Mkurugenzi wa Vodacom Business Biashara Nguvu Kamando, akizungumza wakati wa kutangazwa kwa ushirikiano mpya wa miaka mitatu kati ya Vodacom Digital Accelerator (VDA) na Bridge for Billions, unaolenga kuimarisha mfumo wa ujasiriamali nchini na kuwawezesha wajasiriamali na wabunifu kukua. Ushirikiano huo ulitangazwa wakati wa Wiki ya Ubunifu Tanzania (IWTz) 2026, Septemba 3 jijini Dar es Salaam. Kulia ni Mkurugenzi wa Programu za Afrika wa Bridge for Billions, Liliosa Mbirimi.
Na Mwandishi Wetu.
● Ushirikiano huu kupitia taasisi zinazosaidia wajasiriamali vyuoni unalenga kuwafikia zaidi ya wajasiriamali 1,000 na kusaidia biashara zaidi ya 40 kukua na kupanuka
Dar es Salaam, Septemba 4, 2026: Vodacom Tanzania Plc leo imetangaza kuingia katika ubia wa miaka mitatu na Bridge for Billions, mtandao wa kimataifa wa ujasiriamali, kwa lengo la kupanua wigo na kuongeza matokeo ya mpango wa Vodacom Digital Accelerator (VDA).
Katika kipindi cha miaka mitatu ya ubia huo, mashirika hayo mawili yatazijengea uwezo na kuziwezesha taasisi zinazosaidia wajasiriamali (ESOs) kote nchini Tanzania na hivyo kuwafikia zaidi ya wajasiriamali 1,000 na kusaidia biashara zaidi ya 40 kukua na kupanuka.
Ushirikiano huu unaashiria mabadiliko katika namna VDA inavyotekeleza na kuongeza matokeo yake. Pamoja na kuendelea na lengo la kusaidia biashara changa moja kwa moja, mpango huu sasa utawekeza pia katika vituo vya kulea na kukuza biashara, vituo vya ujasiriamali, vyuo vikuu na mashirika ya maendeleo ya biashara yanayowasaidia waanzilishi wa biashara kila siku. Hatua hii inalenga kuimarisha mifumo ambayo wajasiriamali nchini Tanzania wanaihitaji hata baada ya kumalizika kwa programu ya kundi fulani la washiriki.
Kupitia makubaliano hayo, Bridge for Billions italeta nchini utaalamu wake katika programu za kulea na kukuza biashara changa (incubation), teknolojia za kidijitali na uzoefu wa kujenga uwezo wa taasisi zinazosaidia wajasiriamali. Taasisi zitakazochaguliwa zitapatiwa mafunzo maalumu, zitawezeshwa kutumia zana na mifumo ya Bridge for Billions, pamoja na kupata msaada katika kubuni programu na kuziendesha.
Aidha, taasisi hizo zitaunganishwa na mtandao wa kimataifa wa washauri na taasisi zinazosaidia wajasiriamali, hivyo kuwawezesha kujifunza, kubadilishana uzoefu na kujenga mahusiano na taasisi nyingine.
Wajasiriamali watakaopatikana kupitia taasisi hizo watapitia mchakato maalumu wa kulea na kukuza biashara zao, huku biashara zitakazoonesha uwezo mkubwa wa kukua zikiendelea kwenye hatua ya acceleration, ambapo zitapatiwa msaada wa kina zaidi katika kukuza biashara na kujiandaa kwa fursa za uwekezaji.
Tangu kuzinduliwa kwake mwaka 2019, Vodacom Digital Accelerator imekuwa ikiunga mkono biashara changa na zinazokua zinazotumia teknolojia kutengeneza bidhaa na huduma zenye uwezo wa kukua, katika sekta mbalimbali ikiwemo afya, kilimo, elimu na huduma za kifedha.
Kupitia awamu mbalimbali, programu hiyo imewapatia wajasiriamali mafunzo, ushauri wa kitaalamu, teknolojia, fursa za kuunganishwa na wawekezaji, pamoja na fursa za kufikia mitandao na washirika wa Vodacom.Ubia huu wa miaka mitatu unaendeleza safari ya VDA kutoka kwenye programu zinazotekelezwa kwa awamu moja baada ya nyingine hadi kwenye uwekezaji wa muda mrefu katika kuimarisha mfumo wa ujasiriamali nchini.
Kundi la kwanza la taasisi zitakazoshiriki katika mpango huu linatarajiwa kutangazwa Oktoba 2026, huku maombi kwa wajasiriamali yakitarajiwa kufunguliwa mwishoni mwa Septemba 2026.
Toa Maoni Yako:
0 comments: