Na Mwandishi Wetu.

Dar es Salaam-Tanzania, 17 Septemba 2026: Je, umekwama katika ufanyaji wa kazi ambayo unajua kabisa hiyo siyo kwa ajili yako, na umewahi kujiuliza kama kitu ambacho una uwezo nacho ni kile ambacho unakifanya kila siku ukiwa nyumbani, njiani au kwa ajili ya kujifurahisha tu, kinaweza kuwa zaidi ya burudani?

Serengeti Lite, kinywaji pendwa cha Kampuni ya vinywaji ya Serengeti, kwa kushirikiana na KUNTA Africa, wanataka kupata jibu la swali hilo, kwa kutangaza rasmi ujio wa awamu nyingine ya Nyota Bigi msimu wa pili, ambayo inalenga kusaka nyota mkubwa ajaye wa Tanzania, katika mikoa ya Dar es salaam, Mwanza, Arusha na Dodoma. Usaili utaanza jijini Dar es salaam kuanzia tarehe 3 Oktoba, tarehe 10 safari itaendelea katika mkoa wa Mwanza, Arusha tarehe 17, na Oktoba 24 itakuwa jijini Dodoma.

Msimu wa pili wa Nyota Bigi unatafuta waimbaji, wacheza mziki, waigizaji, wachekeshaji, wabunifu, wana mitindo, na vipaji vingine vya ubunifu ambavyo Tanzania bado haijavivumbua. Mpango huu ni sehemu ya Kampeni ya Serengeti Lite ya “Lite your Imagination” inayolenga kuwahamasisha vijana kuchukulia ubunifu wao kwa uzito, kujieleza na kuona kipaji chao kinaweza kuwafikisha wapi.

Akizungumza katika uzinduzi wa msimu wa pili wa Nyota Bigi jijini Dar es salaam, Mkurugenzi wa Masoko na Ubunifu wa Kampuni ya vinywaji ya Serengeti, Henry Esiaba, alisema jukwaa hili lipo kwa ajili ya kuthibitisha kwamba vipaji viko kila mahali na Nyota Bigi ipo wa ajili ya vipaji hivyo. 

“Tuna vipaji vingi katika kila kona ya nchi hii. Ila kinachokosekana wakati mwingine ni nafasi ya kuonekana. Nyota Bigi ipo kwa ajili ya kuwapa vijana wa Tanzania jukwaa hilo. Tumerudi kwa msimu wa pili, pamoja na washirika wetu KUNTA Africa, kwa sababu tunataka kugundua vipaji zaidi, kuviweka mbele ya hadhira kubwa na kuvipa msukumo unaostahili, popote vilipo,.” Alisema Esiaba.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Bia wa Kampuni ya vinywaji ya Serengeti, Rhona Namanya, amesema kuwa msimu huu wa pili ni mkubwa zaidi na kuwa wamejikita katika kutafuta vipaji mbalimbali katika miji zaidi Tanzania kulinganisha na msimu wa kwanza mwaka jana. 
“Mwaka huu tunafurahi kuwajulisha Watanzania kuwa msimu wa pili utakwenda katika miji mbalimbali Tanzania ukilinganisha na mwaka jana ambapo tulitafuta vipaji hapa Dar es Salaam tu.  Msimu huu wa pili tutakwenda kwenye miji mingine ikiwepo Arusha, Mwanza na Dodoma. Hii inaonyesha dhamira yetu ya kukuza vipaji zaidi hapa Tanzania.” Alisema Rhona.

Usajili tayari umefunguliwa kupitia msimbo wa QR wa Nyota Bigi, tovuti ya Nyota Bigi, WhatsApp au simu. Waombaji wanapaswa kuwa na umri wa miaka 18 hadi 35, kuwa na kitambulisho halali na kuwasilisha video fupi inayoonyesha kipaji chao. Usaili utafanyika ana kwa ana na mtandaoni, hivyo kutoa njia mbalimbali kwa wenye vipaji kujitokeza.

Kwa watakaofanikiwa kuvuka hatua hiyo, Nyota Bigi inatoa fursa ya kuingia katika tasnia pana ya ubunifu, huku nafasi zikiongezeka zaidi ya mashindano yenyewe. Washiriki wanaweza kupata fursa za kuunganishwa na maeneo mbalimbali ya masoko kupitia mitandao ya kijamii, uanamitindo, burudani, usimamizi wa vipaji na studio za kurekodi, na hivyo kupata nafasi yakufanikiwa zaidi.

Kwa Serengeti Lite, Nyota Bigi inaweka “Lite Your Imagination” katika vitendo kwa kuwapa vijana nafasi ya kutoka kwenye kufikiria tu kile wanachoweza kufanya na kuanza kukiweka wazi kupitia vipaji vyao. Jukwaa hili ni sehemu ya mwendelezo wa Serengeti Lite katika kukuza ubunifu wa vijana nchini Tanzania.

Kajunason Blog

Kajunason Blog

A Tanzanian blog operating since October 2007, covering Local News, Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers / viewers.

Toa Maoni Yako:

0 comments: