TRENDING NOW





Na Mwandishi Wetu

DAR ES SALAAM: Wafanyakazi wa Puma Energy Tanzania wamekutana jijini Dar es Salaam kusherehekea hatua ya kampuni hiyo kufikisha vituo 100 vya mafuta na huduma za ziada nchini, huku wakitambua mchango wao katika mafanikio hayo.

Tukio hilo lililofanyika Septemba 19, 2026, liliwakutanisha wafanyakazi kutoka idara na maeneo mbalimbali ya kampuni, ambapo walipata fursa ya kuimarisha ushirikiano na mshikamano, pamoja na kujadili mwelekeo wa kampuni na mipango ya ukuaji wa biashara.

Hatua ya kufikisha vituo 100 imekuja wakati Puma Energy Tanzania ikiendelea kutambuliwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) kwa nafasi yake katika soko la mafuta nchini kwa miaka minne mfululizo.
Akizungumza katika tukio hilo, Mkurugenzi Mtendaji wa Puma Energy Tanzania, Fatma M. Abdallah, alisema mafanikio hayo ni matokeo ya juhudi na ushirikiano wa wafanyakazi katika maeneo mbalimbali ya kampuni.

“Kufikisha vituo 100 vya mafuta na huduma za ziada ni hatua muhimu katika ukuaji wa biashara yetu, lakini pia ni matokeo ya kazi ya watu walio nyuma ya mafanikio haya. Tumefikia hapa kutokana na kujituma na ushirikiano wa wafanyakazi katika maeneo mbalimbali ya kampuni,” alisema.

Alisema tukio hilo ni fursa ya kutambua mchango wa wafanyakazi, kuimarisha mahusiano ya kikazi na kuangalia kwa pamoja hatua inayofuata katika ukuaji wa kampuni.
 
“Tunapoadhimisha kufikisha vituo 100, tunatambua pia kuwa kila hatua ya mafanikio huleta majukumu mapya. Sasa tunalenga kujenga zaidi juu ya tulichokifikia, kuimarisha ushirikiano wetu na kuendelea kuwahudumia wateja kwa ufanisi. Wafanyakazi wetu wataendelea kuwa sehemu muhimu ya safari hii,” alisema.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, kufikisha vituo 100 si tu ishara ya kupanuka kwa mtandao wa huduma za Puma Energy Tanzania, bali pia ni matokeo ya mchango wa wafanyakazi katika kuhakikisha shughuli za kampuni zinaendeshwa kwa ufanisi na huduma zinawafikia wateja katika maeneo mbalimbali nchini.

Katika tukio hilo, uongozi pia uliwashirikisha wafanyakazi kuhusu vipaumbele vya kampuni katika kipindi kijacho, hatua iliyowapa nafasi ya kuelewa mwelekeo wa biashara na nafasi yao katika kutekeleza mipango hiyo.
Puma Energy Tanzania inaendesha shughuli mbalimbali katika sekta ya nishati, ikiwemo uendeshaji wa vituo vya mafuta, usambazaji wa mafuta, huduma za mafuta ya ndege, vilainishi, LPG na lami, pamoja na nishati safi na suluhisho zinazolenga kupunguza uzalishaji wa hewa ukaa.

Puma Energy ni kampuni ya kimataifa inayojihusisha na huduma za nishati katika zaidi ya nchi 35, hasa Amerika ya Kati na Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara.
Dar es Salaam, Tanzania: The Tanzania National Commission for UNESCO and UNESCO continue to strengthen their cooperation in advancing shared priorities in education, science, culture, communication and information, and sustainable development.
The photograph was taken during an official engagement at the UNESCO Office, UN House, PSSSF Tower Complex, Dar es Salaam, reflecting the continued collaboration between the two institutions in support of UNESCO’s mandate and Tanzania’s development priorities.

Pictured from left: Prof. Hamisi Masanja Malebo, Executive Secretary, Tanzania National Commission for UNESCO; and Mr Michel Toto, UNESCO Country Representative in Tanzania.
Photo: Tanzania National Commission for UNESCO

Na Mwandishi Wetu, Dodoma.

Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Paul Christian Makonda, ametangaza kutoutambua mchakato wa kubadilisha jezi za timu za taifa, akisema umefanyika bila kuishirikisha Wizara licha ya maelekezo aliyoyatoa Februari 2026.

Sambamba na hatua hiyo, Waziri Makonda ameagiza kuundwa kwa kamati maalumu itakayochunguza mikataba ya wazabuni wa jezi hizo, manufaa yake kwa timu za taifa pamoja na mapato yanayotokana na mauzo yake.

Uamuzi huo umetangazwa siku mbili baada ya Waziri Makonda kukataa hadharani jezi mpya zilizoonekana zikivaliwa na Naibu Waziri wa Wizara hiyo, akisema hazikuwa na ubora unaoendana na hadhi ya Taifa Stars.

“Hii siyo jezi ya Taifa Stars. Taifa Stars kwa ubora wake hatuwezi kuwa na jezi za kiwango cha chini hivi. Acheni kutumia picha za Naibu wangu huku ofisi yangu haina taarifa. Tuheshimiane,” alisema Waziri Makonda kupitia mitandao ya kijamii.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Wizara leo, Septemba 18, 2026, uchunguzi huo unalenga kubaini iwapo mikataba iliyopo inanufaisha timu za taifa kwa kiwango kinacholingana na fedha nyingi zinazotolewa na Serikali kugharamia timu hizo.

