TRENDING NOW





GEITA: Kwa vijana walio nje ya mfumo rasmi wa elimu, kukosa ajira si lazima kuwe na maana ya kukosa kabisa fursa za kufanya kazi; wakati mwingine changamoto kubwa ni kukosa maarifa na ujuzi unaowawezesha kuzitambua na kuzitumia fursa zilizopo.

Hilo ndilo linalolenga kushughulikiwa na Mradi wa BRIDGE Tanzania, unaotekelezwa na Tume ya Taifa ya UNESCO ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Korea Kusini, kwa kuwapatia vijana walio nje ya mfumo rasmi wa elimu elimu ya msingi na ujuzi wa vitendo unaoweza kuwawezesha kujiajiri na kushiriki katika shughuli za kiuchumi.

Katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita, vijana 210 tayari wamepatiwa mafunzo kupitia mradi huo, huku baadhi yao wakianza kutumia ujuzi walioupata katika uzalishaji wa bidhaa mbalimbali, zikiwemo sabuni za miche, sabuni za maji na vyakula vya mifugo.

Mafunzo hayo pia yanahusisha kusoma, kuandika, kuhesabu na ujasiriamali, yakilenga kuwajengea vijana uwezo unaoweza kutumika katika maisha yao na katika mazingira ya soko.

Akizungumza wakati wa kikao cha Kamati ya Uongozi ya Wilaya (District Steering Committee) ya Mradi wa BRIDGE Tanzania kilichofanyika Nzera, Geita, Mratibu Msaidizi wa Kitaifa wa mradi huo, Adriano Adrian Hyera, alisema hadi sasa vijana 210 katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita wamepatiwa mafunzo.

Alisema mradi huo unaweka mkazo katika kuwapa vijana fursa ya kupata maarifa na ujuzi ambao unaweza kuwasaidia kujenga uwezo wa kujitegemea.

“Lengo si kuwapa vijana mafunzo pekee, bali kuwajengea uwezo ambao wataweza kuutumia baada ya mafunzo ili kujipatia kipato na kujitegemea,” alisema Hyera.

Kwa mujibu wa muundo wa mradi, vijana ambao hawakupata fursa ya kukamilisha elimu ya msingi hupewa nafasi ya kujenga uwezo katika kusoma, kuandika na kuhesabu, kabla ya kuendelea na mafunzo ya ujuzi wa vitendo unaoendana na mazingira yao na fursa zinazopatikana katika soko.

Mtazamo huo unaweka msisitizo katika kuunganisha elimu na ujuzi wa vitendo, ili kijana anapomaliza mafunzo asiishie kuwa na maarifa ya darasani pekee, bali awe na uwezo wa kutumia ujuzi huo katika shughuli za uzalishaji na kujiajiri.

Katika utekelezaji wake Geita, mradi unawawezesha vijana kujifunza kwa vitendo na pia unatoa vifaa na mahitaji muhimu kwa ajili ya mafunzo, ili kuwapa nafasi ya kufanya mazoezi ya uzalishaji wakati wa kujifunza.

Baadhi ya vijana walionufaika na programu hiyo wamesema mafunzo yamewajengea uwezo wa kufanya shughuli mbalimbali za uzalishaji na kuwapa mtazamo mpya kuhusu namna wanavyoweza kutumia ujuzi wao kama njia ya kujipatia kipato.

Ujuzi huo unawapa pia nafasi ya kutengeneza bidhaa ambazo zinaweza kutumika katika jamii na, kwa kuzingatia ubora na mahitaji ya soko, kuwa sehemu ya shughuli zao za kiuchumi.

Kutoka elimu ya msingi hadi ujuzi wa soko

Kwa mtazamo wa mradi, elimu na ujuzi haviwekwi katika maeneo mawili tofauti, bali vinaunganishwa ili kumjengea kijana uwezo wa kutumia maarifa yake katika mazingira halisi.

Baada ya kujenga msingi wa kusoma, kuandika na kuhesabu, kijana hupewa ujuzi wa vitendo unaozingatia eneo analotoka na fursa zinazopatikana katika soko.

Hii inalenga kuwapa vijana ambao hawakumaliza elimu rasmi nafasi ya kupata ujuzi unaoweza kuwasaidia kushindana katika shughuli za kiuchumi pamoja na vijana wengine waliopitia njia rasmi za elimu na mafunzo ya ufundi.

Kwa maana hiyo, BRIDGE Tanzania inalenga kujenga daraja kati ya elimu, ujuzi na soko, badala ya kuishia katika utoaji wa mafunzo pekee.

