

Mkuu wa Idara ya Masoko na Uwezeshaji wa Vodacom Business Joseph Sayi, akishiriki mashindano ya Vodacom Corporate Masters 2026 Golf Cup yaliyofanyika Lugalo Golf Club, Dar es Salaam, Septemba 5, 2026. Mashindano hayo yalishirikisha wachezaji gofu 150 kutoka Tanzania na nje ya nchi.
Na Mwandishi Wetu.
Dar es salaam, Septemba 5, 2026: Vodacom Tanzania PLC, kwa kushirikiana na Oakwood Holdings Limited, imehitimisha mashindano ya Vodacom Corporate Masters 2026 yaliyofanyika katika Uwanja wa TPDF Lugalo Golf Club, yakiwakutanisha wachezaji wapatao 150 kutoka Tanzania na nchi jirani, wakiwemo viongozi wa biashara, wakurugenzi na wakuu wa makampuni pamoja na wapenzi wa mchezo wa golf.
Wachezaji gofu Khalid Shemndolwa na Yvonne Ondari wameibuka washinda kwa jumla shindano la Vodacom Corporate Masters kwa upande wa wanaume na wanawake. Katika shindano hilo lililofanyika kwenye uwanja wa Lugalo, Shemndolwa alikusanya pointi 42 huku Ondari akikusanya pointi kama hizo katika mashindano hayo ya siku moja.
Mbali ya Shemndolwa na Ondari, Godfrey Abel aliibuka mhsindi katika daraja A, kwa kupata pointi 42, akifuatiwa na Likuli Juma aliyepata pointi 41 ambapo Sigfrid Urassa alitwaa ubingwa wa daraja B kwa pointi 40, akimzidi Godfrey Kilenga aliyemaliza na pointi hizo hizo, lakini Urassa akashinda kwa kanuni ya countback.
Boniface Japhet alitwaa ubingwa wa daraha C baada ya kupata pointi 39, huku Abdallah Singano akimaliza nafasi ya pili kwa pointi 37. Kwa upande wa wanawake, Neema Job alimaliza na pointi 42 na kutwaa ubingwa, akifuatiwa na Leticia Kapalia aliyepata pointi 40. Mashindano ya timu za kampuni nayo yalikuwa kivutio kikubwa, huku timu ya KQ ikiibuka mshindi baada ya kushindana na timu nyingine tisa za kampuni.
Zawadi maalum za mtu mmoja mmoja zilienda kwa Michael Norbert aliyeshinda Longest Drive kwa wanaume, huku Kapalia akitwaa tuzo hiyo kwa wanawake. Harshid Barmeda alishinda Nearest to the Pin kwa wanaume, wakati Vaileth James akitwaa tuzo hiyo kwa wanawake.
Mbali na ushindani, washiriki pamoja na familia zao walifurahia shughuli mbalimbali katika eneo la Corporate Village, lililokuwa na burudani, maonesho ya biashara, magari ya zamani pamoja na eneo maalum la watoto.
Mkurugenzi wa Vodacom Business wa Vodacom Tanzania PLC, Nguvu Kamando, alisema mashindano hayo yameendelea kuonyesha nafasi ya michezo katika kujenga mahusiano yenye tija katika biashara.
“Vodacom Corporate Masters 2026 Golf Cup imethibitisha tena kwamba michezo ni jukwaa lenye nguvu katika kujenga mahusiano ya muda mrefu ya kibiashara. Tunafurahishwa na ushiriki mkubwa wa kampuni na kasi ya mahusiano mapya yaliyojengwa wiki hii,” alisema Kamando.
Mwenyekiti wa Kamati ya Corporate Masters, Ken Kariuki, alizipongeza kampuni zilizoshiriki na kusema mashindano hayo yanaendelea kuchangia katika kujenga mtandao wa kibiashara na kukuza mchezo wa gofu.“Mwaka huu tulishuhudia ushindani wa kiwango cha juu uwanjani na ushiriki wenye maana katika biashara nje ya uwanja. Hilo ndilo lengo kuu la Corporate Masters, kuzikutanisha kampuni katika mazingira rafiki yanayozalisha fursa halisi za ushirikiano,” alisema Kariuki.
Alisema ushirikiano kati ya Vodacom na Corporate Masters unaonyesha namna kampuni zinavyoweza kufanya kazi pamoja katika kutengeneza thamani kwa wateja na wadau, huku zikiunga mkono maendeleo ya mchezo wa gofu nchini Tanzania.
Kufanikiwa kwa mashindano ya Vodacom Corporate Masters 2026 kunaendelea kuthibitisha mkakati wa Vodacom Tanzania wa kutumia michezo kama jukwaa la kuimarisha mahusiano ya kibiashara, kuhamasisha ubunifu na kuwasogeza karibu viongozi wa biashara na suluhisho za kidijitali zinazochochea ukuaji wa uchumi wa Tanzania.

Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) umeeleza dhamira ya kutumia nguvu ya majukwaa ya kidijitali kuwafikia wananchi wengi zaidi kwa elimu kuhusu hifadhi ya jamii, pensheni na uwekezaji, kupitia ushirikiano na Mtandao wa Wanablogu Tanzania (TBN).
Ushirikiano huo umejadiliwa wakati timu ya maofisa wa PSSSF ilipotembelea Makao Makuu ya Mtandao wa Wanablogu Tanzania (TBN) yaliyopo Kijitonyama, Dar es Salaam, ambapo pande hizo zilikubaliana kuimarisha ushirikiano katika utoaji wa taarifa sahihi na uelimishaji wa umma.
Mwenyekiti wa TBN, Beda Msimbe, alisema mtandao huo wenye zaidi ya wanachama 200 nchini na Diaspora una nafasi kubwa ya kusaidia taasisi mbalimbali kuwafikia wananchi kupitia majukwaa ya kidijitali.
Kilimanjaro-Tanzania: Kampuni ya Bia Serengeti (SBL) imeeleza mchango wa uwekezaji wa sekta binafsi katika mageuzi ya kiuchumi ya Tanzania wakati wa ziara ya wajumbe wa Kamati ya Kudumi ya Bunge ya Bajeti katika kiwanda chake Kilimanjaro-Moshi.
Ziara hiyo ilitoa fursa kwa kamati kujionea moja kwa moja uwekezaji wa SBL nchini Tanzania, mchango wake katika sekta ya viwanda na uchumi kwa ujumla, pamoja na hatua zinazounga mkono kilimo cha ndani, ajira, maendeleo ya ujuzi, jamii na uendelevu wa mazingira.
Mkutano huo umefanyika wakati Tanzania ikiendelea kutekeleza Dira 2050, ambayo inatambua sekta binafsi imara na yenye nguvu kama kichocheo muhimu cha mageuzi ya kiuchumi, tija, ubunifu, uwekezaji na uundwaji wa ajira.
Akizungumza wakati wa ziara hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Bia ya Serengeti, Dkt. Obinna Anyalebechi, alisema SBL inaona uwekezaji wake nchini Tanzania ukienda mbali zaidi ya shughuli zake za uzalishaji hadi kufikia mnyororo mzima wa thamani na jamii inazofanya nazo kazi.
"Tanzania inapoelekea 2050, sekta binafsi ina jukumu muhimu la kuhakikisha matarajio ya Dira 2050 ya nchi yetu yanageuka kuwa matokeo halisi. Kwa hiyo tumefurahi kuwakaribisha wajumbe wa Kamati ya Bunge ya Bajeti katika Kiwanda chetu cha Moshi na kuonyesha moja kwa moja uwekezaji tunaoufanya katika uzalishaji wa ndani, watu wetu, na mnyororo mpana wa thamani. Katika SBL, tunaendelea kujitolea kufanya kazi kwa ushirikiano na Serikali kuunga mkono ajenda ya viwanda ya Tanzania, kujenga na kuongeza ajira, kuimarisha minyororo ya thamani ya ndani, na kuchangia ukuaji endelevu wa kiuchumi," alisema Dkt. Anyalebechi.
Kwa miaka mingi, SBL imeendelea kuwekeza katika mnyororo wake wa thamani na katika mipango inayounga mkono vipaumbele vya maendeleo vya Tanzania. Kupitia mpango wake wa Shamba ni Mali, kampuni inasaidia wakulima wadogo wanaolima mazao muhimu ikiwemo mtama, shayiri na mahindi, ikiwa na lengo la kufikia wakulima 10,000 ifikapo mwaka 2030. Mpango huu unalenga kuimarisha tija ya kilimo huku ukijenga uhusiano thabiti zaidi kati ya kilimo cha ndani na uzalishaji viwandani.
Katika ziara hiyo SBL pia ilieleza kuwa imewekeza katika jamii kupitia mpango wake wa ‘Water for Life’. Tangu mwaka 2010, kampuni imetekeleza miradi 32 ya maji yenye thamani ya zaidi ya shilingi Bilioni 2, nakunufaisha zaidi ya Watanzania milioni mbili wanaoishi vijijini kwa kuwapatia maji safi na salama. Uwekezaji huu unaonyesha dhamira ya kampuni katika kushughulikia mahitaji ya jamii huku ikisaidia ustawi wa jamii na uchumi wa muda mrefu.
Aidha, kupitia mpango wake wa ‘Learning for Life’, unaotekelezwa kwa ushirikiano na Chuo cha Taifa cha Utalii (NCT), SBL imewasaidia vijana wa Kitanzania kupata ujuzi katika sekta ya hoteli na utalii unaolenga kuboresha nafasi zao za ajira na kuimarisha mnyororo wa thamani wa utalii na ukarimu nchini.Uendelevu unaendelea kuwa kiini cha mkakati wa uwekezaji wa muda mrefu wa SBL, huku kampuni ikiendelea kuzingatia matumizi bora ya maji, kilimo endelevu, nishati jadidifu, ufungashaji wa bidhaa na hatua nyingine zinazolenga kupunguza athari zake za kimazingira huku ikijenga biashara imara.
Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti Mhe. Mashimba Ndaki, alisema mkutano huo ulikuwa muhimu katika kuimarisha ushirikiano kati ya Bunge na sekta binafsi na kutambua mchango wa biashara katika kuunga mkono ajenda ya maendeleo ya Tanzania.
"Ziara hii imetoa fursa ya kuelewa moja kwa moja mchango wa uwekezaji wa sekta binafsi katika uzalishaji viwandani, ajira, minyororo ya thamani ya ndani na jamii. Tunapoelekea kutimiza matarajio ya Dira 2050, ushirikiano endelevu kati ya Serikali na sekta binafsi ni muhimu katika kujenga mazingira yanayowezesha uwekezaji, tija na ukuaji endelevu wa uchumi," Mhe. Ndaki.Ziara hiyo imethibitisha tena umuhimu wa ushirikiano kati ya Serikali na sekta binafsi katika kusukuma mbele matarajio ya maendeleo ya muda mrefu ya Tanzania. Kwa SBL, ziara hii pia imesisitiza dhamira yake endelevu ya kuwekeza nchini Tanzania na kujenga thamani ya pamoja kupitia watu wake, minyororo ya thamani ya ndani pamoja na jamii kwa ujumla.