Wizara imeeleza kuwa Februari 2026, Waziri Makonda alitoa maelekezo ya kuboresha jezi za timu za taifa ili ziakisi utambulisho wa Tanzania na kuzalisha manufaa mapana kwa nchi.

Hatua hiyo imeelezwa kuwa muhimu kutokana na uwekezaji mkubwa unaofanywa na Serikali katika maandalizi ya timu za taifa zinazoshiriki mashindano ya kimataifa, pamoja na Tanzania kuwa mwenyeji mwenza wa Kombe la Mataifa ya Afrika mwaka 2027 (AFCON 2027).

Kamati hiyo pia itachunguza mapato yanayotokana na mauzo ya jezi na mchango wake katika kugharamia uendeshaji wa timu za taifa.

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Majaji, Viongozi na Watumishi wa Mahakama pamoja na Wadau wa Haki Jinai wakati wa Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. Aliyeketi kushoto ni Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma na kulia ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala Ndogo Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga.
Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akitoa hotuba ya kufunga Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.




Baadhi ya Viongozi, Watumishi wa Mahakama pamoja na Wadau wa Haki Jinai wakisikiliza hotuba ya Jaji Mkuu alipokuwa akifunga Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma akitoa neno wakati wa kufunga Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya akitoa taarifa ya utekelezaji wa mikakati kwa upande wa Mahakama wakati wa Mkutano kati ya Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani uliofanyika tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. (Picha na Mary Gwera, Mahakama-Dodoma).

Na Habiba Mbaruku, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju amesema kuwa, Haki Jinai si mali ya Taasisi moja bali ni mfumo wenye Taasisi nyingi, wenye lengo la kuhakikisha haki inapatikana mapema ipasavyo kwa usawa, uadilifu na kwa kuzingatia Katiba na Sheria za nchi huku akieleza kuwa wadau wote wanapaswa kushirikiana kwa pamoja ili kuhakikisha haki haicheleweshwi bila sababu za msingi.

Mhe. Masaju ameyasema hayo wakati wa kufunga Mkutano wa Mahakama na Wadau wa Haki Kuhusu Ushirikiano na Mahusiano katika Utekelezaji Majukumu ya Utoaji Haki Mahakamani leo tarehe 17 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

“Haki jinai ni mfumo mmoja wenye taasisi nyingi lakini wenye lengo moja, yaani kuhakikisha kuwa haki inapatikana mapema ipasavyo tunapaswa kuzungumza kuhusu mfumo mzima kwa sababu udhaifu wa kiungo kimoja katika mnyororo wa haki jinai unaweza kuchelewesha haki kwa mfumo mzima,” amesema Jaji Mkuu.

Mhe. Masaju ametoa mfano wa Mtume Paulo anapozungumza kuhusu kanisa ambapo amesema, “ni kama mwili wa binadamu, kama ambavyo kuna mikono, macho, miguu, lakini hivyo vyote ndiyo vinakamilisha mwili. Yaani macho hayawezi kujifanya yenyewe ni bora kuliko mguu na vile viungo vilivyoonekana kama ni dhaifu, hivyo Mungu alivifanya kuwa vya maana zaidi lakini ukweli hapa wote hakuna kiungo dhaifu, hizi Taasisi zote ni muhimu.”

Ameongeza kuwa, jukumu la kwanza la sheria duniani kote ni kusimamia utawala wa sheria, amani na usalama katika jamii na jukumu la pili ni kukusanya kodi kwa ajili ya maendeleo mbalimbali na kuongeza kuwa hata Mwenyezi Mungu huko mbinguni aliweka sheria, na aliyekwenda kinyume na sheria aliwajibika kama ambavyo Lucifer alivyowajibika.

“Kwa hiyo, mkishakuwa zaidi ya mtu mmoja tu lazima mjiwekee sheria namna ya kufanya mambo yenu na kwetu Tanzania utawala wa sheria unapatikana katika Ibara ya 26 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na mfumo wowote lazima uwe unaongozwa na utawala wa sheria, hata Mwenyezi Mungu kule mbinguni aliweka sheria, na bwana mkubwa yule akiitwa Lucifer alipoasi akawajibika” amesema Mhe. Masaju.

Katika hatua nyingine Jaji Mkuu amefafanua kuwa, Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 inasisitiza juu ya amani, usalama na utulivu, ulinzi wa haki, uhuru wa msingi, uimara wa Taasisi na utawala wa sheria ambao ni kipengele muhimu cha utawala bora kinachosaidia kujenga jamii yenye usawa, uwajibikaji, haki na kuaminiana.

Aidha, ameeleza kuwa, mashauri ya jinai hayaanzii mahakamani wala polisi pekee kwa kuwa vyombo hivyo vyote haviwi sehemu na wakati ambapo matukio hayo ya kihalifu yanatokea hivyo, wadau wote wanapaswa kuungana na kufanya kazi kwa pamoja kama ambavyo viungo katika mwili vinavyofanya kazi kwa pamoja na kutegemeana.