Vijana wahimizwa kutumia fursa za mikopo

Akizungumzia hatua zinazofuata baada ya mafunzo, Hyera aliwashauri vijana kujiunga katika vikundi vya watu watano ili waweze kuchangamkia fursa za mikopo zinazotolewa na Halmashauri.

Alisema ushiriki katika vikundi unaweza kuwasaidia vijana kutumia ujuzi walioupata katika shughuli za kiuchumi na kutafuta fursa za kukuza shughuli zao.

Hatua hiyo inalenga kuhakikisha kuwa mafunzo wanayopata vijana yanaunganishwa na fursa za mitaji na uzalishaji, ili kuongeza uwezekano wa ujuzi huo kuleta matokeo katika maisha yao.

Majaribio yenye matarajio ya kupanuka

BRIDGE Tanzania ni mpango wa majaribio unaotekelezwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita, Halmashauri ya Wilaya ya Masasi na Kaskazini A Unguja.

Mradi una lengo la kuwafikia vijana 3,000 katika kipindi cha miaka mitano, sawa na takribani vijana 600 kila mwaka.

Majaribio hayo yanatoa nafasi ya kutathmini namna ya kuwaunganisha vijana walio nje ya mfumo rasmi wa elimu na elimu ya msingi, ujuzi wa vitendo na fursa za kiuchumi.

Matokeo na uzoefu unaopatikana katika maeneo ya utekelezaji utasaidia katika kutathmini namna mfumo huo unavyoweza kuimarishwa na, baada ya tathmini, kupanuliwa katika maeneo mengine nchini.

Tume ya UNESCO katika utekelezaji

Utekelezaji wa BRIDGE Tanzania unaenda sambamba na juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita za kuwawezesha vijana kupata maarifa, ujuzi na fursa za kushiriki katika shughuli za kiuchumi na maendeleo ya Taifa.

Kupitia Tume ya Taifa ya UNESCO, ushirikiano wa Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Korea Kusini umegeuzwa kuwa fursa ya kuwafikia vijana ambao kwa sababu mbalimbali hawapo katika mfumo rasmi wa elimu.

Tume ya Taifa ya UNESCO, kwa jukumu lake la kuratibu, kutathmini na kufuatilia utekelezaji wa shughuli za UNESCO nchini, inaendelea kushirikiana na Serikali na wadau mbalimbali katika kuhakikisha programu zinazotekelezwa zinachangia mahitaji na vipaumbele vya maendeleo ya Tanzania.

Kwa BRIDGE Tanzania, msisitizo ni kuhakikisha kijana aliye nje ya mfumo rasmi hapotezi fursa ya kujenga uwezo. Badala yake, anapewa nafasi ya kujifunza, kupata ujuzi na kuutumia katika kujenga maisha yake.

Kikao cha Kamati ya Uongozi ya Wilaya kilichofanyika Nzera, Geita, kilitoa nafasi kwa wadau kupitia utekelezaji wa mradi, mafanikio, changamoto na hatua zinazoweza kuchukuliwa ili kuongeza manufaa yake kwa vijana.

Kwa vijana hao 210 wa Geita, safari inaanzia katika kujenga msingi wa elimu na ujuzi; lakini lengo kubwa ni kuwawezesha kutumia uwezo huo katika ulimwengu halisi wa kazi, uzalishaji na kujitegemea.
Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Jakaya Mrisho Kikwete, akiwa katika siku ya kwanza ya ziara yake ya kikazi ya siku nne mkoani Tabora, ametembelea Kitongoji cha Ipembe, Kata ya Kiloli, Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge, akikagua utekelezaji wa Mradi wa Jamii Salama (Safer Communities Project) unaotekelezwa na Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete (JMKF) kwa kushirikiana na Serikali.
 Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Jakaya Mrisho Kikwete, akikagua zahanati na nyumba mbili za watumishi Kitongoji cha Ipembe, Kata ya Kiloli, Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge, mkoa wa Tabora.
Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Jakaya Mrisho Kikwete, akipatiwa zawadi ya dumu la asali baada ya kukagua zahanati na nyumba mbili za watumishi Kitongoji cha Ipembe, Kata ya Kiloli, Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge, mkoa wa Tabora.
Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Jakaya Mrisho Kikwete, akiwa na kinamama wajawazito na wenye watoto waliojitokeza kwa wingi kupata huduma katika kliniki tembezi ya mradi wa Jamii Salama (Safer Communities Project) unaotekelezwa na Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete (JMKF) kwa kushirikiana na Serikali. Ameambatana na Naibu Waziri, Ofisi ya Rais–TAMISEMI, Dkt Jafar Seif; Naibu Katibu Mkuu katika Ofisi hiyo, Profesa Tumaini Nagu.
Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Jakaya Mrisho Kikwete, akiwa akiwagawia mifuko ya uzazi pamoja na vyandarua vyenye dawa kinamama wajawazito na wenye watoto waliojitokeza kwa wingi kupata huduma katika kliniki tembezi ya mradi wa Jamii Salama (Safer Communities Project) unaotekelezwa na Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete (JMKF) kwa kushirikiana na Serikali. Pamoja naye ni Naibu Waziri, Ofisi ya Rais–TAMISEMI, Dkt Jafar Seif; Naibu Katibu Mkuu katika Ofisi hiyo, Profesa Tumaini Nagu.
Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt Jakaya Mrisho Kikwete, akiwa katika siku ya kwanza ya ziara yake ya kikazi ya siku nne mkoani Tabora, ametembelea Kitongoji cha Ipembe, Kata ya Kiloli, Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge, kujionea utekelezaji wa Mradi wa Jamii Salama (Safer Communities Project) unaotekelezwa na Taasisi ya Jakaya Mrisho Kikwete (JMKF) kwa kushirikiana na Serikali.

