TRENDING NOW





Mkurugenzi wa Vodacom Business Nguvu Kamando (kushoto), akisalimiana na Mkurugenzi wa Programu za Afrika wa Bridge for Billions, Liliosa Mbirimi (kulia), muda mfupi baada ya kutangazwa kwa ushirikiano wa miaka mitatu kati ya Vodacom Digital Accelerator (VDA) na Bridge for Billions. Ushirikiano huo unalenga kuimarisha mfumo wa ujasiriamali nchini kwa kuwafikia zaidi ya wajasiriamali na wabunifu 1,000 na kusaidia zaidi ya biashara 40 kukua na kupanuka, ushirikiano huu ulitangazwa wakati wa Wiki ya Ubunifu Tanzania (IWTz) 2026, Septemba 3 jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi wa Programu za Afrika wa Bridge for Billions, Liliosa Mbirimi (kulia), akizungumza wakati wa kutangazwa kwa ushirikiano wa miaka mitatu kati ya Vodacom Digital Accelerator (VDA) na kampuni hiyo unaolenga kuimarisha mfumo wa ujasiriamali nchini kwa kuwafikia zaidi ya wajasiriamali na wabunifu 1,000 na kusaidia zaidi ya biashara 40 kukua na kupanuka. Ushirikiano huo ulitangazwa wakati wa Wiki ya Ubunifu Tanzania (IWTz) 2026, Septemba 3 jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Mkurugenzi wa Vodacom Business Nguvu Kamando.

Mkurugenzi wa Programu za Afrika wa Bridge for Billions, Liliosa Mbirimi (kulia) akifafanua kuhusu ushirikiano mpya wa miaka mitatu kati ya Vodacom Digital Accelerator (VDA) na kampuni hiyo unaolenga kuimarisha mfumo wa ujasiriamali nchini kwa kuwafikia zaidi ya wajasiriamali na wabunifu 1,000 na kusaidia zaidi ya biashara 40 kukua na kupanuka. Ushirikiano huo ulitangazwa wakati wa Wiki ya Ubunifu Tanzania (IWTz) 2026, Septemba 3 jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Mkurugenzi wa Vodacom Business Nguvu Kamando.

Baadhi ya washiriki na wabunifu wakifuatilia uzinduzi wa ushirikiano wa miaka mitatu kati ya Vodacom Digital Accelerator (VDA) na Bridge for Billions unaolenga kuimarisha mfumo wa ujasiriamali nchini uliotangazwa wakati wa Wiki ya Ubunifu Tanzania (IWTz) 2026, Septemba 3 jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi wa Vodacom Business Biashara Nguvu Kamando, akizungumza wakati wa kutangazwa kwa ushirikiano mpya wa miaka mitatu kati ya Vodacom Digital Accelerator (VDA) na Bridge for Billions, unaolenga kuimarisha mfumo wa ujasiriamali nchini na kuwawezesha wajasiriamali na wabunifu kukua. Ushirikiano huo ulitangazwa wakati wa Wiki ya Ubunifu Tanzania (IWTz) 2026, Septemba 3 jijini Dar es Salaam. Kulia ni Mkurugenzi wa Programu za Afrika wa Bridge for Billions, Liliosa Mbirimi.

Na Mwandishi Wetu.

● Ushirikiano huu kupitia taasisi zinazosaidia wajasiriamali vyuoni unalenga kuwafikia zaidi ya wajasiriamali 1,000 na kusaidia biashara zaidi ya 40 kukua na kupanuka

Dar es Salaam, Septemba 4, 2026: Vodacom Tanzania Plc leo imetangaza kuingia katika ubia wa miaka mitatu na Bridge for Billions, mtandao wa kimataifa wa ujasiriamali, kwa lengo la kupanua wigo na kuongeza matokeo ya mpango wa Vodacom Digital Accelerator (VDA).

Katika kipindi cha miaka mitatu ya ubia huo, mashirika hayo mawili yatazijengea uwezo na kuziwezesha taasisi zinazosaidia wajasiriamali (ESOs) kote nchini Tanzania na hivyo kuwafikia zaidi ya wajasiriamali 1,000 na kusaidia biashara zaidi ya 40 kukua na kupanuka.

Ushirikiano huu unaashiria mabadiliko katika namna VDA inavyotekeleza na kuongeza matokeo yake. Pamoja na kuendelea na lengo la kusaidia biashara changa moja kwa moja, mpango huu sasa utawekeza pia katika vituo vya kulea na kukuza biashara, vituo vya ujasiriamali, vyuo vikuu na mashirika ya maendeleo ya biashara yanayowasaidia waanzilishi wa biashara kila siku. Hatua hii inalenga kuimarisha mifumo ambayo wajasiriamali nchini Tanzania wanaihitaji hata baada ya kumalizika kwa programu ya kundi fulani la washiriki.