“Kesi ya jinai inaanza kwenye jamii huko tukio linapotokea, inaenda kwenye vyombo vya uchunguzi iwe ni Polisi, ni Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, ni Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, inaenda Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, hatimaye kama kuna ushahidi inaenda mahakamani, na waliohusika kumkamata mshukiwa wanakuja kutoa ushahidi mahakamani kama amepatikana na hatia anarudi gerezani kwa ajili ya reform, utaona kwamba huu mnyororo ni mpana ni mnyororo mrefu lakini mnyororo imara, ” ameeleza Mhe. Masaju.

Katika hatua nyingine, amesema kuwa, ni vema kukawa na mtiririko mzuri wa kimfumo wa usimamizi wa mashauri ya jinai ili kuondoa changamoto zinazokwamisha mashauri kumalizika na kuongeza kuwa Mahakama haiwezi kuwa na ufanisi wa asilimia 100, ikiwa hatua zilizotangulia hazifanyi kazi mapema ipasavyo na kwa ufanisi na kwamba kunaweza kuwa na Mahakama yenye uwezo wa kusikiliza Mashauri Majaji na Mahakimu wenye uwezo lakini kama uchunguzi haujakamilika au kuwepo kwa changamoto yoyote shauri haliwezi kuendelea.

“Mahakama haiwezi kuwa na ufanisi wa asilimia 100 ikiwa hatua zilizotangulia Mahakama hazifanyi kazi mapema ipasavyo na kwa ufanisi. Tunaweza kuwa na Mahakama yenye uwezo wa kusikiliza mashauri, Majaji na Mahakimu wenye uwezo, na mifumo ya kielektroniki au miundombinu, lakini pia ni waadilifu. Lakini kama uchunguzi haujakamilika, jalada halijawasilishwa, mashahidi hawapatikani, maelezo hayajakamilika, hati za mashtaka zina kasoro, mshtakiwa hajaletwa mahakamani, au nyaraka muhimu hazijafikishwa mahakamani mapema, katika mtiririko kama huu kesi haiwezi kwenda mbele, hivyo ni vema kukawa na ile systematic flow ya criminal justice ya case management ili kuondoa hizo changamoto” amesisitiza Jaji Mkuu.

Akizungumza kuhusu uwajibikaji na kujituma, Mhe. Masaju amesema kuwa, kila Taasisi ya Haki Jinai inapaswa kuwajibika ipasavyo ili kuondoa ucheleweshaji wa mashauri bila kusubiri shauri lifike mahakamani huku akirejea Ibara ya 25 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo inasisitiza juu ya uwajibikaji na kujituma katika kila kazi kwa kufahamu chanzo cha kukwama kwa shauri, wapi lilipofikia katika utekelezaji, imefikia hatua zipi za ushahidi, jambo litakalosaidia mnyororo mzima wa haki jinai kufanya kazi vizuri.

Kadhalika, Mhe. Masaju amewakumbusha wadau wa Haki Jinai kwamba, mfumo unahitaji ushirikiano thabiti, mawasiliano ya karibu na uratibu mzuri ambayo ndio nguzo ya mafanikio hivyo, taasisi zote zifanye kazi bila kujitenga.

“Ni vyema tukumbuke kuwa, mfumo wetu wa haki jinai unahitaji ushirikiano thabiti (cooperation), mawasiliano ya karibu (communication), na uratibu mzuri (coordination). Hivi vitu vitatu yaani Cooperation, Communication, and Coordination ndivyo nguzo kuu za mafanikio yetu katika usimamizi wa haki jinai. Kama taasisi moja inafanya kazi kwa kujitenga au bila kutoa taarifa kwa nyingine, ni wazi kuwa, kutakuwa na kukwama kwa mashauri au kuchelewa kwa haki,” amesisitiza Jaji Mkuu.

Kadhalika, Mhe. Masaju amezitaka Taasisi za mnyororo wa Haki Jinai kuzingatia matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) na kuhakikisha mifumo inasomana ili kurahisisha mchakato mzima wa kuhakikisha haki inapatikana mapema ipasavyo bila kucheleweshwa na sababu zisizo na msingi.

Akihitimisha hotuba yake. Mhe. Masaju amezitaka Taasisi za mnyororo wa Haki Jinai kuchukua tahadhari juu ya uwepo wa mvua za El nino kwa kuhakikisha wanaweka miundombinu imara itakayowawezesha kufanya kazi pindi mvua hizo zitakapoanza kunyesha.

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya akiwasilisha Taarifa ya Mahakama Kuhusu Utekelezaji wa Mikakati kwa Wadau Wa Mashauri ya Ardhi, Kodi, Biashara, Mabenki, Ushindani wa Kibiashara na Uwekezaji wakati wa Mkutano wa Wadau hao uliofanyika tarehe 16 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (katikati), wakiwa katika Mkutano wa Wadau kuhusu Tathmini ya Utekelezaji wa Mikakati ya Mashauri ya Ardhi, Kodi, Biashara, Mabenki, Ushindani wa Kibiashara na Uwekezaji, uliofanyika tarehe 16 Septemba 2026 katika Ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, jijini Dodoma. Kulia kwake ni Kaimu Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Amir Mruma, na kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Dodoma, Mhe. Joachim Tiganga.