Katika ziara hiyo ya 13 tarehe Septemba 2026, Dkt Kikwete, ambaye pia ni Muasisi na Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya JMKF, alitembelea kliniki tembezi inayohudumia wananchi wa maeneo ya pembezoni kabla ya kukagua Zahanati mpya ya Ipembe pamoja na nyumba mbili za watumishi wa zahanati hiyo..

Uwekezaji huo umelenga kusogeza huduma muhimu za afya karibu zaidi na wananchi ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakisafiri umbali mrefu kufuata matibabu, huduma za wajawazito, afya ya mama na mtoto pamoja na huduma nyingine za msingi.

Dkt Kikwete aliambatana na Naibu Waziri, Ofisi ya Rais–TAMISEMI, Dkt Jafar Seif; Naibu Katibu Mkuu katika Ofisi hiyo, Profesa Tumaini Nagu; pamoja na viongozi mbalimbali wa Mkoa wa Tabora na Wilaya ya Sikonge.

Baada ya kukagua kliniki tembezi, zahanati na nyumba za watumishi, Dkt Kikwete alihutubia mkutano wa hadhara uliohudhuriwa na wananchi wa Ipembe na maeneo jirani, akisisitiza umuhimu wa kuendelea kusogeza huduma za msingi karibu na wananchi, hususan wanaoishi katika maeneo ya pembezoni.

Kwa wananchi wa Ipembe, ujio wa zahanati hiyo ni zaidi ya ongezeko la jengo la huduma za afya. Ni mwanzo wa kupungua kwa safari ndefu za kufuata matibabu, kuimarika kwa huduma kwa wajawazito na watoto, na uwezekano mkubwa zaidi wa kupata huduma kwa wakati.

Kwa JMKF, uwekezaji huo unaakisi dhamira kwamba mahali mtu anapoishi hapapaswi kuwa sababu ya kukosa huduma bora za afya. Ipembe sasa inakuwa mfano wa namna ushirikiano kati ya Serikali, taasisi na jamii unavyoweza kugeuza matumaini kuwa huduma halisi zinazogusa maisha ya wananchi.

Kwa furaha na shukrani zao, wananchi wa Ipembe walimzawadia Dkt Kikwete dumu lililojaa asali, zawadi lakini yenye ujumbe mkubwa wa ukarimu, heshima na furaha ya jamii inayoshuhudia huduma za afya zikisogezwa karibu zaidi na nyumbani.
KIZIMKAZI, ZANZIBAR — Mkurugenzi Mtendaji na Rais wa Kundi la Hanspaul, Satbir Singh Hanspaul, amefika Kizimkazi, Zanzibar, kutoa salamu za pole kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kufuatia kifo cha mume wake mpendwa, Marehemu Maalim Hafidh Ameir Hassan.

Hanspaul amefika katika makazi ya Rais Samia yaliyopo Kizimkazi, ambapo ametoa pole kwa Rais pamoja na familia yake kufuatia msiba huo.

Katika salamu zake za pole, Hanspaul amemuomba Mwenyezi Mungu ailaze roho ya Marehemu Maalim Hafidh Ameir Hassan mahali pema peponi, huku akimtakia Rais Samia pamoja na familia yake nguvu, subira na faraja katika kipindi hiki cha maombolezo.