Kupitia makubaliano hayo, Bridge for Billions italeta nchini utaalamu wake katika programu za kulea na kukuza biashara changa (incubation), teknolojia za kidijitali na uzoefu wa kujenga uwezo wa taasisi zinazosaidia wajasiriamali. Taasisi zitakazochaguliwa zitapatiwa mafunzo maalumu, zitawezeshwa kutumia zana na mifumo ya Bridge for Billions, pamoja na kupata msaada katika kubuni programu na kuziendesha.

Aidha, taasisi hizo zitaunganishwa na mtandao wa kimataifa wa washauri na taasisi zinazosaidia wajasiriamali, hivyo kuwawezesha kujifunza, kubadilishana uzoefu na kujenga mahusiano na taasisi nyingine.

Wajasiriamali watakaopatikana kupitia taasisi hizo watapitia mchakato maalumu wa kulea na kukuza biashara zao, huku biashara zitakazoonesha uwezo mkubwa wa kukua zikiendelea kwenye hatua ya acceleration, ambapo zitapatiwa msaada wa kina zaidi katika kukuza biashara na kujiandaa kwa fursa za uwekezaji.

Tangu kuzinduliwa kwake mwaka 2019, Vodacom Digital Accelerator imekuwa ikiunga mkono biashara changa na zinazokua zinazotumia teknolojia kutengeneza bidhaa na huduma zenye uwezo wa kukua, katika sekta mbalimbali ikiwemo afya, kilimo, elimu na huduma za kifedha.

Kupitia awamu mbalimbali, programu hiyo imewapatia wajasiriamali mafunzo, ushauri wa kitaalamu, teknolojia, fursa za kuunganishwa na wawekezaji, pamoja na fursa za kufikia mitandao na washirika wa Vodacom.Ubia huu wa miaka mitatu unaendeleza safari ya VDA kutoka kwenye programu zinazotekelezwa kwa awamu moja baada ya nyingine hadi kwenye uwekezaji wa muda mrefu katika kuimarisha mfumo wa ujasiriamali nchini.

Kundi la kwanza la taasisi zitakazoshiriki katika mpango huu linatarajiwa kutangazwa Oktoba 2026, huku maombi kwa wajasiriamali yakitarajiwa kufunguliwa mwishoni mwa Septemba 2026.
Benki ya Exim Tanzania imehitimisha mafunzo kwa wanawake wajasiriamali 50 waliofanikiwa kukamilisha programu ya wiki sita ya Women Empowerment Programme (WEP) 2026 jijini Dar es Salaam.

Utekelezaji wa programu hii kupitia mpango wao wa kurudisha kwa jamii wa Exim Cares unalenga kuwajengea wanawake wajasiriamali maarifa na ujuzi kwa vitendo na kuimarisha biashara zao, ikiwemo usimamizi wa fedha, uandaaji wa bajeti, kuwafahamu wateja wao, kutambua fursa za soko na kupanga mikakati ya ukuaji endelevu wa biashara.
Programu hii haiishii kwenye mafunzo pekee. Wahitimu wanaunganishwa na fursa, mitandao ya masoko pamoja na huduma za kifedha zinazoweza kuwasaidia kuchukua hatua inayofuata katika safari zao za biashara.

Wakati wakiwapongeza wanawake hao 50, Benki ya Exim inaendelea kutarajia kuona biashara zao zikikua, zikitoa fursa kwa wengine na kuleta matokeo chanya katika familia na jamii zinazowazunguka.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Dkt. Jabiri K. Bakari akizungumza wakati wa kikao cha kuhitimisha ujumbe wa timu wataalam kutoka Shirika la Usalama wa Anga la Umoja wa Ulaya (EASA).

Na Mwandishi Wetu.

Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Dkt. Jabiri K. Bakari, amethibitisha dhamira ya Mamlaka hiyo ya kujenga Mamlaka ya Usafiri wa Anga ya kiwango cha kimataifa barani Afrika, yenye matarajio ya kufikia viwango vinavyolingana na mamlaka za usafiri wa anga za Ulaya katika ubora wa udhibiti, umahiri wa kitaalamu, ufanisi wa kiutendaji na usimamizi wa usalama wa anga.