Majaji na Wadau wa Mahakama waliohudhuria katika Mkutano wa Wadau wa Mashauri ya Ardhi, Kodi, Biashara, Mabenki, Ushindani wa Kibiashara na Uwekezaji uliofanyika tarehe 16 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Sehemu ya Wadau wa Mahakama wakiwasilisha taarifa za utekelezaji wa mikakati iliyowekwa kuhusu mashauri ya Ardhi, Kodi, Biashara, Mabenki, Ushindani wa Kibiashara na Uwekezaji.

Na Halima Mnete- Mahakama Dodoma.

Mahakama ya Tanzania imeeleza mikakati mbalimbali inayochukua katika kuimarisha utoaji haki na kuongeza ufanisi wa kushughulikia mashauri, huku ikibainisha changamoto zinazojitokeza katika utekelezaji wa mikakati ya kuboresha mfumo wa utoaji haki nchini.

Akiwasilisha Taarifa ya Mahakama Kuhusu Utekelezaji wa Mikakati kwa Wadau wa Mashauri ya Ardhi, Kodi, Biashara, Mabenki, Ushindani wa Kibiashara na Uwekezaji katika Mkutano wa Wadau hao uliofanyika tarehe 16 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, amesema Mahakama imeendelea kutekeleza mikakati iliyowekwa kwa mafanikio kwa kushirikiana na wadau wa mnyororo wa haki.

Mhe. Nkya amesema mikakati hiyo ambayo idadi yake imefikia 10, mikakati nane inahusu Mahakama na wadau kwa pamoja, huku miwili ikiwahusu wadau pekee.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, katika kipindi cha Januari hadi Juni, 2026 Mahakama imekamilisha utekelezaji wa hukumu katika mashauri 1,290, huku kati ya Juni na Agosti, mwaka huu kukiwa na maombi 207 ya utekelezaji katika ngazi mbalimbali za Mahakama.

Aidha, Msajili Mkuu amesema, Mahakama imeendelea kuimarisha mawasiliano na wadau kupitia vikao vya (Bench-Bar), ambapo mwaka huu vikao 17 vimefanyika katika Mahakama Kuu, 23 katika Mahakama za Hakimu Mkazi na 115 katika Mahakama za Wilaya.

Katika upande wa usikilizaji wa mashauri, Mhe. Nkya anabainisha kuwa, Mahakama katika ngazi zake mbalimbali ilisikiliza jumla ya mashauri 101,879 kati ya 170,059 yaliyofunguliwa katika kipindi husika. Amesema, uwezo wa Mahakama kumaliza mashauri umefikia asilimia 95 ya idadi ya mashauri yanayofunguliwa.

Kwa upande wa mashauri ya madai, Mhe. Nkya ameeleza kwamba, jumla ya 69,911 yalisikilizwa kati ya 74,514 yaliyofunguliwa, huku mashauri 23,850 yakiwa bado Mahakamani na 1,913 yakitajwa kuwa mlundikano.

Mhe. Nkya pia amesema kuwa, Mahakama imeendelea kuhimiza matumizi ya njia za usuluhishi katika kutatua migogoro. Katika kipindi cha Juni hadi Agosti, mashauri 151 yalifanyiwa usuluhishi katika ngazi mbalimbali za Mahakama.

“Kati ya Januari na Agosti, mwaka huu Mahakama Kuu ilimaliza mashauri 181 kwa njia ya usuluhishi, Kituo cha Usuluhishi cha Mahakama Kuu kikamaliza 283, Mahakama za Hakimu Mkazi 141 na Mahakama za Wilaya 200,” ameeleza.

Msajili Mkuu huyo ameongeza kuwa, Mahakama imeweka mikakati maalum ya kushughulikia mashauri ya kimkakati ambapo Mahakama ya Rufani imepanga mashauri 300 kwa ajili ya kikao kijacho, wakati Mahakama ya Ardhi imeanza kikao maalum tangu Agosti 24 kinacholenga kumaliza mashauri 399.

Aidha, Mahakama ya Biashara imeanza kikao maalum kinacholenga kumaliza mashauri 88, huku wadau wakitakiwa kutoa ushirikiano ili mashauri hayo yakamilishwe kwa wakati.

Mhe. Nkya ameongeza kuwa, Mahakama imewezesha utekelezaji wa hukumu za mashauri 532 ya Ardhi, Biashara, Kibenki, Hifadhi ya Jamii, Kazi na Madai.

Katika upande wa matumizi ya Akili Unde, Mhe. Nkya anasema miongoni mwa changamoto alizozitaja ni matumizi yasiyofaa ya Akili Bandia (AI) na baadhi ya Mawakili kutumia katika maandalizi ya nyaraka za mashauri.

“Tayari kumekuwa na matukio kadhaa ambapo kuna hukumu ambazo hazipo zimetengenezwa kwa kutumia Akili Unde na kuwasilishwa Mahakamani kama nyaraka halisi,” amesema Mhe. Nkya na kuongeza kuwa, baadhi ya waliohusika wamechukuliwa hatua wakiwemo waliopewa onyo.

Msajili Mkuu ametaja changamoto nyingine kuwa ni pamoja na matumizi mabaya ya Kanuni 96 (7) inayoruhusu kurekebisha nyaraka za rufaa zikiwa na mapungufu, Mashauri ambayo yanatakiwa kuanza katika mamlaka nyingine kufunguliwa kwanza mahakamani, Mawakili kufungua maombi rasmi hata katika masuala ambayo wangeweza kuomba wakati shauri linaendelea mfano application for dismissal of the pending case, Baadhi ya mabenki, yanapopokea amri ya kukamata fedha (Garnishee Order Nisi).

Aidha, Mhe. Nkya ameeleza kuwa, ufanisi wa utoaji haki ni sehemu muhimu ya maendeleo ya uchumi na utekelezaji wa Dira ya Maendeleo ya Taifa ya Maendeleo, 2050 huku akitoa wito kwa Mahakama na wadau wote wa mnyororo wa haki kuendelea kushirikiana katika kuboresha mfumo wa utoaji haki nchini.
Na Mwandishi Wetu.

Dar es Salaam-Tanzania, 17 Septemba 2026: Je, umekwama katika ufanyaji wa kazi ambayo unajua kabisa hiyo siyo kwa ajili yako, na umewahi kujiuliza kama kitu ambacho una uwezo nacho ni kile ambacho unakifanya kila siku ukiwa nyumbani, njiani au kwa ajili ya kujifurahisha tu, kinaweza kuwa zaidi ya burudani?

Serengeti Lite, kinywaji pendwa cha Kampuni ya vinywaji ya Serengeti, kwa kushirikiana na KUNTA Africa, wanataka kupata jibu la swali hilo, kwa kutangaza rasmi ujio wa awamu nyingine ya Nyota Bigi msimu wa pili, ambayo inalenga kusaka nyota mkubwa ajaye wa Tanzania, katika mikoa ya Dar es salaam, Mwanza, Arusha na Dodoma. Usaili utaanza jijini Dar es salaam kuanzia tarehe 3 Oktoba, tarehe 10 safari itaendelea katika mkoa wa Mwanza, Arusha tarehe 17, na Oktoba 24 itakuwa jijini Dodoma.

Msimu wa pili wa Nyota Bigi unatafuta waimbaji, wacheza mziki, waigizaji, wachekeshaji, wabunifu, wana mitindo, na vipaji vingine vya ubunifu ambavyo Tanzania bado haijavivumbua. Mpango huu ni sehemu ya Kampeni ya Serengeti Lite ya “Lite your Imagination” inayolenga kuwahamasisha vijana kuchukulia ubunifu wao kwa uzito, kujieleza na kuona kipaji chao kinaweza kuwafikisha wapi.

Akizungumza katika uzinduzi wa msimu wa pili wa Nyota Bigi jijini Dar es salaam, Mkurugenzi wa Masoko na Ubunifu wa Kampuni ya vinywaji ya Serengeti, Henry Esiaba, alisema jukwaa hili lipo kwa ajili ya kuthibitisha kwamba vipaji viko kila mahali na Nyota Bigi ipo wa ajili ya vipaji hivyo. 

“Tuna vipaji vingi katika kila kona ya nchi hii. Ila kinachokosekana wakati mwingine ni nafasi ya kuonekana. Nyota Bigi ipo kwa ajili ya kuwapa vijana wa Tanzania jukwaa hilo. Tumerudi kwa msimu wa pili, pamoja na washirika wetu KUNTA Africa, kwa sababu tunataka kugundua vipaji zaidi, kuviweka mbele ya hadhira kubwa na kuvipa msukumo unaostahili, popote vilipo,.” Alisema Esiaba.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Bia wa Kampuni ya vinywaji ya Serengeti, Rhona Namanya, amesema kuwa msimu huu wa pili ni mkubwa zaidi na kuwa wamejikita katika kutafuta vipaji mbalimbali katika miji zaidi Tanzania kulinganisha na msimu wa kwanza mwaka jana. 
“Mwaka huu tunafurahi kuwajulisha Watanzania kuwa msimu wa pili utakwenda katika miji mbalimbali Tanzania ukilinganisha na mwaka jana ambapo tulitafuta vipaji hapa Dar es Salaam tu.  Msimu huu wa pili tutakwenda kwenye miji mingine ikiwepo Arusha, Mwanza na Dodoma. Hii inaonyesha dhamira yetu ya kukuza vipaji zaidi hapa Tanzania.” Alisema Rhona.

Usajili tayari umefunguliwa kupitia msimbo wa QR wa Nyota Bigi, tovuti ya Nyota Bigi, WhatsApp au simu. Waombaji wanapaswa kuwa na umri wa miaka 18 hadi 35, kuwa na kitambulisho halali na kuwasilisha video fupi inayoonyesha kipaji chao. Usaili utafanyika ana kwa ana na mtandaoni, hivyo kutoa njia mbalimbali kwa wenye vipaji kujitokeza.

Kwa watakaofanikiwa kuvuka hatua hiyo, Nyota Bigi inatoa fursa ya kuingia katika tasnia pana ya ubunifu, huku nafasi zikiongezeka zaidi ya mashindano yenyewe. Washiriki wanaweza kupata fursa za kuunganishwa na maeneo mbalimbali ya masoko kupitia mitandao ya kijamii, uanamitindo, burudani, usimamizi wa vipaji na studio za kurekodi, na hivyo kupata nafasi yakufanikiwa zaidi.

