TRENDING NOW








Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameshuhudia uapisho wa Mheshimiwa Deogratius John Ndejembi kuwa Makamu wa Rais, na kumuasa kutekeleza dhamana hiyo kwa uzalendo, bidii, uadilifu na uwajibikaji.

Akizungumza katika hafla ya uapisho leo, tarehe 29 Agosti, 2026, Ikulu Chamwino, mkoani Dodoma, Rais Dkt. Samia amesema nafasi ya Makamu wa Rais inahitaji uongozi wenye kuunganisha watu, kusimamia utekelezaji wa shughuli za Serikali na kutanguliza maslahi ya Taifa.

“Cheo si ufalme, ni dhamana. Dhamana uliyopewa ni ya kuwatumikia Watanzania,” amesema Rais Dkt. Samia.

Rais Dkt. Samia amesema uzoefu wa Mheshimiwa Ndejembi katika nafasi mbalimbali alizowahi kushika Serikalini, pamoja na bidii, uwezo wa kujifunza, kufuatilia na kusimamia vyema dhamana anazopewa, unampa msingi mzuri wa kutekeleza wajibu wake mpya katika nafasi ya Makamu wa Rais.

Aidha, amemtaka Makamu wa Rais kuendelea kuimarisha umoja, mshikamano, ushirikiano na utulivu, huku akishirikiana na viongozi wengine katika kutekeleza majukumu ya Serikali.

Ameongeza kuwa, matarajio ya wananchi kuhusu maendeleo yanaweza kufikiwa kwa Serikali na viongozi wake kufanya kazi kwa ushirikiano, nidhamu na uongozi bora katika kila ngazi.

Rais Dkt. Samia amesema utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi pamoja na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 unahitaji uongozi unaosukuma matokeo na kutanguliza maslahi ya wananchi.

Katika hatua nyingine, Rais Dkt. Samia ameipongeza Kamati Kuu na Halmashauri Kuu ya Taifa ya Chama cha Mapinduzi kwa kuridhia jina la Mheshimiwa Ndejembi, akisema uteuzi wake umezingatia uwezo, uzoefu na sifa za kiuongozi.

Amesema umri wa Mheshimiwa Ndejembi unampa nafasi ya kutumia nguvu na maarifa yake katika kulitumikia Taifa, huku akimtaka kuendelea kujifunza na kukua katika majukumu yake mapya. Mheshimiwa Ndejembi ameapishwa kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania baada ya kuteuliwa na Chama cha Mapinduzi, na baadaye uteuzi wake kuthibitishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Na Janeth Raphael - MichuziTv -Ikulu Chamwino

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema uamuzi wa kumteua Deogratius Ndejembi kuwa Makamu wa Rais ulizingatia sifa, uzoefu na uwezo wake wa kubeba dhamana kubwa ya uongozi wa taifa.

Rais Samia amesema nafasi hiyo imekabidhiwa tena kwa kijana, akimtaka Ndejembi kutumia fursa hiyo kujifunza, kukua kiakili na kutekeleza majukumu yake kwa weledi, utii na uaminifu kwa maslahi ya Watanzania.

Akizungumza leo, Agosti 29, 2026, katika hafla ya kumuapisha Ndejembi kuwa Makamu wa Rais iliyofanyika Ikulu Chamwino, Dodoma, Rais Samia amesema uamuzi wa kumrudisha kijana katika nafasi hiyo ulifanyika kwa kauli moja.

“Kwa kauli moja tuliamua kuirudisha nafasi ya Makamu wa Rais kwa vijana na tuendelee kulea. Imetoka kwa kijana na tumeirudisha kwa kijana. Tunakuomba kijana (Ndejembi) ukakue sio kwa umri bali ukakue kiakili, tumekupa majukumu makubwa ni imani yangu utaweza,” amesema Rais Samia.

Rais Samia amesema Ndejembi alipata uungwaji mkono wa wabunge kwa kauli moja kutokana na sifa alizonazo zinazomfanya astahili kushika nafasi hiyo.

“Wabunge walimpitisha Deogratius Ndejembi kwa kauli moja kwa kuzingatia sifa za Makamu wetu wa Rais,” amesema.

Amesema kabla ya kufikia nafasi ya Makamu wa Rais, Ndejembi amewahi kushika nafasi mbalimbali za uongozi serikalini na katika sekta binafsi, akieleza kuwa uzoefu huo utakuwa nyenzo muhimu katika utekelezaji wa majukumu yake mapya.

“Makamu wa Rais Deogratius Ndejembi, kabla ya wadhifa huu, ulishika nafasi mbalimbali za uongozi serikalini na sekta binafsi. Sina shaka kwamba uzoefu huo utakusaidia kutekeleza majukumu ya dhamana hii uliyopewa,” amesema Rais Samia.

Kwa mujibu wa Rais Samia, hakuna shule maalumu inayomwandaa mtu kuwa Makamu wa Rais, bali uwezo wa kutekeleza majukumu hayo unajengwa kupitia sifa binafsi, bidii, weledi, nidhamu pamoja na utayari wa kujifunza na kusimamia utekelezaji wa majukumu.

Amesema sifa hizo zitamsaidia Ndejembi kutekeleza ipasavyo dhamana aliyopewa na taifa.

Rais Samia pia amesema uzoefu wa Ndejembi ndio uliowafanya viongozi kutokuwa na kusita katika kupitisha jina lake wakati wa kutafuta mtu wa kujaza nafasi hiyo.

“Kwa uzoefu huo ndio maana wakati tunatafuta mtu wa kujaza nafasi hii, hatukusita hata kidogo kupitisha jina lako. Hivyo ni matamanio na matarajio yetu sote Watanzania utalitumikia vyema, kwa utii, uaminifu, utu, busara, uzalendo, hekima, maarifa na uzoefu ulio nao, ukimtanguliza Mungu mbele na kwa maslahi ya taifa,” amesema.

Katika hatua nyingine, Rais Samia amemtaka Ndejembi kwenda kuwatumikia Watanzania wote bila kujali tofauti zao, akisisitiza umuhimu wa kiongozi kuweka mbele maslahi ya taifa.

“Nenda ukawatumikie Watanzania bila kujali tofauti zao,” amesema Rais Samia.

Rais Samia amesema serikali ina kazi kubwa ya kutekeleza ahadi zilizowekwa kupitia Ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM) ya mwaka 2025–2030, sambamba na kuanza utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya miaka 25 ijayo.

Amesema dira hiyo imebeba matarajio makubwa ya maendeleo kwa wananchi, hivyo utekelezaji wake unahitaji umoja, mshikamano, ushirikiano, utulivu na uongozi bora.

“Ili tuweze kutekeleza haya yote kwa maslahi ya wananchi wetu na taifa kwa ujumla, tunahitaji umoja, mshikamano, ushirikiano, utulivu na uongozi bora,” amesema.

Uapisho wa Ndejembi unafungua rasmi ukurasa mpya katika safari yake ya uongozi wa kitaifa, huku akianza kutekeleza majukumu ya Makamu wa Rais chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan
















RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amesema ni matamanio na matarajio ya Watanzania wote kwamba Makamu wa Rais, Deogratius Ndejembi, ataitumikia vyema Tanzania kwa utii, uaminifu, utu, busara, hekima, uzalendo na maarifa

Rais Samia ameyasema hayo leo Jumamosi, Agosti 29, 2026, Ikulu ya Chamwino, Dodoma, mara baada ya kumuapisha Ndejembi kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Amesema uteuzi wa Ndejembi umetokana na kuzingatia sifa na vigezo alivyo navyo, ikiwemo umri wake ambao, kwa mujibu wa Rais Samia, bado ni kijana mwenye nguvu, ari na kasi ya kujituma katika kutekeleza shughuli za Serikali.

“Nivishukuru vikao vya Chama cha Mapinduzi vya Kamati Kuu na Halmashauri Kuu kwa kupendekeza na kuridhia jina la Deogratius Ndejembi katika nafasi ya Makamu wa Rais,” amesema Rais Samia.

