rasmi za elimu na mafunzo ya ufundi.

Kwa maana hiyo, BRIDGE Tanzania inalenga kujenga daraja kati ya elimu, ujuzi na soko, badala ya kuishia katika utoaji wa mafunzo pekee.

Vijana wahimizwa kutumia fursa za mikopo

Akizungumzia hatua zinazofuata baada ya mafunzo, Hyera aliwashauri vijana kujiunga katika vikundi vya watu watano ili waweze kuchangamkia fursa za mikopo zinazotolewa na Halmashauri.

Alisema ushiriki katika vikundi unaweza kuwasaidia vijana kutumia ujuzi walioupata katika shughuli za kiuchumi na kutafuta fursa za kukuza shughuli zao.

Hatua hiyo inalenga kuhakikisha kuwa mafunzo wanayopata vijana yanaunganishwa na fursa za mitaji na uzalishaji, ili kuongeza uwezekano wa ujuzi huo kuleta matokeo katika maisha yao.

Majaribio yenye matarajio ya kupanuka

BRIDGE Tanzania ni mpango wa majaribio unaotekelezwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita, Halmashauri ya Wilaya ya Masasi na Kaskazini A Unguja.

Mradi una lengo la kuwafikia vijana 3,000 katika kipindi cha miaka mitano, sawa na takribani vijana 600 kila mwaka.

Majaribio hayo yanatoa nafasi ya kutathmini namna ya kuwaunganisha vijana walio nje ya mfumo rasmi wa elimu na elimu ya msingi, ujuzi wa vitendo na fursa za kiuchumi.

Matokeo na uzoefu unaopatikana katika maeneo ya utekelezaji utasaidia katika kutathmini namna mfumo huo unavyoweza kuimarishwa na, baada ya tathmini, kupanuliwa katika maeneo mengine nchini.

Tume ya UNESCO katika utekelezaji

Utekelezaji wa BRIDGE Tanzania unaenda sambamba na juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita za kuwawezesha vijana kupata maarifa, ujuzi na fursa za kushiriki katika shughuli za kiuchumi na maendeleo ya Taifa.

Kupitia Tume ya Taifa ya UNESCO, ushirikiano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Korea Kusini umegeuzwa kuwa fursa ya kuwafikia vijana ambao kwa sababu mbalimbali hawapo katika mfumo rasmi wa elimu.

Tume ya Taifa ya UNESCO, kwa jukumu lake la kuratibu, kutathmini na kufuatilia utekelezaji wa shughuli za UNESCO nchini, inaendelea kushirikiana na Serikali na wadau mbalimbali katika kuhakikisha programu zinazotekelezwa zinachangia mahitaji na vipaumbele vya maendeleo ya Tanzania.

Kwa BRIDGE Tanzania, msisitizo ni kuhakikisha kijana aliye nje ya mfumo rasmi hapotezi fursa ya kujenga uwezo. Badala yake, anapewa nafasi ya kujifunza, kupata ujuzi na kuutumia katika kujenga maisha yake.

Kikao cha Kamati ya Uongozi ya Wilaya kilichofanyika Nzera, Geita, kilitoa nafasi kwa wadau kupitia utekelezaji wa mradi, mafanikio, changamoto na hatua zinazoweza kuchukuliwa ili kuongeza manufaa yake kwa vijana.

Kwa vijana hao 210 wa Geita, safari inaanzia katika kujenga msingi wa elimu na ujuzi; lakini lengo kubwa ni kuwawezesha kutumia uwezo huo katika ulimwengu halisi wa kazi, uzalishaji na kujitegemea.
Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Jakaya Mrisho Kikwete, akiwa katika siku ya kwanza ya ziara yake ya kikazi ya siku nne mkoani Tabora, ametembelea Kitongoji cha Ipembe, Kata ya Kiloli, Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge, akikagua utekelezaji wa Mradi wa Jamii Salama (Safer Communities Project) unaotekelezwa na Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete (JMKF) kwa kushirikiana na Serikali.
 Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Jakaya Mrisho Kikwete, akikagua zahanati na nyumba mbili za watumishi Kitongoji cha Ipembe, Kata ya Kiloli, Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge, mkoa wa Tabora.
Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Jakaya Mrisho Kikwete, akipatiwa zawadi ya dumu la asali baada ya kukagua zahanati na nyumba mbili za watumishi Kitongoji cha Ipembe, Kata ya Kiloli, Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge, mkoa wa Tabora.
Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Jakaya Mrisho Kikwete, akiwa na kinamama wajawazito na wenye watoto waliojitokeza kwa wingi kupata huduma katika kliniki tembezi ya mradi wa Jamii Salama (Safer Communities Project) unaotekelezwa na Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete (JMKF) kwa kushirikiana na Serikali. Ameambatana na Naibu Waziri, Ofisi ya Rais–TAMISEMI, Dkt Jafar Seif; Naibu Katibu Mkuu katika Ofisi hiyo, Profesa Tumaini Nagu.
Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Jakaya Mrisho Kikwete, akiwa akiwagawia mifuko ya uzazi pamoja na vyandarua vyenye dawa kinamama wajawazito na wenye watoto waliojitokeza kwa wingi kupata huduma katika kliniki tembezi ya mradi wa Jamii Salama (Safer Communities Project) unaotekelezwa na Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete (JMKF) kwa kushirikiana na Serikali. Pamoja naye ni Naibu Waziri, Ofisi ya Rais–TAMISEMI, Dkt Jafar Seif; Naibu Katibu Mkuu katika Ofisi hiyo, Profesa Tumaini Nagu.
Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Jakaya Mrisho Kikwete, akiwa katika siku ya kwanza ya ziara yake ya kikazi ya siku nne mkoani Tabora, ametembelea Kitongoji cha Ipembe, Kata ya Kiloli, Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge, kujionea utekelezaji wa Mradi wa Jamii Salama (Safer Communities Project) unaotekelezwa na Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete (JMKF) kwa kushirikiana na Serikali.