Alitoa kauli hiyo wakati wa kikao cha kuhitimisha ujumbe wa wataalamu wa msaada wa kujengeana uwezo kutoka Shirika la Usalama wa Anga la Umoja wa Ulaya (EASA), kilichofanyika tarehe 3 Septemba 2026 katika Makao Makuu ya TCAA jijini Dar es Salaam. Dkt. Bakari aliushukuru Umoja wa Ulaya kwa kuendelea kutoa msaada na kuonyesha imani katika maendeleo ya Tanzania. Pia alieleza juhudi zinazofanywa na TCAA kuimarisha mifumo yake ya usimamizi, ikiwemo uundaji na utekelezaji wa Mfumo wake wa ndani wa TCAA wa Huduma za Usafiri wa Anga (Civil Aviation Services Portal – CASP), ambao ulipewa pongezi na timu ya EASA.

Timu ya EASA ilieleza kuridhishwa kwake na maendeleo na juhudi zilizooneshwa na TCAA wakati wa ziara hiyo ya siku tatu. Aidha, timu hiyo ilitambua maendeleo yaliyofikiwa na kuhimiza TCAA kuendeleza kasi katika kushughulikia masuala yote muhimu ya usimamizi wa usalama wa anga.

Kwa upande wake Mkuu wa Ujumbe wa Umoja wa Ulaya alithibitisha dhamira ya EU ya kuendelea kuisaidia Tanzania kupitia msaada wa kitaalamu, mbinu za utekelezaji wa vitendo na kubadilishana ujuzi. Aidha, alieleza kuwa Umoja wa Ulaya umetenga Euro milioni 2 kwa ajili ya msaada unaohusiana na kuboresha zaidi Masuala ya usafiri wa anga nchini.

Ujumbe wa EASA uliongozwa na Bw. Jose Miguel Manso Angulo akiambatana na Bw. Gustavo Juan Roman Barba na Bw. Antonio Portales Pelaez.

Ujumbe huo, uliofika nchini kwa siku tatu kuanzia tarehe 1 hadi 3 Septemba 2026, ulifuatilia maendeleo ya Nchi (State) katika utekelezaji wa hatua za marekebisho pamoja na kuimarisha usimamizi wa usalama wa Usafiri wa anga. Majadiliano yalihusu maeneo ya ki sheria, muundo wa taasisi, uchunguzi wa ajali ndege, utoaji wa leseni kwa eneo la rasilimali watu la Usafiri wa anga, ubora wa ndege kwa matumizi (airworthiness) na uendeshaji wa ndege, pamoja na kufanya vikao na waendeshaji wa mashirika ya ndege kuhusu hoja zilizobainishwa, Mipango ya Hatua za Marekebisho (Corrective Action Plans) na ufuatiliaji wa utekelezaji wake.

Ujumbe huo ni sehemu ya juhudi zinazoendelea za Tanzania za kuimarisha usimamizi wa usalama wa Usafiri wa anga na kuonesha maendeleo endelevu kuelekea kutimiza matakwa ya kuondolewa kwenye Orodha ya Usalama wa Anga ya Umoja wa Ulaya (European Union Air Safety List).

Wafanyakazi wa Puma Energy Tanzania wakiwa katika picha ya pamoja huku wakipeperusha bendera, ikiwa ni ishara ya uzinduzi wa ziara ya PumaGas katika mikoa mitano nchini. Ziara hiyo imezinduliwa katika kituo cha Puma kilichopo Bunju, Dar es Salaam, tarehe 3 Septemba 2026, na itaendelea kwa wiki nane ikianzia Dar es Salaam, Pwani, Morogoro na Dodoma, kabla ya kuhitimishwa rasmi jijini Mwanza.

Dar es Salaam, 3 Septemba 2026: Puma Energy Tanzania imeanza rasmi ziara ya PumaGas itakayopita katika mikoa mitano nchini, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kampuni hiyo kusogeza huduma za gesi ya kupikia karibu na wananchi na wafanyabiashara.

Ziara hiyo imezinduliwa katika kituo kipya cha Puma Energy kilichopo Bunju, Dar es Salaam, na itaendelea kwa kipindi cha wiki nane katika mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Morogoro, Dodoma na kuhitimishwa rasmi jijini Mwanza.Kupitia ziara hiyo, Puma Energy inalenga kuwafikia watumiaji wa gesi ya kupikia katika maeneo mbalimbali, kuwapa nafasi ya kupata taarifa kuhusu matumizi ya gesi, kujifunza zaidi kuhusu bidhaa na huduma zinazopatikana, pamoja na kuwasiliana na mawakala wa PumaGas katika maeneo yao.

Ziara hiyo inabeba ujumbe wa kampeni yao ya “Hakuna Kuchochea, Tumerahisisha na PumaGas,” unaolenga kuzungumzia namna gesi ya kupikia inavyoweza kutumika katika shughuli za kila siku za kaya na biashara.
“Lengo letu si kuwaambia watu kuhusu gesi ya kupikia pekee, bali kuwapa nafasi ya kuifahamu, kuona namna inavyotumika na kupata taarifa wanazohitaji kabla ya kufanya uamuzi. Kwa kupeleka PumaGas moja kwa moja kwenye jamii, tunataka kuwa karibu zaidi na wateja wetu na kuelewa mahitaji yao katika maeneo mbalimbali,” alisema Bi. Lilian Kanora, Mkuu wa Kitengo cha Masoko wa Puma Energy Tanzania.

Katika maeneo yatakayofikiwa, timu za PumaGas zitakutana na kaya, wafanyabiashara wa chakula, migahawa, hoteli pamoja na mawakala wa gesi. Kutakuwa pia na maonesho ya matumizi ya gesi na fursa kwa wananchi kuuliza maswali kuhusu matumizi, upatikanaji na ujazaji wa gesi kwenye mitungi.

Kwa upande wa wafanyabiashara wanaotumia gesi katika shughuli zao za kila siku, ziara hiyo itatoa nafasi ya kujifunza zaidi kuhusu matumizi ya gesi katika biashara kama vile mama ntilie, watoa chipsi, migahawa na hoteli. Mawakala nao watashirikishwa katika kuimarisha upatikanaji wa bidhaa na huduma kwa wateja katika maeneo yao.

Safari hiyo itafikia kilele chake Mwanza, ambapo Puma Energy itaingia rasmi katika soko la Kanda ya Ziwa. Uzinduzi huo utahusisha hafla ya kutambulisha PumaGas katika soko hilo, kukabidhi mtungi kwa mteja wa kwanza na kumtambua wakala wa kwanza wa PumaGas katika eneo hilo, pamoja na kushirikisha wadau na vyombo vya habari.

Sehemu ya uzinduzi katika Mkoa wa Mwanza pia itahusisha maonesho ya matumizi ya gesi katika shughuli za kawaida za kila siku. Mama ntilie atapika chapati kwa kutumia mtungi wa PumaGas, huku wananchi wakipata nafasi ya kuona moja kwa moja kiasi cha chakula kinachoweza kuandaliwa kwa kutumia gesi hiyo.

Kwa Puma Energy, ziara hii ni sehemu ya mpango mpana wa kuongeza upatikanaji wa gesi ya kupikia na kuifikisha huduma hiyo kwa wananchi katika maeneo mengi zaidi nchini.

Kuanzia Dar es Salaam hadi Mwanza, ziara hiyo itachukua wiki nane kuzunguka jamii mbalimbali, kusikiliza mahitaji ya watumiaji na kuwasogezea huduma za PumaGas karibu zaidi na maeneo wanayoishi na kufanya biashara.PumaGas: Hakuna Kuchochea, Tumerahisisha.


Na Mwandishi Wetu.

Dar es Salaam, Septemba 3, 2026: Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imetoa wito kwa taasisi, kampuni, mashirika na wadau wa maendeleo kujitokeza kudhamini Samia Kalamu Awards 2026 ili kuunga mkono uandishi wa habari unaochochea maendeleo ya Taifa.

Wito huo umetolewa leo, Septemba 3, 2026, na Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, Mhandisi Peter Mwasalyanda, wakati akitangaza kufuzu kwa kazi 294 zilizoingia katika hatua ya kupigiwa kura na wananchi.

Mhandisi Mwasalyanda amesema ushiriki wa wadau kupitia udhamini ni sehemu muhimu ya juhudi za kutambua, kuenzi na kuhamasisha uandishi wa habari wenye ubora, weledi na ubunifu pamoja na maudhui yenye manufaa kwa jamii.

Amesema udhamini wa tuzo hizo utasaidia kujenga na kuimarisha mazingira yatakayowahamasisha waandishi wa habari na vyombo vya habari kuendelea kuzalisha maudhui bora, yenye taarifa sahihi na yanayozingatia maadili ya taaluma.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, kuunga mkono Samia Kalamu Awards ni kushiriki katika juhudi za kukuza uandishi wa habari unaochangia maendeleo ya kijamii, kiuchumi na kitaifa.

Katika msimu wa mwaka 2026, kazi 3,003 kutoka kwa waombaji 985 ziliwasilishwa kwa ajili ya kushindanishwa. Baada ya tathmini ya jopo la majaji, kazi 294 zilizopata alama za juu zimefuzu kuingia katika hatua ya kupigiwa kura na wananchi.

Naye Mwenyekiti Mwenza wa Mashindano hayo na Mkurugenzi wa TAMWA, Dkt. Rose Reuben, amesema mashindano hayo yamewaleta pamoja waandishi wa habari kutoka maeneo ya vijijini na mijini, akisisitiza kuwa washiriki watashindana kwa kuzingatia ubora wa kazi zao na si umaarufu wao.