Amesema kwa kauli moja waliamua kuirudisha nafasi hiyo kwa vijana ili waendelee kulelewa katika uongozi, akimtaka Ndejembi akue kiakili kutokana na ukubwa wa majukumu aliyopewa.

Rais Samia amesema Ndejembi ana uzoefu wa uongozi serikalini na sekta binafsi, hivyo anaamini uzoefu huo utamsaidia kutekeleza majukumu ya dhamana hiyo.

“Cheo ni dhamana, cheo hiki tulichokupa sio ufalme ni dhamana. Ni dhamana uliyopewa na Watanzania kupitia Chama cha Mapinduzi lakini pia kupitia Bunge,” amesema.

Ametoa wito kwa Ndejembi kuwatumikia Watanzania bila kujali tofauti zao, huku akisisitiza umuhimu wa umoja, mshikamano, ushirikiano, utulivu na uongozi bora katika kutekeleza Ilani ya CCM ya 2025–2030 na Dira ya Maendeleo ya miaka 25 ijayo.

Rais Samia pia amewashukuru mabalozi na wakuu wa mashirika ya kimataifa waliohudhuria tukio hilo, akisema uwepo wao unaonesha urafiki, udugu na ushirikiano na Tanzania, pamoja na ushahidi wa uwezo wa nchi kubadilisha viongozi kwa amani na utulivu.

Na TAEC, Dodoma.

Kila mwaka tarehe 29 Agosti, dunia huadhimisha Siku ya Kimataifa ya Kupinga Majaribio ya Nyuklia (International Day against Nuclear Tests), ikiwa ni fursa ya kutafakari madhara yaliyosababishwa na majaribio ya silaha za nyuklia na kuendelea kuhimiza juhudi za kujenga dunia yenye amani na usalama.

Siku hii ilianzishwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mwaka 2009 kupitia Azimio Na. 64/35, kwa lengo la kuongeza uelewa kuhusu madhara ya majaribio ya silaha za nyuklia na umuhimu wa kuyasitisha. Tarehe 29 Agosti pia ina umuhimu wa kihistoria kutokana na kufungwa kwa eneo la majaribio ya nyuklia la Semipalatinsk nchini Kazakhstan mwaka 1991.

Tangu jaribio la kwanza la silaha ya nyuklia mwaka 1945, zaidi ya majaribio 2,000 yamefanyika duniani, yakiacha historia ya madhara kwa afya ya binadamu, mazingira na usalama wa dunia.

Katika kuadhimisha siku hii, Tume ya Nguvu za Atomu Tanzania (TAEC) inaungana na jumuiya ya kimataifa kupinga majaribio ya silaha za nyuklia na kusisitiza matumizi salama, yenye uwajibikaji na ya amani ya sayansi na teknolojia ya nyuklia.

Ni muhimu kuelewa kuwa kupinga majaribio ya silaha za nyuklia si kupinga teknolojia ya nyuklia. Teknolojia hii inapotumika kwa madhumuni ya amani na chini ya mifumo madhubuti ya usalama na udhibiti, ina mchango mkubwa katika kuboresha maisha na kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Nchini Tanzania, TAEC ina jukumu la kusimamia na kudhibiti matumizi salama ya vyanzo vya mionzi pamoja na kuhamasisha matumizi ya amani ya teknolojia ya nyuklia katika sekta mbalimbali zikiwemo afya, kilimo, mifugo, viwanda, migodi, maji, utafiti, mazingira na nishati.

Katika afya, teknolojia ya mionzi inatumika katika uchunguzi na matibabu ya magonjwa mbalimbali; katika kilimo na mifugo inachangia katika utafiti, uboreshaji wa uzalishaji na udhibiti wa baadhi ya wadudu na magonjwa. Mbinu za nyuklia pia zina matumizi muhimu katika tafiti za rasilimali za maji, viwanda, migodi na maeneo mengine ya maendeleo.

