Kauli hiyo ilitolewa wakati wa Mkutano Mkuu wa Mwaka wa Wanahisa wa Africa50 na Jukwaa la Miundombinu la Afrika (Africa Infrastructure Forum), lililofanyika kwa siku mbili jijini Dar es Salaam, likiwakutanisha viongozi wa kisiasa, wataalamu wa masuala ya fedha na maendeleo kujadili namna taasisi za Afrika zinavyoweza kushirikiana kufadhili maendeleo ya bara, wakati ambapo uwekezaji wa kimataifa unazidi kuwa wa kuchagua.
Akizungumza katika kikao cha mjadala kilichokuwa na mada “Pace Setters: African-Designed, African-Led” (Waongoza Njia: Yaliyobuniwa na Kuongozwa na Waafrika), Mkurugenzi Mtendaji wa Stanbic Bank Tanzania, Manzi Rwegasira, alisema Afrika tayari ina taasisi imara za kifedha, lakini kinachohitajika sasa ni kuongeza uwezo wa taasisi hizo ili kukidhi mahitaji makubwa na yanayoongezeka ya miundombinu barani.

Alisema miundombinu ni kichocheo muhimu cha ukuaji wa uchumi kwa kuwa hurahisisha usafirishaji wa mazao ya kilimo na bidhaa nyingine, kuwezesha biashara ya kimataifa na kuchangia katika maendeleo ya uchumi kwa ujumla.
Kwa mujibu wa Manase, somo kubwa zaidi kutoka katika mkutano huo wa siku mbili ni umuhimu wa ushirikiano kati ya benki za biashara, taasisi za fedha za maendeleo, kampuni za bima, serikali na wawekezaji binafsi, kwa kuwa hakuna taasisi moja inayoweza kugharamia mahitaji ya muda mrefu ya miundombinu ya Afrika pekee.
“Jambo kubwa nililojifunza ni umuhimu wa ushirikiano. Kila mdau ana nafasi muhimu ya kutekeleza, lakini hakuna mmoja wetu anayeweza kufikia malengo haya peke yake,” alisema.
Manase alieleza kuwa ingawa benki za biashara zina nafasi muhimu katika ufadhili wa miundombinu, miradi hiyo inahitaji mitaji ya muda mrefu na yenye uvumilivu, ambayo inaweza kupatikana kupitia ushirikiano na taasisi za fedha za maendeleo pamoja na wawekezaji wa kitaasisi.
“Benki za biashara zinaweza kusaidia ufadhili wa miundombinu kwa kiwango fulani. Kwa kuwa hii ni uwekezaji wa muda mrefu, tunahitaji taasisi za fedha za maendeleo, kampuni za bima, pamoja na sekta ya umma na binafsi kufanya kazi kwa pamoja,” alisema.
Mtendaji huyo pia alisema Tanzania iko katika nafasi nzuri kimkakati ya kuwa lango kuu la usafirishaji na biashara kwa Afrika Mashariki, akitaja uwekezaji unaoendelea katika bandari, reli ya Standard Gauge Railway (SGR) na miundombinu ya barabara.
“Tanzania iko katika eneo la kimkakati sana. Tuna nchi jirani nane, ambapo sita kati ya hizo hazina bandari. Hii inatupa fursa ya kipekee ya kuwa kitovu cha ukanda huu,” alisema.
Kwa upande wake, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, alisema ufadhili wa miundombinu unapaswa hatimaye kuboresha maisha ya wananchi na hivyo kwenda sambamba na uwekezaji katika rasilimali watu.
Dkt. Kikwete alisema ongezeko la idadi ya vijana barani Afrika linaweza kuwa faida kubwa zaidi ya kiuchumi kwa bara hilo ikiwa serikali zitawekeza katika elimu bora, ukuzaji wa ujuzi na fursa za ajira.
Alisisitiza kuwa barabara, reli na miradi ya nishati haipaswi kuonekana kama mafanikio ya maendeleo yenyewe, bali kama nyenzo za kuongeza uzalishaji, kukuza biashara na kufikia ustawi wa pamoja.





























.jpeg)



.jpeg)




