Na Mwandishi Wetu, Tanga
Ujumbe kutoka International Fund for Agricultural Development (IFAD) pamoja na wataalamu kutoka sekta zinazotekeleza Programu ya Kuendeleza Kilimo na Uvuvi (AFDP), wamekutana mkoani Tanga kwa ajili ya kufanya mapitio ya utekelezaji wa programu hiyo na kutathmini mafanikio yaliyopatikana.
Timu hiyo pia inatarajiwa kutembelea maeneo mbalimbali yanayotekeleza AFDP mkoani Tanga, ikiwemo Kata ya Msomela katika Halmashauri ya Handeni Vijijini, ambako programu imehamasisha jamii ya Kimasai kushiriki katika kilimo bora.
Kupitia programu hiyo, jamii hiyo ambayo kwa asili ni wafugaji imeanza kujihusisha na kilimo cha mahindi chenye tija. Aidha, AFDP imewezesha kuanzishwa kwa mashamba darasa (FFS) kwa ajili ya mazao ya alizeti, mahindi na maharage.

Mashamba hayo yameonyesha mafanikio makubwa, ambapo hekta moja imekuwa na uwezo wa kuzalisha takribani magunia 20 ya mahindi, kila moja likiwa na uzito wa kilogramu 100. Hatua hiyo imewezesha jamii kupata chakula na kuongeza shughuli za kiuchumi kupitia kilimo.
Kwa upande wa sekta ya uvuvi, AFDP inaendelea na ujenzi wa Soko la Kimataifa la Samaki Kipumbwi katika Halmashauri ya Pangani. Ujenzi wa soko hilo umefikia asilimia 68 na unatarajiwa kukamilika ifikapo Oktoba 2026.

Programu hiyo pia inaendelea na ujenzi wa vichanja 40 vya kukaushia dagaa, ambavyo kwa pamoja vina uwezo wa kukaushia takribani tani tano za dagaa kwa wakati mmoja.
Aidha, AFDP inaendelea na ujenzi wa ghala la baridi pamoja na mtambo wa barafu katika soko hilo, hatua inayolenga kuboresha uhifadhi na usafirishaji wa samaki na kuongeza thamani ya mazao ya uvuvi.

Awali, Mkurugenzi Mkazi wa IFAD nchini, Seth Meng, alikutana na Kaimu Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga, Emmanuel Kisongo, na kufanya mazungumzo kuhusu utekelezaji wa programu hiyo mkoani humo pamoja na mafanikio yanayotarajiwa kwa wananchi wa maeneo yanayonufaika.
Kaimu Katibu Tawala huyo alisema AFDP ni muhimu katika kuchochea maendeleo ya sekta za kilimo na uvuvi mkoani Tanga, huku akiishukuru IFAD kwa juhudi za kuwafikia wananchi na kuomba uwekezaji zaidi uongezwe mkoani humo.














