Mkurugenzi wa Vodacom Business, Nguvu Kamando (kushoto) akimkabidhi zawadi ya ukumbusho Mkurugenzi Mtendaji wa Tanzania Breweries Limited (TBL) Bi. Michelle Kilpin (kulia) mara baada ya hafla ya kusainiwa kwa Makubaliano ya Ushirikiano (MoU) kati ya kampuni hizo mbili, iliyofanyika jijini Dar es Salaam, Septemba 11, 2026. Kupitia ushirikiano huo, zaidi ya wafanyabiashara 26,000 wa TBL nchini watanufaika na mafunzo ya biashara pamoja na suluhisho za kidijitali za Vodacom kupitia Mpango wa Maendeleo ya Wafanyabiashara wa Rejareja (Retailer Development Programme).

●Ushirikiano huu wa kimkakati utawawezesha wafanyabiashara wa TBL kupata suluhisho za kidijitali za Vodacom unatarajiwa kuzinduliwa rasmi jijini Mwanza Septemba 16.

Dar es Salaam, Septemba 11, 2026: Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) na Vodacom Tanzania PLC leo zimeingia makubaliano ya ushirikiano (MoU) ya muda wa miaka miwili, yenye lengo la kuimarisha uwezo wa wafanyabiashara nchini kupitia Mpango wa Maendeleo ya Wafanyabiashara wa Rejareja (Retailer Development Programme), uliobuniwa mahususi ili kuwapatia ujuzi wa vitendo katika usimamizi wa biashara, fedha na matumizi ya teknolojia vitakavyopelekea kukuza biashara zao.

Ukiendeshwa chini ya kaulimbiu ya ‘Growing Innovatively Together’ (GRIT), mpango huu unadhihirisha azma ya pamoja ya taasisi zote mbili za kuwasaidia wafanyabiashara wanaoshiriki kwa kiwango kikubwa katika mnyororo wa thamani wa TBL pamoja na mchango wao katika ukuaji wa uchumi wa nchi.

Akizungumza wakati wa hafla ya kusaini makubaliano hayo, Mkurugenzi wa Masuala ya Kisheria na Uhusiano wa Kampuni wa TBL Neema Temba, alisema ushirikiano huu unaonesha umuhimu wa kushirikiana katika kuimarisha uwezo wa wafanyabiashara na kuwawezesha kukua kwa muda mrefu.

"Kwa TBL, wafanyabiashara ni nguzo muhimu ya biashara na ukuaji wa uchumi. Kupitia ushirikiano na Vodacom Tanzania, tunawekeza katika ujuzi, teknolojia na uendelevu wa biashara ili kuwawezesha kukuza shughuli zao na kunufaika na fursa mpya. Hivyo tunajenga thamani inayonufaisha biashara, familia na jamii kote nchini,” alisema Bi Temba.


Ushirikiano huu utaunganisha mtandao mkubwa wa TBL wa zaidi ya wafanyabiashara 26,000 na uzoefu wa Vodacom katika mawasiliano, ubunifu wa kidijitali na huduma za kifedha kimtandao, kwa lengo la kuwasaidia wafanyabiashara kuboresha ufanisi, uimara na uendelevu wa biashara zao.

Kupitia mpango huo, wafanyabiashara watapatiwa mafunzo katika maeneo mbalimbali muhimu ya uendeshaji wa biashara, ikiwemo usimamizi wa biashara na fedha, mtiririko wa fedha, usimamizi wa bidhaa, mauzo na masoko, huduma kwa wateja, ujasiriamali, biashara inayozingatia uwajibikaji pamoja na matumizi ya teknolojia za kidijitali.

Mbali na mafunzo, washiriki watawezeshwa kupata uelewa na matumizi ya suluhisho za kidijitali na kifedha zinazoweza kuwasaidia kuongeza ufanisi wa biashara, kuboresha faida na kuimarisha mahusiano na wateja.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Vodacom Business, Nguvu Kamando, alisema ushirikiano huo ni sehemu ya dhamira ya Vodacom ya kutumia teknolojia na ubunifu kusaidia wafanyabiashara na kuchochea ukuaji wa biashara nchini.

"Biashara ndogo ni muhimili wa uchumi wa Tanzania. Kupitia ushirikiano wa TBL na Vodacom Tanzania, wafanyabiashara wanapatiwa zana, maarifa na teknolojia za kuboresha biashara, kuongeza tija na kufungua fursa za ukuaji endelevu. Kwa pamoja, tunachochea ujumuishaji wa kidijitali na kifedha, na kuwawezesha kustawi katika uchumi unaoongozwa na teknolojia,” alisema Bw Nguvu.