Katika ziara hiyo ya 13 tarehe Septemba 2026, Dkt Kikwete, ambaye pia ni Muasisi na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya JMKF, alitembelea kliniki tembezi inayohudumia wananchi wa maeneo ya pembezoni kabla ya kukagua Zahanati mpya ya Ipembe pamoja na nyumba mbili za watumishi wa zahanati hiyo..

Uwekezaji huo umelenga kusogeza huduma muhimu za afya karibu zaidi na wananchi ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakisafiri umbali mrefu kufuata matibabu, huduma za wajawazito, afya ya mama na mtoto pamoja na huduma nyingine za msingi.

Dkt Kikwete aliambatana na Naibu Waziri, Ofisi ya Rais–TAMISEMI, Dkt Jafar Seif; Naibu Katibu Mkuu katika Ofisi hiyo, Profesa Tumaini Nagu; pamoja na viongozi mbalimbali wa Mkoa wa Tabora na Wilaya ya Sikonge.

Baada ya kukagua kliniki tembezi, zahanati na nyumba za watumishi, Dkt Kikwete alihutubia mkutano wa hadhara uliohudhuriwa na wananchi wa Ipembe na maeneo jirani, akisisitiza umuhimu wa kuendelea kusogeza huduma za msingi karibu na wananchi, hususan wanaoishi katika maeneo ya pembezoni.

Kwa wananchi wa Ipembe, ujio wa zahanati hiyo ni zaidi ya ongezeko la jengo la huduma za afya. Ni mwanzo wa kupungua kwa safari ndefu za kufuata matibabu, kuimarika kwa huduma kwa wajawazito na watoto, na uwezekano mkubwa zaidi wa kupata huduma kwa wakati.

Kwa JMKF, uwekezaji huo unaakisi dhamira kwamba mahali mtu anapoishi hapapaswi kuwa sababu ya kukosa huduma bora za afya. Ipembe sasa inakuwa mfano wa namna ushirikiano kati ya Serikali, taasisi na jamii unavyoweza kugeuza matumaini kuwa huduma halisi zinazogusa maisha ya wananchi.

Kwa furaha na shukrani zao, wananchi wa Ipembe walimzawadia Dkt Kikwete dumu lililojaa asali, zawadi lakini yenye ujumbe mkubwa wa ukarimu, heshima na furaha ya jamii inayoshuhudia huduma za afya zikisogezwa karibu zaidi na nyumbani.
KIZIMKAZI, ZANZIBAR — Mkurugenzi Mtendaji na Rais wa Kundi la Hanspaul, Satbir Singh Hanspaul, amefika Kizimkazi, Zanzibar, kutoa salamu za pole kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kufuatia kifo cha mume wake mpendwa, Marehemu Maalim Hafidh Ameir Hassan.

Hanspaul amefika katika makazi ya Rais Samia yaliyopo Kizimkazi, ambapo ametoa pole kwa Rais pamoja na familia yake kufuatia msiba huo.

Katika salamu zake za pole, Hanspaul amemuomba Mwenyezi Mungu ailaze roho ya Marehemu Maalim Hafidh Ameir Hassan mahali pema peponi, huku akimtakia Rais Samia pamoja na familia yake nguvu, subira na faraja katika kipindi hiki cha maombolezo.

Mkurugenzi wa Vodacom Business, Nguvu Kamando (kushoto) akimkabidhi zawadi ya ukumbusho Mkurugenzi Mtendaji wa Tanzania Breweries Limited (TBL) Bi. Michelle Kilpin (kulia) mara baada ya hafla ya kusainiwa kwa Makubaliano ya Ushirikiano (MoU) kati ya kampuni hizo mbili, iliyofanyika jijini Dar es Salaam, Septemba 11, 2026. Kupitia ushirikiano huo, zaidi ya wafanyabiashara 26,000 wa TBL nchini watanufaika na mafunzo ya biashara pamoja na suluhisho za kidijitali za Vodacom kupitia Mpango wa Maendeleo ya Wafanyabiashara wa Rejareja (Retailer Development Programme).

●Ushirikiano huu wa kimkakati utawawezesha wafanyabiashara wa TBL kupata suluhisho za kidijitali za Vodacom unatarajiwa kuzinduliwa rasmi jijini Mwanza Septemba 16.