Kwa msingi huo, tunapaswa kutofautisha kati ya matumizi ya nyuklia kwa madhumuni ya kijeshi na matumizi yake kwa madhumuni ya amani. Hofu inayotokana na madhara ya silaha za nyuklia isiwe sababu ya kuiona teknolojia yote ya nyuklia kama tishio.

TAEC itaendelea kuhakikisha matumizi ya vyanzo vya mionzi nchini yanafanyika kwa kuzingatia sheria na viwango vya usalama ili kuwalinda wafanyakazi, wagonjwa, wananchi na mazingira. Tutaendelea pia kutoa elimu kwa umma ili kuondoa dhana potofu na kuongeza uelewa kuhusu manufaa ya matumizi salama ya teknolojia ya nyuklia.

Tunapoadhimisha Siku ya Kimataifa ya Kupinga Majaribio ya Nyuklia, tunatoa wito kwa wananchi kuendelea kupata taarifa sahihi na kuunga mkono matumizi salama na ya amani ya teknolojia ya nyuklia kwa manufaa ya Taifa na ustawi wa binadamu.

Ujumbe wetu ni wazi: HAPANA kwa majaribio ya silaha za nyuklia; NDIYO kwa matumizi salama na ya amani ya teknolojia ya nyuklia kwa maendeleo ya Taifa.

“Mionzi kwa Matumizi Salama na Teknolojia ya Nyuklia kwa Maendeleo ya Taifa.”

Na Lusungu Helela, Dodoma.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Ridhwani Kikwete, amesema uamuzi wa Serikali ya Somalia kumtuma Waziri mwenye dhamana ya Utumishi wa Umma nchini Tanzania ni ishara ya kutambua mafanikio yaliyofikiwa na Tanzania katika eneo la matumizi ya mifumo katika masuala ya Utumishi wa Umma nchini.

Mhe. Kikwete amesema hayo leo jijini Dodoma wakati akizungumza na ujumbe wa Serikali ya Somalia unaoongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Masuala ya Utumishi wa Umma, Hirsi Jama Ganni, uliofika nchini kwa ziara ya kikazi ya siku tatu.

Amesema ujio wa ujumbe huo unaonyesha kuwa Somalia inatambua na kuthamini uzoefu wa Tanzania katika uendeshaji wa Serikali, utumishi wa umma na matumizi ya mifumo ya kidijitali katika utoaji wa huduma kwa wananchi.

“Ukiona wenzako wanakufuata hasa katika eneo hili ambalo sisi ni watoa huduma, ni wazi kuwa huduma tunayotoa wapo wenzetu wanatambua na kuthamini tunachokifanya na ndiyo maana wameamua kuja kujifunza na kupata uzoefu,” amesema Mhe. Kikwete

Amesema anaamini uzoefu ambao Somalia itaupata kupitia ziara hiyo utasaidia kuboresha zaidi masuala ya utumishi wa umma nchini humo.

Mhe. Kikwete amesema ujumbe huo unapata fursa ya kujifunza maeneo mbalimbali, ikiwemo namna Serikali inavyohusiana na wananchi, uratibu wa masuala ya kazi na ajira, usalama wa wafanyakazi mahali pa kazi pamoja na mifumo ya pensheni kwa watumishi wanaostaafu katika taasisi za Serikali na sekta binafsi.

“Hii ziara ni kielelezo tosha kuwa Somalia imedhamiria, ndiyo maana haijaweza kutuma maafisa pekee, lakini Waziri mwenye dhamana ya Utumishi wa Umma ameamua kuja mwenyewe na timu yake kwa lengo la kujifunza na kuja kuona kwa macho yake kazi kubwa iliyofanyika Tanzania,” amesisitiza Mhe. Kikwete

Kwa upande wake, Mhe. Ganni amesema ujumbe wake umefika Tanzania kujifunza namna Tanzania ilivyofanikiwa katika masuala ya utumishi wa umma, hususan matumizi ya mifumo ya kidijitali katika kuboresha utoaji wa huduma.

Amesema Tanzania imekuwa ikifanya vizuri katika utoaji wa huduma kwa wananchi, huku watumishi wa umma wakitumia mifumo ya kidijitali kuwahudumia wananchi na kuhakikisha wanapata haki zao.

Mhe. Ganni amesema ujio wao ni muhimu kutokana na hatua ambazo Tanzania imepiga katika kuboresha utendaji wa Serikali na utoaji wa huduma kwa wananchi.

Amesema wamevutiwa pia na namna mifumo ya Serikali inavyowawezesha watumishi kuwahudumia wananchi kwa ufanisi.

Akizungumzia mfumo wa e-Mrejesho, Mhe.Ganni amesema ni miongoni mwa mifumo waliyoona ina umuhimu katika kuimarisha mawasiliano kati ya Serikali na wananchi, hivyo wanatarajia kujifunza namna unavyofanya kazi na uwezekano wa kutumia uzoefu huo katika kuboresha huduma nchini Somalia.

Ziara hiyo ya ujumbe wa Somalia inalenga pia kujifunza kuhusu mifumo ya Baraza la Mawaziri, usimamizi wa rasilimali watu, uajiri kwa kuzingatia sifa, Serikali mtandao, usimamizi wa ajira na mifumo ya taarifa za soko la ajira.

Ujumbe huo pia unatarajiwa kutembelea Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Mahusiano pamoja na Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma, kwa ajili ya kujionea namna shughuli za Serikali zinavyoratibiwa na kutekelezwa.
Na Janeth Raphael - MichuziTv - Bungeni Dodoma.

Waziri Mkuu Dkt Mwigulu Nchemba, amempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kwa uamuzi wa kumwona Deogratius Ndejembi kuwa miongoni mwa viongozi wanaoweza kumsaidia katika utekelezaji wa majukumu ya kitaifa, akielezwa kuwa msaidizi wake mpya katika nafasi ya Makamu wa Rais.

Dkt Mwigulu ametoa pongezi hizo leo Alhamisi, Agosti 27, 2026, wakati akijibu maswali ya papo kwa papo katika Bunge jijini Dodoma, akianza kwa kumpongeza Ndejembi ambaye amependekezwa kushika nafasi hiyo.

Ndejembi, ambaye ni Mbunge wa Chamwino mkoani Dodoma, alipendekezwa jana Jumatano, Agosti 26, 2026, na vikao vya Chama cha Mapinduzi (CCM) kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Pendekezo hilo limekuja baada ya Dk Emmanuel Nchimbi kujiuzulu nafasi ya Makamu wa Rais, hatua iliyokubaliwa na Rais Samia.

Kabla ya kupewa nafasi hiyo, Ndejembi alikuwa Waziri wa Nishati, nafasi aliyohudumu akisimamia masuala mbalimbali yanayohusu sekta ya nishati nchini.

Akizungumza Bungeni, Dkt. Mwigulu amemtakia Ndejembi mafanikio katika jukumu hilo jipya, huku akimpongeza Rais Samia kwa kumuamini na kumteua kuwa sehemu muhimu ya uongozi wa Serikali.

Uteuzi wa Ndejembi sasa unafungua ukurasa mpya katika uongozi wa Serikali, huku akitarajiwa kuendelea na majukumu ya kitaifa kwa nafasi yake mpya baada ya taratibu za kikatiba kukamilika.

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

Viongozi wapya wa Chama cha Waandishi Waendesha Ofisi Tanzania (TAPSEA) wameapishwa rasmi jijini Dar es Salaam, huku wakitakiwa kusimamia Katiba ya chama, kulinda maslahi ya wanachama na kuhakikisha wanatekeleza majukumu yao kwa uadilifu, uwajibikaji na mshikamano.

Uapisho huo umefanyika leo, Agosti 26, 2026, katika hafla iliyowakutanisha viongozi wa chama, wanachama pamoja na wageni mbalimbali, ikiwa ni hatua muhimu ya kuanza rasmi kwa kipindi kipya cha uongozi wa TAPSEA.