Katika utekelezaji wa mpango huo, Vodacom itawapatia wafanyabiashara fursa ya kufahamu na kutumia suluhisho mbalimbali za biashara na huduma za kidijitali, ikiwemo SME Bomba, M-Wekeza, Lipa kwa M-Pesa na M-Koba, zinazolenga kusaidia ujumuishaji wa huduma za kifedha, ufanisi wa biashara na matumizi ya teknolojia katika shughuli za kila siku.

Kadhalika, ushirikiano huu utakuza ubunifu, ujasiriamali na uwajibikaji katika biashara kupitia mafunzo ya ana kwa ana na majukwaa ya kidijitali. TBL na Vodacom Tanzania pia zitashirikiana katika mawasiliano, ushirikishwaji wa wadau, ufuatiliaji na tathmini ili kuhakikisha matokeo yanayopimika na yenye manufaa ya muda mrefu. Mafunzo ya kwanza chini ya Mpango wa Maendeleo ya Wafanyabiashara wa Rejareja yatafanyika Mwanza Septemba 16, yakiwapa wafanyabiashara ujuzi wa usimamizi wa biashara, fedha na matumizi ya teknolojia kwa ajili ya kuboresha utendaji na ukuaji endelevu. 

Kupitia ushirikiano huu, TBL na Vodacom zinaendelea kuimarisha ujasiriamali, matumizi ya huduma za kidijitali na kuwawezesha wafanyabiashara kuchangia ukuaji wa uchumi wa Tanzania.
Washirika wa Nyerere Cycling Tour, wakiongozwa na Mkurugenzi wa Uhusiano na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania PLC, Zuweina Farah (wa nne kulia), ambaye aliwakilisha Vodacom Tanzania PLC kama mdhamini mkuu wa msafara huo, wakiwa katika picha ya pamoja wakati wa mkutano na waandishi wa habari na wadau wa msafara huo uliolenga kutangaza rasmi washirika wa zamani na wapya wa msafara huo. Katika picha kutoka kushoto ni Mkurugenzi wa Afroil, Mohamed Al-Jabry(wa pili kushoto) Meneja wa Uendelevu wa Stanbic Bank Tanzania, Annette Nkini (wa tatu kushoto), Mkuu wa Masoko na Mauzo wa BYD, Samwel Msonsa (wanne kushoto), Mwanzilishi wa Nyerere Cycling Tour, Gabriel Landa, Meneja wa Akaunti wa Vodacom Huawei, Victor Wang, na Katibu Mtendaji wa Coca-Cola Tanzania, Yvette Gadi. Mkutano huo ulifanyika jijini Dar es Salaam, Septemba 11, 2026.
Baadhi ya washiriki wa msafara wa Nyerere cycling tour wakiwa katika mkutano na waandishi wa habari na wadau wa msafara huo uliolenga kutangaza rasmi washirika wa zamani na wapya wa msafara huo.
Mwanzilishi wa Nyerere Cycling Tour Gabriel Landa (wa kwanza kulia) akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari na washirika wao. Majadiliano hayo yalihusu namna gani watajumuika katika msafara huo.
 Washirika, Washiriki na Wadau wa Nyerere Cycling Tour wakiwa kwenye picha ya pamoja baada ya kuhitimisha mkutano wa waandishi wa habari uliopangwa kwa ajili ya kutangaza rasmi washirika wapya na wa zamani wa msafara huo.
Mwanzilishi wa Nyerere Cycling Tour Gabriel Landa akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari na wadau wa msafara. Mkutano huo ulilenga kutangaza rasmi washirika wa zamani na wapya wa msafara huo.

Na Mwandishi Wetu.

Nyerere Cycling Tour Watangaza Washirika wao wa mwaka 2026Nyerere Cycling Tour Imetangaza washirika wa safari ya mwaka huu itakayokuwa na umbali wa kilomita 1,500 hadi Butiama, huku Vodacom Tanzania ikiendelea kuwa mshirika mkuu wa msafara huo, ikishirikiana na Afro Oil, Stanbic Bank Tanzania, BYD, ABC Bicycle, Coca-Cola na Huawei.

Akizungumza wakati wa mkutano na waandishi wa habari, Mkurugenzi wa uhusiano na Mawasiliano wa Vodacom Tanzania, Zuweina Farah, alisema Vodacom itaendelea kushirikiana na Nyerere Cycling Tour kama mshirika mkuu, akieleza kuwa ushirikiano huo unaonesha dhamira ya kampuni ya  kuendelea kuunga mkono mipango yenye kuleta matokeo chanya kwa jamii nchini. Alisema Vodacom pia inafurahia kuwapokea washirika wapya ambao ushiriki wao utaongeza thamani katika safari ya mwaka huu na kusaidia kupanua wigo na matokeo ya msafara huo.