Dar es Salaam, Septemba 11, 2026: Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) na Vodacom Tanzania PLC leo zimeingia makubaliano ya ushirikiano (MoU) ya muda wa miaka miwili, yenye lengo la kuimarisha uwezo wa wafanyabiashara nchini kupitia Mpango wa Maendeleo ya Wafanyabiashara wa Rejareja (Retailer Development Programme), uliobuniwa mahususi ili kuwapatia ujuzi wa vitendo katika usimamizi wa biashara, fedha na matumizi ya teknolojia vitakavyopelekea kukuza biashara zao.

Ukiendeshwa chini ya kaulimbiu ya ‘Growing Innovatively Together’ (GRIT), mpango huu unadhihirisha azma ya pamoja ya taasisi zote mbili za kuwasaidia wafanyabiashara wanaoshiriki kwa kiwango kikubwa katika mnyororo wa thamani wa TBL pamoja na mchango wao katika ukuaji wa uchumi wa nchi.

Akizungumza wakati wa hafla ya kusaini makubaliano hayo, Mkurugenzi wa Masuala ya Kisheria na Uhusiano wa Kampuni wa TBL Neema Temba, alisema ushirikiano huu unaonesha umuhimu wa kushirikiana katika kuimarisha uwezo wa wafanyabiashara na kuwawezesha kukua kwa muda mrefu.

"Kwa TBL, wafanyabiashara ni nguzo muhimu ya biashara na ukuaji wa uchumi. Kupitia ushirikiano na Vodacom Tanzania, tunawekeza katika ujuzi, teknolojia na uendelevu wa biashara ili kuwawezesha kukuza shughuli zao na kunufaika na fursa mpya. Hivyo tunajenga thamani inayonufaisha biashara, familia na jamii kote nchini,” alisema Bi Temba.


Ushirikiano huu utaunganisha mtandao mkubwa wa TBL wa zaidi ya wafanyabiashara 26,000 na uzoefu wa Vodacom katika mawasiliano, ubunifu wa kidijitali na huduma za kifedha kimtandao, kwa lengo la kuwasaidia wafanyabiashara kuboresha ufanisi, uimara na uendelevu wa biashara zao.

Kupitia mpango huo, wafanyabiashara watapatiwa mafunzo katika maeneo mbalimbali muhimu ya uendeshaji wa biashara, ikiwemo usimamizi wa biashara na fedha, mtiririko wa fedha, usimamizi wa bidhaa, mauzo na masoko, huduma kwa wateja, ujasiriamali, biashara inayozingatia uwajibikaji pamoja na matumizi ya teknolojia za kidijitali.

Mbali na mafunzo, washiriki watawezeshwa kupata uelewa na matumizi ya suluhisho za kidijitali na kifedha zinazoweza kuwasaidia kuongeza ufanisi wa biashara, kuboresha faida na kuimarisha mahusiano na wateja.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Vodacom Business, Nguvu Kamando, alisema ushirikiano huo ni sehemu ya dhamira ya Vodacom ya kutumia teknolojia na ubunifu kusaidia wafanyabiashara na kuchochea ukuaji wa biashara nchini.

"Biashara ndogo ni muhimili wa uchumi wa Tanzania. Kupitia ushirikiano wa TBL na Vodacom Tanzania, wafanyabiashara wanapatiwa zana, maarifa na teknolojia za kuboresha biashara, kuongeza tija na kufungua fursa za ukuaji endelevu. Kwa pamoja, tunachochea ujumuishaji wa kidijitali na kifedha, na kuwawezesha kustawi katika uchumi unaoongozwa na teknolojia,” alisema Bw Nguvu.

Katika utekelezaji wa mpango huo, Vodacom itawapatia wafanyabiashara fursa ya kufahamu na kutumia suluhisho mbalimbali za biashara na huduma za kidijitali, ikiwemo SME Bomba, M-Wekeza, Lipa kwa M-Pesa na M-Koba, zinazolenga kusaidia ujumuishaji wa huduma za kifedha, ufanisi wa biashara na matumizi ya teknolojia katika shughuli za kila siku.

Kadhalika, ushirikiano huu utakuza ubunifu, ujasiriamali na uwajibikaji katika biashara kupitia mafunzo ya ana kwa ana na majukwaa ya kidijitali. TBL na Vodacom Tanzania pia zitashirikiana katika mawasiliano, ushirikishwaji wa wadau, ufuatiliaji na tathmini ili kuhakikisha matokeo yanayopimika na yenye manufaa ya muda mrefu. Mafunzo ya kwanza chini ya Mpango wa Maendeleo ya Wafanyabiashara wa Rejareja yatafanyika Mwanza Septemba 16, yakiwapa wafanyabiashara ujuzi wa usimamizi wa biashara, fedha na matumizi ya teknolojia kwa ajili ya kuboresha utendaji na ukuaji endelevu. 

Kupitia ushirikiano huu, TBL na Vodacom zinaendelea kuimarisha ujasiriamali, matumizi ya huduma za kidijitali na kuwawezesha wafanyabiashara kuchangia ukuaji wa uchumi wa Tanzania.