Kwa mujibu wa mmoja wa majaji wa mashindano hayo, Bi. Beatrice Bandawe, amesema kuwa miongoni mwa maeneo yaliyopatiwa kipaumbele katika kazi zilizowasilishwa ni pamoja na afya, jinsia na makundi maalum, mazingira pamoja na elimu.

Tuzo za Samia Kalamu Awards zinajumuisha makundi mbalimbali yanayowapa waandishi wa habari, maafisa habari na vyombo vya habari fursa ya kushindana kupitia kazi zilizochapishwa au kurushwa ndani ya kipindi kilichobainishwa.

Tuzo hizo zinaratibiwa na TCRA kwa kushirikiana na TAMWA na JAB, chini ya kaulimbiu ya “Kalamu kwa Maendeleo.”

Mstahiki Meya wa Halmashauri ya Manispaa ya Kibaha Dr Nicas Mawazo amewataka wazazi wa Shule zilizopo Manispaa ya Kibaha kuiga  jitihada zinazofanywa na Shule zingine katika kuimarisha na kuboresha elimu kwenye Shule zao kwa kushirikiana na walimu.

Hayo ameyasema wakati wa kikao na Kamati ya Shule ya Sekondari ya Mwambisi iliyopo Kata ya Kongowe Manispaa ya Kibaha,  iliyofika katika Ofisi ya Mstahiki Meya kwa ajili ya kujadiliana na masuala mbalimbali.

Akizungumza baada ya Kamati hiyo kuwasilisha mapendekezo yao, Mstahiki Meya Dr Nicas ameipongeza Kamati hiyo kwa kazi kubwa wanayoifanya ya kuhakikisha wanafunzi wa Shule yaSekondari Mwambisi wanaendelea kufanya vizuri kwenye mitihani yao.

"Nawapongeza sana Kamati ya Shule kwa jitihada kubwa mnazofanya , Shule zingine wangekuwa wanafuata utaratibu huu unaofanywa na shule yenu tungekuwa tuna matokeo makunwa na jitihada hizi zina maana kubwa na tungekuwa tunafanya vizuri zaidi  hata hivyo zipo baadhi ya Shule zinafanya hivyo na matokeo yao yanakuwa ni mazuri," amesema Dr Nicas.

Ameongeza kuwa, Ofisi ya Mstahiki Meya itaongezea hela ya ununuzi wa mashine ya Photocopy ambapo iliyokuwepo awali imeharibika na kusababisha wanafunzi kushindwa kupata fursa ya kufanya mitihani mara kwa mara kutokana na gharama.

"Ofisi yangu itachangia kiasi cha Tshs 1,500,000/ = kwa ajili ya ununuzi wa Photocopy ili wanafunzi 1080 waliopo katika Shule ya Sekondari Mwambisi iweze kuwasaidia,"amesema Dr Nicas.

Aidha, Mstahiki Meya amesema Manispaa ya Kibaha imejipanga katika kuhakikisha inajenga miundombinu ya kutosha kwa ajili ya wanafunzi wapya na hivyo amewaasa wanafunzi na wazazi kulinda miundo mbinu hiyo ili wanafunzi wengine waje kuitumia.

Naye Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Shule ya Sekondari Mwambisi, Bw. Hamza Omari Duruge amemshukuru Mstahiki Meya wa Manispaa ya Kibaha kwa kukubali kuonana nao pamoja na kuchangia kiasi cha Tshs 1,500,000/= kwa ajili ya ununuzi wa Mashine ya photocopy ambayo iliyokuwepo imeharibika.

Duruge amesema, jambo hilo ni kubwa sana na wao kama Kamati ya Shule wataendelea kusimamia jitihada zinazofanywa na wazazi za kuhakikisha Shule ya Sekondari Mwambisi inaendelea kufanya vizuri kwenye mitihani yake inayokuja kwa kidato cha pili na kidato cha nne.

Katika kikao hicho, Mstahiki  Meya ametoa rai kwa wazazi wote kuwa serikali inayoongozwa na Rais Dkt Samia Suluhu Hassan imeendelea kujenga shule za nsingi na sekondari na Halmashauri inatoa fedha kwa ajili ya kuboresha miundo mbinu ya Shule ikiwemo madawati ya wanafunzi na ukarabati wa baadhi ya majengo.


Mkurugenzi wa Kitengo cha Mtandao wa Vodacom Tanzania Plc Andrew Lupembe (kushoto) na Mkurugenzi wa Uhusiano na Mawasiliano wa kampuni hiyo Zuweina Farah wakizungumza wakati wa uzinduzi wa Ripoti ya Mazingira, Jamii na Utawala (ESG) ya kampuni hiyo kwa mwaka wa fedha ulioishia Machi 2026, ambayo imeonesha kupungua kwa uzalishaji hewa chafu (carbon emissions) kwa asilimia 24 na uwekezaji mkubwa katika uboreshaji wa mtandao. Tukio hilo lilifanyika jijini Dar es Salaam tarehe 3 Septemba, 2026.