Msafara huo utafanyika kuanzia tarehe 5 hadi 14 Oktoba 2026, ukiwa na mkazo katika elimu, afya na uhifadhi wa mazingira, sambamba na kuhamasisha wanafunzi, hususan wasichana, kushiriki katika michezo ya kuendesha baiskeli. Katika safari ya mwaka huu, Vodacom wanatarajia kutoa madawati 1,000 kwa shule 10, kukarabati madarasa 40 na kujenga madarasa mapya 10, huku shughuli hizo zikitarajiwa kuwafikia zaidi ya wanafunzi 25,000. Katika safari zilizopita, Nyerere Cycling Tour ilifikia  shule 107 na zaidi ya wanafunzi 75,000 walinufaika.

Akizungumzia ushirika wao, Meneja wa Uendelevu wa Stanbic Bank Tanzania, Annette Mkini, alisema benki hiyo itatumia msafara huo kuhamasisha elimu ya fedha kwa wanafunzi na vijana, ili kuwajengea uelewa itakayowasaidia kufanya maamuzi bora kuhusu matumizi na usimamizi wa fedha. Kwa upande wake, Afro Oil imesema ushiriki wake unatokana na dhamira ya kampuni ya kurudisha kwa jamii, huku Samwel Msonsa kutoka BYD alisema kampuni hiyo itashiriki katika uzalishaji na uhamasishaji wa msafara huo, pamoja na shughuli za uhifadhi wa mazingira ikiwemo upandaji miti.

Msafara huo hadi sasa umesajili waendesha baiskeli 213, huku wengine wakitarajiwa kujiunga njiani. Waendesha baiskeli kutoka nchi 12 wanatarajiwa kushiriki, zikiwemo Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Malawi, Zambia, Afrika Kusini, Australia, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na Uholanzi. Aidha, wanawake 23 tayari wamesajiliwa kushiriki katika msafara huo.

Vodacom pia ilitoa taarifa kuhusu Vodacom Coastal Classic, ambayo hadi sasa imeandikisha washiriki 147. Na washindi wa nafasi ya kwanza kwa wanawake na wanaume watapata Sh milioni 10 kila mmoja, nafasi ya pili Sh milioni 7 na nafasi ya tatu Sh milioni 5. Waendesha baiskeli watakaomaliza nafasi ya nne hadi ya kumi watapata Sh milioni 1 kila mmoja.

Vodacom Tanzania imewekeza Sh milioni 160 katika Msafara wa Baiskeli wa Nyerere, huku Vodacom Foundation ikichangia zaidi ya Sh milioni 300 kwa shughuli za kijamii zitakazotekelezwa katika maeneo yatakayopitiwa na msafara huo, ikiwemo uboreshaji wa shule na utoaji wa madawati. Safari hiyo itahitimishwa Butiama, nyumbani kwa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere.
Na Mwandishi Wetu.

RAIS wa awamu ya nne , Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete, amesisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano kati ya Tanzania na Japan katika sekta za uzalishaji na usalama wa chakula, teknolojia, uvuvi na uchumi wa buluu.

Dkt. Kikwete ameyasema hayo baada ya kukutana na kufanya mazungumzo na Mtafiti Mkuu wa Taasisi ya Sasakawa Peace Foundation ya Japan, Bw. Masanori Kobayashi, katika ofisi yake ndogo iliyopo Masaki, Dar es Salaam.

Mazungumzo hayo yalilenga kufuatilia utekelezaji wa masuala mbalimbali yaliyoibuliwa wakati wa ziara ya kikazi ambayo Dkt. Kikwete alifanya nchini Japan kuanzia Julai 23 hadi 24, 2025.

Katika ziara hiyo, Dkt. Kikwete alikuwa miongoni mwa viongozi sita mashuhuri kutoka Afrika walioalikwa na Serikali ya Japan kupitia taasisi za Sasakawa Peace Foundation na Nippon Foundation.

Viongozi hao walishiriki katika kutoa ushauri kuhusu namna bora ya kuimarisha uhusiano na ushirikiano kati ya Afrika na Japan, hususan kupitia Mkutano wa Kimataifa wa Tokyo kuhusu Maendeleo ya Afrika (TICAD).

Mkutano wa tisa wa TICAD ulifanyika baadaye jijini Yokohama, Japan, kuanzia Agosti 20 hadi 22, 2025, ukiwakutanisha viongozi na wadau mbalimbali kujadili masuala ya maendeleo na ushirikiano kati ya Afrika na Japan.