Akizungumza wakati wa kuwaapisha viongozi hao, Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Franco Kiswaga, aliwataka viongozi hao kuzingatia Katiba ya TAPSEA na kuitumia kama msingi wa kuwaongoza wanachama pamoja na kufanya maamuzi yenye maslahi kwa chama.
Mhe. Kiswaga amesema uongozi wa chama unahitaji umakini, hekima na uwezo wa kusimamia tofauti zinazoweza kujitokeza miongoni mwa wanachama, akisisitiza kuwa viongozi wanapaswa kuhakikisha changamoto zinatatuliwa kwa kufuata Katiba na taratibu zilizowekwa.

Amesema TAPSEA ni chama kikubwa chenye wajibu wa kuwatumikia wanachama wake, hivyo viongozi wapya wanapaswa kuwa imara katika kutetea na kusimamia maslahi yao, huku wakihakikisha chama kinaendelea kukua na kufikia malengo yaliyowekwa.

“Niwaombe viongozi mnapotoka hapa mkasimamie vyema Katiba yenu ili kuweza kuondoa migogoro itakayojitokeza,” amesema Kiswaga.
Aidha, Mhe. Kiswaga amewataka viongozi hao kuwa mfano kwa wanachama katika utekelezaji wa majukumu yao, akieleza kuwa uongozi bora hujengwa kupitia uwazi, ushirikishwaji na kuheshimu taratibu zinazokubalika ndani ya chama.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Taifa wa TAPSEA, Leah Mwamba, amewashukuru wanachama kwa kumpa dhamana ya kuwaongoza na kuahidi kufanya kazi kwa kushirikiana nao ili kuhakikisha chama kinafikia malengo yake.

Mwamba amesema tukio la uapisho ni hatua muhimu katika safari ya uongozi wa TAPSEA na kwamba dhamana waliyopewa viongozi hao inahitaji ushirikiano wa wanachama pamoja na wadau mbalimbali.
“Ninatoa shukrani zangu za pekee kwa wote walioungana nasi katika historia hii. Jambo hili la uapisho ni kubwa sana, hivyo tunaomba mzidi kutuombea tufanye vyema katika uongozi,” amesema Mwamba.

Amesema uongozi mpya utaendelea kusikiliza maoni ya wanachama na kutafuta njia zitakazosaidia kuimarisha umoja, mshikamano na maendeleo ya chama, huku ukizingatia majukumu na wajibu uliowekwa kupitia Katiba ya TAPSEA.

Naye Katibu Mkuu wa TAPSEA, Hellen Magati, amewashukuru wageni na wadau waliohudhuria hafla hiyo, akiahidi kuwa uongozi mpya utashirikiana na wanachama katika kutekeleza majukumu yake.
Magati amesema ushirikiano wa viongozi na wanachama ni muhimu katika kuhakikisha mipango ya chama inatekelezwa kwa ufanisi na changamoto zinazojitokeza zinapata ufumbuzi kwa wakati.

Amesisitiza kuwa uongozi mpya utazingatia misingi ya ushirikiano katika kuendeleza shughuli za TAPSEA na kuhakikisha wanachama wanapata nafasi ya kutoa maoni na kushiriki katika masuala yanayohusu maendeleo ya chama.

Viongozi wengine walioapishwa ni pamoja na Naibu Katibu Mkuu, Halima Twaha Mgulo, Makamu Mwenyekiti, Zainab Ibrahim Ally, Mweka Hazina, Nyanza Msongela, pamoja na wajumbe wengine waliochaguliwa katika uongozi huo.
Uapisho huo unatajwa kuwa hatua ya kukamilisha mchakato wa uchaguzi na kuweka rasmi uongozi mpya katika nafasi zao za kuwahudumia wanachama, huku matarajio yakiwa ni kuona chama kinaendelea kuimarisha umoja na kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.

Viongozi hao walioapishwa leo, Agosti 26, 2026, walichaguliwa katika Mkutano Mkuu wa 13 wa Chama cha Waandishi Waendesha Ofisi Tanzania (TAPSEA) uliofanyika mwishoni mwa mwezi Mei mwaka huu katika Ukumbi wa Kimataifa wa Mikutano wa Ngurdoto, mkoani Arusha.