Mkurugenzi wa Miundombinu wa Vodacom Tanzania Plc Andrew Lupembe akizungumza na waandishi wa Habari wakati wa uzinduzi wa ripoti  ya ESG ya mwaka 2026.

Mmoja wa wasikilizaji wakati wa uzinduzi wa ripoti ya ESG akiuliza swali ili apate ufafanuzi zaidi ya namna gani matokeo ya ripoti hiyo yatakavyozidi kuwanufaisha wananchi wa Kawaida.

Baadhi ya wananchi waliohudhuria uzinduzi wa ripoti hiyo wakisikiliza ufafanuzi wa namna kampuni hiyo inavyochukulia  ESG kwa uzito unaotakiwa, wakati Vodacom ilipozindua ripoti ya ESG ya mwaka ulioishia Machi 31, 2026

Na Mwandishi Wetu.

Dar es Salaam 1 Septemba 2026: Vodacom Tanzania Plc leo imezindua ripoti ya Mazingira, Jamii na Utawala (ESG) kwa mwaka uliomalizika Machi 31, 2026, ikionesha kupungua kwa asilimia 24 ya hewa chafu, sambamba na mpango mkubwa zaidi wa uboreshaji wa mtandao katika historia ya kampuni.

Kampuni pia imewekeza shilingi 3.5 bilioni katika ufanisi wa nishati kwa mwaka huu, na kufikisha uokoaji wa megawati 18,340, ikiwa zaidi ya mara sita ya megawati 2,861 zilizookolewa kwa mwaka wa 2025. 

Uzalishaji wa hewa chafu ulishuka hadi tani 18,445.5, kutoka tani 24,285.6. Pia, matumizi ya mafuta dizeli yalipungua kwa asilimia 24, kutoka lita milioni 8.6 hadi lita milioni 6.6.

Upunguaji  huo ulitokana na kubadilisha vifaa vya zamani vya mawasiliano ya redio katika maeneo 1,808 ndani ya miezi saba, pamoja na uimarishaji wa upatikanaji wa umeme wa gridi uliopunguza muda wa uendeshaji wa jenereta katika vituo vya data vya kampuni.

Mtandao wa Vodacom Tanzania unatumia takriban jigawati (GWh) 169.5 kwa mwaka katika zaidi ya maeneo 3,800, ambapo 2,190 kati yake yapo vijijini. Vituo vya msingi vinachukua asilimia 78.9 ya matumizi yote.

Mwaka huu, maeneo 169 yaliyokuwa nje ya gridi ya taifa yaliunganishwa kwenye gridi ya taifa. Katika kituo cha data cha Kwale, umeme wa gridi ya Taifa uliongezeka kutoka 11kVA hadi 33kVA na kupunguza matumizi ya  jenereta kutoka saa 18 kwa siku hadi saa mbili, sawa na upunguzaji wa asilimia 88 wa matumizi ya dizeli katika kituo hicho.

Asilimia 57 ya nishati yote iliyotumiwa na Vodacom Tanzania ilitokana na vyanzo vya nishati jadidifu. Kampuni iliendelea kuhakikisha kuwa umeme wote wa gridi iliyonunua unaendana na nishati inayotokana na vyanzo jadidifu, hatua iliyosaidia kufikia uzalishaji sifuri wa hewa chafuzi. Aidha, Vodacom Tanzania ilihuisha tena cheti chake cha ISO 50001. Uzalishaji wa hewa chafuzi unaotokana na shughuli zake za biashara na mnyororo wake wa thamani pia ulipungua hadi tani 94,944 kutoka tani 100,455.

"Mafanikio haya ya kimazingira yametokana na kufanya uhandisi wa msingi kwa usahihi, siyo kutoka mradi tofauti wa uendelevu," alisema Mkurugenzi wa Miundombinu ya Mtandao Andrew Lupembe huku akiongeza, "kubadilisha vifaa vya zamani katika maeneo 1,808 kunampa mteja muunganisho wa haraka zaidi huku taifa likifaidika na upunguzaji wa athari za mazingira ambazo zingesababishwa na lita milioni mbili zilizopunguzwa kwenye matumizi.” 