Katika mazungumzo yake na Kobayashi, Dkt. Kikwete aliishukuru Serikali ya Japan, kupitia Sasakawa Peace Foundation, kwa kuendelea kudumisha na kuendeleza ushirikiano wa kihistoria uliopo kati ya Tanzania na Japan.

Alisema ushirikiano huo una umuhimu mkubwa katika kusaidia Tanzania kuimarisha mifumo ya uzalishaji, kuongeza usalama wa chakula na kutumia fursa zilizopo katika uchumi wa buluu.

Kwa mujibu wa Dkt. Kikwete, Tanzania ina fursa kubwa ya kutumia teknolojia na tafiti za kisasa kuongeza tija katika sekta zinazohusiana na bahari, maziwa na rasilimali nyingine za maji.

Alisisitiza umuhimu wa kuendeleza tafiti na kuimarisha ushirikiano katika matumizi ya teknolojia za kisasa ili kuongeza tija katika shughuli za wavuvi wadogo na ufugaji wa samaki.

Dkt. Kikwete alisema matumizi sahihi ya teknolojia yanaweza kusaidia wavuvi wadogo kuongeza uzalishaji, kuboresha ubora wa mazao ya uvuvi na kuongeza kipato, huku yakisaidia pia katika matumizi endelevu ya rasilimali za maji.


Aidha, Dkt. Kikwete alihimiza juhudi zaidi kuelekezwa katika kukuza kilimo cha mwani kwenye maeneo ya mwambao wa Tanzania, hususan Zanzibar.

Alieleza kuwa kuimarisha kilimo cha mwani kunaweza kuwa na mchango mkubwa katika kuongeza uzalishaji, thamani ya mazao na mapato ya wananchi wanaotegemea sekta hiyo kama chanzo cha ajira na kipato.

Kwa mtazamo huo, alisisitiza umuhimu wa kuangalia namna ya kuongeza thamani ya mwani badala ya kuuza zao hilo likiwa katika hali isiyosindikwa, ili wananchi waweze kunufaika zaidi na mnyororo mzima wa thamani.

Hatua hiyo pia inaweza kuongeza fursa za ajira, biashara na uwekezaji katika maeneo ya mwambao, sambamba na kuimarisha mchango wa uchumi wa buluu katika maendeleo ya Tanzania.

Kwa upande wake, Bw. Masanori Kobayashi alieleza utayari wa Sasakawa Peace Foundation kutumia nafasi na ushawishi wake kuendeleza na kuimarisha zaidi ushirikiano kati ya Tanzania na Japan.

Kobayashi alisema taasisi hiyo iko tayari kuendelea kushirikiana na Tanzania katika maeneo yenye maslahi ya pamoja, huku ikitambua umuhimu wa mahusiano ya muda mrefu yaliyopo kati ya nchi hizo mbili.

Mazungumzo hayo yanaonekana kuendelea kujenga msingi wa utekelezaji wa masuala yaliyojadiliwa wakati wa ziara ya Dkt. Kikwete nchini Japan, pamoja na kuendeleza nafasi ya Tanzania katika kukuza ushirikiano wa Afrika na Japan.

Ushirikiano huo unatajwa kuwa na umuhimu zaidi katika kipindi ambacho Tanzania inaendelea kutafuta fursa za kutumia teknolojia, tafiti na uwekezaji kuongeza tija katika kilimo, uvuvi, ufugaji wa samaki na shughuli nyingine za uchumi wa buluu.

Kwa upande mwingine, ushirikiano kati ya taasisi za Tanzania na Japan unaweza kutoa fursa zaidi za kubadilishana maarifa, teknolojia na uzoefu, hususan katika maeneo ambayo yanagusa moja kwa moja maisha ya wananchi na uchumi wa nchi.

Kwa Dkt. Kikwete, kuendeleza ushirikiano huo ni sehemu ya kuhakikisha Tanzania inanufaika zaidi na fursa zinazotokana na mahusiano yake ya muda mrefu na Japan, huku ikiendelea kushirikiana na wadau wa kimataifa katika kutafuta suluhisho la changamoto za uzalishaji, usalama wa chakula na kuongeza kipato cha wananchi.

President of the United Republic of Tanzania, Dr Samia Suluhu Hassan, has expressed her sincere gratitude to Tanzanians and people around the world for the messages of condolence, prayers, love and support following the death of her beloved husband, Mr Hafidh Ameir Hassan.