Kwa Serengeti Lite, Nyota Bigi inaweka “Lite Your Imagination” katika vitendo kwa kuwapa vijana nafasi ya kutoka kwenye kufikiria tu kile wanachoweza kufanya na kuanza kukiweka wazi kupitia vipaji vyao. Jukwaa hili ni sehemu ya mwendelezo wa Serengeti Lite katika kukuza ubunifu wa vijana nchini Tanzania.

Mkuu wa Idara ya Masoko na Uwezeshaji, Vodacom Business, Joseph Sayi, akizungumza na wafanyabiashara wa rejareja wa bidhaa za Tanzania Breweries PLC (TBL) wakati wa semina ya kuwajengea uwezo kupitia Mpango wa Maendeleo ya Wafanyabiashara wa Rejareja (GRIT), iliyofanyika jijini Mwanza jana. Mafunzo hayo yaliyowashirikisha wafanyabiashara 150 yalilenga kuwaongezea ujuzi katika usimamizi wa biashara, fedha na matumizi ya suluhisho za kidijitali. Semina hiyo ni sehemu ya ushirikiano wa miaka miwili kati ya TBL na Vodacom Tanzania unaolenga kuwafikia zaidi ya wafanyabiashara 24,000  nchini.
Zaidi ya wafanyabiashara 150 jijini Mwanza leo wamefanya mafunzo yanayolenga kuwajengea uwezo ili kuwasaidia kuendesha biashara zao kwa ufanisi zaidi, kusimamia fedha na kuongeza faida, kupitia Mpango wa Maendeleo ya Wafanyabiashara wa Rejareja (GRIT) unaotekelezwa na Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kwa ushirikiano na Vodacom Tanzania Plc yamewaleta pamoja wafanyabiashara kutoka maeneo mbalimbali ya jiji la Mwanza kwa ajili ya kujifunza namna ya kuboresha usimamizi wa biashara, ikiwemo kupanga matumizi ya fedha, kudhibiti bidhaa na kufanya maamuzi yanayoweza kusaidia biashara zao kukua.

Akifungua mafunzo hayo, Mkurugenzi Mtendaji wa TBL, Michelle Kilpin, alisema kuwa GRIT ni sehemu ya juhudi za kampuni hizo ili kuwawezesha wafanyabiashara wanaofanya kazi nazo kwa kuwapatia maarifa na ujuzi unaoweza kuwasaidia kusimamia biashara zao kwa ufanisi zaidi. Alisema uwezo wa kusimamia fedha, bidhaa na shughuli za kila siku ni muhimu katika kuweka biashara katika nafasi nzuri ya kukua na kuchangia maendeleo ya jamii.

Miongoni mwa wakufunzi katika mafunzo hayo ni Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) Dkt. Patrokil Kanje, aliyewafundisha washiriki namna ya kuendesha biashara kwa ufanisi, kusimamia gharama na kutambua maeneo yanayoweza kusaidia kuongeza faida.

Akizungumza katika mafunzo hayo, Dkt. Kanje aliwasisitiza wafanyabiashara kuwa na uelewa wa kina kuhusu biashara zao, hasa katika kufuatilia mauzo, gharama na faida. 
Alieleza kuwa mfanyabiashara anapaswa kufahamu si tu kiasi anachouza, bali pia gharama anazotumia na faida anayobaki nayo, kwa kuwa taarifa hizo ni muhimu katika kufanya maamuzi sahihi, kudhibiti matumizi na kupanga ukuaji wa biashara.

Kwa mfanyabiashara, changamoto ya kila siku si kuuza bidhaa pekee. Ni kuhakikisha fedha zinazopatikana zinatumika kwa uangalifu, bidhaa zinaendelea kuwepo, gharama zinasimamiwa na biashara inabaki na faida. 

Hivyo, mafunzo hayo yanaweka mkazo kwenye maarifa ambayo mfanyabiashara anaweza kuyatumia moja kwa moja katika biashara yake.Kwa upande wake Mkuu wa Idara ya Masoko na Uwezeshaji wa Vodacom Tanzania Plc Joseph Sayi, amewahimiza wafanyabiashara kutumia suluhisho za kidijitali katika shughuli zao za kila siku, akieleza kuwa teknolojia inaweza kurahisisha miamala, kusaidia usimamizi wa fedha na kuimarisha mawasiliano na wateja.

Sayi alisema matumizi sahihi ya suluhisho za kidijitali yanaweza kuwasaidia wafanyabiashara kurahisisha baadhi ya shughuli za biashara, kupata huduma kwa urahisi na kutumia taarifa katika kufanya maamuzi yanayolenga kuimarisha biashara zao.
Mafunzo haya ni sehemu ya mpango wa miaka miwili kati ya TBL na Vodacom Tanzania unaolenga kuwafikia zaidi ya wafanyabiashara 24,000 wa TBL nchini.

Kupitia GRIT, wafanyabiashara wanatarajiwa kupata ujuzi katika maeneo mbalimbali muhimu kwa uendeshaji wa biashara, ikiwemo usimamizi wa mtaji na mtiririko wa fedha, udhibiti wa bidhaa, huduma kwa wateja, ukuaji wa biashara pamoja na matumizi ya teknolojia na suluhisho za kidijitali.

Kwa wafanyabiashara walioshiriki jijini Mwanza, mafunzo hayo yanatoa fursa ya kuangalia biashara zao kwa mtazamo mpana zaidi, si kwa kuzingatia mauzo ya siku hiyo pekee, bali namna ya kujenga biashara inayoweza kusimamiwa vizuri, kukabiliana na changamoto na kukua kwa muda mrefu.

Mpango huo unatarajiwa kuendelea kuwafikia wafanyabiashara katika maeneo mbalimbali nchini, ukiweka mkazo katika kuwapa maarifa na zana zinazoweza kuwasaidia kufanya biashara kwa ufanisi zaidi katika mazingira yanayozidi kubadilika.
Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju akizungumza wakati ya kufunga Mkutano wa nne wa Wadau kuhusu Tathmini ya Utekelezaji wa Mkakati wa Kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki, Ardhi, Uwekezaji na Ushindani wa Kibiashara tarehe 16 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Sehemu ya Viongozi wa Mahakama na Wadau wengine wakiwa katika Mkutano wa nne wa Wadau kuhusu Tathmini ya Utekelezaji wa Mkakati wa Kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki, Ardhi, Uwekezaji na Ushindani wa Kibiashara tarehe 16 Septemba, 2026 uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.


Wajumbe wa Mkutano wakifuatilia hotuba ya Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju (hayupo katika picha) alipokuwa akifunga Mkutano wa nne wa Wadau kuhusu Tathmini ya Utekelezaji wa Mkakati wa Kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki, Ardhi, Uwekezaji na Ushindani wa Kibiashara tarehe 16 Septemba, 2026 uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi (kulia) akichangia jambo wakati wa Mkutano wa nne wa Wadau kuhusu Tathmini ya Utekelezaji wa Mkakati wa Kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki, Ardhi, Uwekezaji na Ushindani wa Kibiashara tarehe 16 Septemba, 2026 kwenye ukumbi wa mikutano, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma. (Picha na Mary Gwera, Mahakama).

Na Habiba Mbaruku, Mahakama-Dodoma

Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. George Masaju ametoa rai kwa wadau wanaoshughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki, Ardhi, Uwekezaji na Ushindani wa Kibiashara kuchukua tahadhari na hatua madhubuti za kukabiliana na mvua za El nino kufuatia taarifa iliyotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) juu ya uwepo wa mvua hizo kuanzia mwezi Oktoba mwaka huu.

Mhe. Masaju ametoa ushauri huo tarehe 16 Septemba, 2026 alipokuwa akifunga Mkutano wa nne wa Wadau kuhusu Tathmini ya Utekelezaji wa Mkakati wa Kushughulikia Mashauri ya Kodi, Biashara, Mabenki, Ardhi, Uwekezaji na Ushindani wa Kibiashara uliofanyika kwenye ukumbi wa mikutano, Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini Dodoma.

Akizungumza na Wadau hao, Mhe. Masaju amesema kuwa, Serikali inachukua hatua za kujikinga na kukabiliana na janga hilo hivyo, na wao wanapaswa kuchukua tahadhari kila mmoja na kutazama ni kwa namna gani wanaweza kuendeleza shughuli ikiwa mvua hizo zitakuwepo, pia kila mmoja kwa imani yake kumuomba Mwenyezi Mungu bila kusubiri kuambiwa na viongozi wa dini na pasipo kuringia kiburi cha uzima.

“Wadau wa haki mmejiandaa vipi, TLS mmeshaandaa namna gani ya kuendelea kusikiliza mashauri haya, wakati pengine njia barabarani hazifikiki, kwenye ‘Law fame’ zenu mna vyumba vya kutosha, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali na wadau wengine humu tumejiandaa namna gani, hayo ndiyo ya kutafakari, sisi wenyewe kwenye sekta hii tuchukue hatua namna gani tutaendeleza shughuli zetu kama hilo janga litakuwepo, lakini pia na kumuomba Mwenyezi Mungu atukinge alitupilie mbali hilo janga, tusiwe na kiburi cha uzima, tuone kama Mungu yupo, maji yana nguvu Ghorofa hazisaidii kitu chochote,” amesema Jaji Mkuu.

Aidha, amesisitiza juu ya maombi huku akirejea Kitabu cha Zaburi 103, kama muongozo katika maombi ambayo itawawezesha wadau kuomba kwa yale ambayo yapo nje ya uwezo wao kuyadhibiti, basi Mwenyezi Mungu kwa rehema na fadhili zake aingilie kati na kuliepusha Taifa na janga hilo kwa sababu hakuna ambaye ana kinga ya uhakika ya kujiweka salama pindi janga hilo litakapotokea.

“Sisi wengine hatuna kinga ya kutofikiwa na hayo majanga ya elnino kama yatakuwepo, yapo mengine yapo nje ya uwezo wetu, na mimi naamini uwepo wa Mwenyezi Mungu, kila mmoja hapa hakuna ambaye anakinga ya kutokufa kwa majanga, kila mmoja achukue tahadhari na kumuomba Mwenyezi Mungu, lazima tuwe tayari kumuomba kwa rehema, neema na fadhili zake kwa mujibu wa Zaburi ya 103 ambayo tunaishi kwayo, anaweza kuingilia kati akatunusuru kwakuwa hata uwezo wetu wa kujikinga na hayo majanga ni mdogo,” ameongeza Mhe. Masaju.