Wigo wa mtandao wa 4G ulifikia asilimia 76.3 ya wakazi, huku wateja milioni 27.7 wakiwa kwenye mtandao baada ya uzinduzi wa huduma ya kwanza ya 5G nchini Tanzania. Umiliki wa simujanja ulifikia asilimia 46.7, huku wateja 325,415 wakipata vifaa kupitia ubia wa mikopo ya rejareja. 

Kwa wateja wasio na simujanja, huduma mpya ya kidijitali inayotumia akili unde inawezesha upatikanaji wa intaneti kupitia jumbefupi (SMS) na simu za sauti, ikisambaza msaada wa kidijitali hadi maeneo ya vijijini.

M-Pesa ilihudumia wateja milioni 14.1 wa ujumuishwaji wa kifedha huku M-Koba, jukwaa la kidijitali la vikundi vya akiba ambao wanachama wake wengi ni wanawake, lilifikia vikundi hai 299,420 huku akiba jumla ikiongezeka kwa asilimia 81.Vodacom Tanzania Foundation ilifikia wanufaika milioni 2.9, kwa kushirikiana na Taasisi ya Elimu Tanzania, kampuni iliondoa gharama ya data kwenye jukwaa la kitaifa la maendeleo ya walimu, na kuwapa walimu 121,832 fursa ya kupata nyenzo za maendeleo ya kitaaluma bila gharama ya data. Miti 80,000 ya asili iliongezwa katika Msitu wa Kahe 2 katika Mlima Kilimanjaro.

Kampuni ilirekodi mwaka wa kumi na nne mfululizo bila kutokea kifo cha mfanyakazi mahali pa kazi. Mpango wa uboreshaji ulihusisha wafanyakazi 411 waliosafiri zaidi ya kilomita milioni 1.7, na awamu ya kwanza ilikamilika bila kutokea kifo au tukio kubwa. Vodacom Tanzania ina uthibitisho wa ISO 27001 kwa usalama wa data na haikurekodi faini yoyote ya ushindani usio halali au utakatishaji fedha."Nyuma ya kila muunganisho kuna maisha yanayobadilika, mwalimu anayefikia nyenzo za kujifunzia bila gharama ya data, kikundi cha akiba ambacho hakihifadhi tena fedha taslimu katika bati. Tutaendelea kuwajibika kwa wananchi wa Tanzania wanaotuamini kila siku,” aliongeza Philip Besiimire, Afisa Mtendaji mkuu wa kampuni hiyo.


Mstahiki Meya Manispaa ya Kibaha Dr Nicas Mawazo amesema serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais Wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan inatambua mchango mkubwa wa wazee  katika taifa hili na ndio maana imeleta mpango wa Bima ya afya kwa watu wote na serikali itaanza na makundi maalumu ikiwemo watoto na wazee.

Hayo ameyasema wakati wa uzinduzi wa Jukwaa la Wazee wa Kata ya Mbwawa (JUWAKAM) ambapo amewataka kutumia jukwa hilo kujiimarisha kiuchumi na kuanzisha miradi endelevu.

Katika uzinduzi huo, Mstahiki Meya amekubali kuwa mlezi wa Jukwaa la Wazee Kata ya Mbwawa na kuwaahidi kuwa nao bega bega katika kubuni miradi yenye tija na hatosita kutafuta wadau wa maendeleo ili waweze kupata mtaji.

Dr Nicas amesema, kumekuwa na majukwaa mengi ya wazee yakianzishwa Kata tofauti ila JUWAKAM wana malengo mazuri hasa ukisikiliza risala yao ila changamoto kubwa inayokuja baadae ni uaminifu ndani ya majukwaa hayo.

Amesema, majukwaa mengi yamekuwa yanadorora na miradi iliyopo kufa na kufikia hatua hadi kuuza vitu vya miradi ila anaamini JUWAKAM watakuwa wamejipanga kuweza kusimamia miradi hiyo ikiwemo kumtafuta msimamizi ambaye atakuwa anasimamia.Kwa upande wa Mwenyekiti wa JUWAKAM Bw. Sebastian Sanga amemshukuru Mstahiki Meya wa Manispaa ya Kibaha kwa kukubali kuwa mgeni rasmi kwenye uzinduzi wa jukwaa hilo pamoja na kukubali kuwa Mlezi wa JUWAKAM, jambo ambalo litaenda kuleta chachu ya kimaendeleo wa wazee wa Kata ya Mbwawa.

Amesema, Kata ya Mbwawa ina wazee 520 ambao wanatambulika na Jukwaa, na walianza mchakato wa kuanzisha jukwaa hili mwaka 2024 na hadi kufikia 2026 wamelisanili kwa mwongozo wa mabaraza ya Kata.

JUWAKAM inalenga katika kuboresha maisha ya wazee wa Kata ya Mbwawa kwa kuanzisha Saccos ambayo watakuwa wanachangia kwa kila mwezi pamoja na kuanzisha miradi ya kiuchumi ili kutunisha mfuko wao wa Saccos.