Mr Hafidh passed away in Zanzibar on September 7, 2026.

In a message of appreciation, President Samia said she and her family have been deeply touched by the kindness and compassion shown to them during this difficult period.

She extended her appreciation to Heads of State and Government, national leaders, members of the diplomatic community, religious leaders and all Tanzanians for standing with her family and providing strength and comfort as they conclude three days of mourning.

DODOMA, TANZANIA — September 8, 2026.

Day One of the Bootcamp at Msalato Girls Secondary School in Dodoma began with the girls taking an active role in the learning process.

Working in groups, the students engaged in discussions, sharing ideas and exploring different challenges that could be addressed through technology.

The discussions gave the girls an opportunity to work together, listen to different perspectives and develop ideas as a team.

After the group discussions, the students came together for presentations.

Standing before the whole class, the groups presented the ideas they had developed during their discussions, giving each student an opportunity to participate and share what her group had explored.

Through this process, the girls were beginning to build important skills in teamwork, communication, confidence and problem-solving.

It was the first practical step of the Bootcamp—moving from discussion to presentation, and creating a foundation for the hands-on technology sessions that followed.

Day One had begun with an important lesson: ideas become more powerful when they are shared, challenged and developed together.

 Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Deogratius Ndejembi, ameagwa rasmi na Menejimenti ya Wizara ya Nishati pamoja na Taasisi zilizo chini yake katika hafla iliyofanyika katika Ukumbi wa Kambarage Treasury Square, Dodoma. Jumatano Septemba 09, 2026.

Hafla hiyo imehudhuriwa na Naibu Waziri wa Nishati, Mhe. Salome Makamba, Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughukia Umeme na Nishati Jadidifu, Mhandisi Felchesmi Mramba, Menejimenti ya Wizara na Wakurugenzi wa Taasisi zilizopo chini ya Wizara hiyo.

Akizungumza katika hafla hiyo, Makamu wa Rais amewaasa Viongozi na Watendaji hao kuendelea kumwombea Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na Wasaidizi wake ili waendelee kutekeleza majukumu yao ya kuwahudumia Watanzania.

Aidha, Makamu wa Rais amewataka Viongozi na Watendaji hao kuendelea kufanya kazi kwa bidii, weledi, uaminifu na uzalendo ili kutimiza matarajio ya wananchi kwa Serikali.












Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhe. Stanslaus Haroon Nyongo, amesema ataendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wawekezaji ili kukuza uwekezaji na uchumi wa Mkoa wa Pwani, huku akisisitiza umuhimu wa kuwawezesha vijana kiuchumi.

Mhe. Nyongo amesema hayo leo, Septemba 8, 2026, wakati wa hafla fupi ya makabidhiano ya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Pwani kati yake na aliyekuwa Mkuu wa Mkoa huo, Mhe. Abubakar Mussa Kunenge, ambaye kwa sasa ni Mkuu wa Mkoa wa Songwe.

Amesema Mkoa wa Pwani ni miongoni mwa maeneo muhimu kwa uwekezaji nchini na kwamba atashirikiana na viongozi na wadau mbalimbali kuhakikisha mazingira yanaendelea kuwa rafiki kwa wawekezaji.

“Mkoa huu ni wa uwekezaji. Nimezunguka maeneo mbalimbali kutafuta wawekezaji, kwa hiyo niwakaribishe kwa kuweka mazingira wezeshi,” amesema Mhe. Nyongo.

Aidha, Mhe. Nyongo ameomba ushirikiano wa jamii katika kuwajenga na kuwawezesha vijana kukabiliana na mabadiliko ya kiuchumi yanayolenga kuboresha maisha yao na jamii kwa ujumla.

Amesema atashirikiana na viongozi wa Mkoa katika kukuza uchumi kupitia sekta mbalimbali, ikiwemo kilimo, mifugo, uchumi wa buluu pamoja na sekta nyingine za uzalishaji.

“Ninaamini utendaji wetu wa pamoja utatumika kikamilifu katika kuendelea kuwatumikia wananchi kwa kutatua changamoto zao mbalimbali, pamoja na kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla,” amesema.

Katika hatua nyingine, Mhe. Nyongo ameomba viongozi na wananchi kutumia sheria, kanuni na taratibu katika kutatua migogoro ya ardhi, akisisitiza umuhimu wa kutumia busara na haki ili kupata suluhisho la kudumu.

Ameahidi kulisimamia kwa karibu suala hilo kwa lengo la kuhakikisha migogoro ya ardhi inapungua na wananchi wanapata haki na fursa ya kuendelea na shughuli zao za kiuchumi.