Katika hatua nyingine, Jaji Mkuu amebainisha changamoto ambazo zinasababisha ucheleweshaji wa usikilizaji wa mashauri ya kiuchumi, ambazo amezitaja kuwa ni changamoto zinazotokana na Mahakama yenyewe, changamoto za kisheria na changamoto zinazotokana na wadau.

Amesema kuwa, changamoto zinazotokana na Mahakama yenyewe ni hasa zile za kisheria, ambazo zinaambatana na mfumo wa kitaasisi na kushauri kuwa wadau waendelee kubaini changamoto hizo na kuzijadili kwa pamoja ili kuzipatia ufumbuzi pale ambapo mhusika amekwama kuzitatua.

Amezitaja changamoto hizo kuwa ni ufunguaji wa mashauri kwa lengo la kuchelewesha ulipaji wa madeni, ambapo watu hufungua mashauri mahakamani ili wasiwajibike kulipa deni na kuongeza kuwa, kukiwa na riba rafiki na upatikanaji wa elimu hususan elimu ya mikopo na masuala ya bima watu watapata uelewa wa kutosha na kufahamu wajibu wao na namna gani wanawajibika.

Kadhalika, ameitaja changamoto nyingine kuwa, ni matumizi ya mbinu za kiufundi ili kuchelewesha usikilizaji na uamuzi wa mashauri, hali ya kuwa Katiba imetoa muongozo wa kutofungwa kupita kiasi na masharti ya kiufundi yanayoweza kukwamisha haki kutendeka akirejelea Ibara ya 107A(2)(e) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, (1977).

“Matumizi ya mbinu za kiufundi ili kuchelewesha usikilizaji na uamuzi wa mashauri hizi (legal technicalities), wakati Katiba imetoa mwongozo kwamba tusifungwe kupita kiasi na masharti ya kiufundi yanayoweza kukwamisha haki kutendeka, hilo sharti limetajwa kwenye Ibara ya 107A(2)(e) haki inapaswa itendeke, tunapojiendekeza kwenye hizi hili tunaahirisha tu mgogoro hatuwezi kutatua mgogoro,” ameongeza Mhe. Masaju.

Pamoja na hayo, Jaji Mkuu amesema kwamba, wadau wanapaswa kuendelea kudhibiti hatua zinazochelewesha usikilizaji wa migogoro kwa kurahisisha matumizi ya notisi ya siku 90, kwa kuangalia wanaohusika kumfanya yule anayepewa notisi kutaka kushtakiwa, awajibike kuchukua hatua ambazo ni za kutatua na ikiwa ni hatua za usuluhishi wajadiliane ili kurahisisha usikilizaji wa migogoro na kuwataka wanaohusika na kuchakata notisi wawajibike ili kumaliza migogoro mapema ipasavyo.

“Wale wanaohusika na kuchakata hizo notisi zinazotolewa na watu wanaotaka kuishtaki Serikali na Taasisi zake, wawajibike kushughulikia hiyo changamoto inayopelekea watake kushtakiwa, kwa namna hiyo migogoro mingi itaisha,” amesema Mhe. Masaju.

Katika hatua nyingine, Jaji Mkuu ameongeza kuwa, uwajibikaji ni moja ya nyenzo inayotajwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050 pia ni sharti la kikatiba kama Ibara ya 25 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inavyosisitiza juu ya uwajibikaji, kujituma na kuzingatia nidhamu ili kufikia malengo yaliyowekwa, hivyo ameipongeza Tume ya Taifa ya Mipango kwa mkakati wanaouweka ili kuleta uwajibikaji.

“Uwajibikaji ni sharti la kikatiba, kitu kikishawekwa kwenye sheria tunawajibika kukitekeleza kwa sababu huwa kuna adhabu usipokitekeleza kwa hiyo Ibara ya 25 ya Katiba inatusisitiza juu ya uwajibikaji lakini pia inasisitiza juu ya kujituma na inasisitiza juu ya kuzingatia nidhamu ya kazi ili kufikia malengo tuliyojiwekea,” amesema Mhe. Masaju.

Aidha, katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA), amesema Mahakama imepiga hatua kubwa kwa kuweka mifumo mbalimbali ya matumizi ya TEHAMA huku mifumo mingine ikiendelezwa na kuwasisitiza wadau hao kuendelea kuimarisha matumizi ya TEHAMA kama yanavyosisitizwa katika Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050. Ametaja manufaa ya kutumia TEHAMA katika utendaji kuwa ni pamoja na kupunguza matumizi ya karatasi ili kuimarisha mwenendo wa mashauri, kupunguza muda na gharama za kiutawala, kuongeza uwazi na uwajibikaji, kuwezesha upatikanaji wa taarifa mapema ipasavyo na kutoa takwimu zinazoweza kusaidia katika kupanga na kupima utendaji wa Mahakama.

Akihitimisha hotuba yake, Jaji Mkuu amemtaka kila mdau wa haki kujitathmini, kubaini changamoto zake za kiuwezo, kiutendaji na kimaadili na kuzifanyia kazi ili kwa pamoja kufikia matarajio ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo, 2050.