 Na Mwandishi Wetu.

 Bodi ya Ithibati ya Waandishi wa Habari (JAB) imekutana na kufanya mazungumzo na watangazaji na waandaaji wa kipindi cha Good Morning kinachorushwa na Wasafi FM, ambapo imewakumbusha umuhimu wa kuzingatia sheria, kanuni na maadili ya uandishi wa habari katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Kikao hicho kimefanyika leo, Septemba 2, 2026, katika Makao Makuu ya JAB, Mtaa wa Jamhuri, jijini Dar es Salaam, kikilenga kuimarisha uelewa wa watangazaji hao kuhusu misingi ya weledi, uwajibikaji na matumizi sahihi ya majukwaa ya habari.

Akizungumza katika kikao hicho, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa JAB, Wakili Patrick Kipangula, amefafanua matakwa ya Sheria ya Huduma za Habari, Sura ya 229; Sheria ya Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta, Sura ya 306; pamoja na kanuni zake zinazopaswa kuzingatiwa katika utayarishaji na utangazaji wa maudhui.

Wakili Kipangula ameeleza kuwa kuzingatia sheria na maadili ni msingi wa kulinda heshima ya taaluma, haki za watu wanaohusika katika maudhui na imani ya jamii kwa Waandishi wa Habari.
Baada ya mazungumzo hayo, watangazaji wakongwe Gelard Hando na Hilary Mtuta, maarufu kama Zembwela, walikabidhiwa vitambulisho vyao vya ithibati ya uandishi wa habari baada ya kukidhi vigezo vilivyowekwa kwa mujibu wa Sheria ya Huduma za Habari.

Makabidhiano hayo yamekamilisha hatua ya kuwatambulisha rasmi kama Waandishi wa Habari wenye ithibati, wenye wajibu wa kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi, maadili na uwajibikaji.


Kutoka kushoto: Tahir Mussa, Kaimu Naibu Mkurugenzi Mkuu wa TanTrade; Juma Burhan, Mkurugenzi Mtendaji wa ZEEA; na Fatma Ahmed, Mkuu wa Huduma za Kibenki kwa Wafanyabiashara, Benki ya Stanbic, katika mkutano na waandishi wa habari uliofanyika Zanzibar jana kutangaza ushirikiano huo.
Stanbic Bank Tanzania imetangaza udhamini wa TZS milioni 200 kwa maonesho ya Fahari ya Zanzibar 2026, hatua inayoonesha dhamira yake ya kuendelea kuchangia ukuaji wa uchumi wa Zanzibar na kuwawezesha wafanyabiashara, wajasiriamali na jamii kwa ujumla.
 
Maonesho hayo yatafanyika kuanzia tarehe 4 hadi 14 Septemba 2026 katika Viwanja vya Maisara, Zanzibar, yakibeba kaulimbiu “Bidhaa Zetu Ndio Fahari Yetu.” Zaidi ya washiriki 300 na wageni 15,000 wanatarajiwa kushiriki katika tukio hilo, linalolenga kuhamasisha matumizi ya bidhaa zinazozalishwa nchini. Maonesho hayo yameandaliwa na Wakala wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi Zanzibar (ZEEA) kwa kushirikiana na Shirika la Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE).
 
Kama mdhamini mkuu, Stanbic Bank itatumia maonesho hayo kuonesha suluhisho mbalimbali za kifedha zinazolenga kusaidia ukuaji wa biashara, kuwezesha biashara za ndani na za kimataifa, pamoja na kukuza ushiriki wa wafanyabiashara katika fursa za masoko mapya.
 
Akizungumza kuhusu ushiriki wa benki hiyo, Fatma Ahmed, Mkuu wa Huduma za Kibenki kwa Wafanyabiashara, Stanbic Bank Tanzania, alisema ushirikiano huo unaakisi imani ya benki katika nafasi ya Zanzibar kama kitovu muhimu cha biashara na uwekezaji.
 
"Fahari ya Zanzibar ni jukwaa linaloonesha ubunifu, juhudi na uwezo wa wafanyabiashara wa Zanzibar. Sisi tunaendelea kujenga mazingira yatakayowasaidia kukuza biashara zao, kuongeza ushindani na kufikia masoko mapana zaidi. Zanzibar ni nyumbani kwetu, na tutaendelea kuunga mkono safari yake ya maendeleo ya kiuchumi," alisema.
 
Maonesho hayo pia yatahusisha mijadala na shughuli mbalimbali zinazolenga vijana, ubunifu, utalii, sanaa, biashara na ujumuishaji wa kiuchumi.